Yos 21:20-45
Yos 21:20-45 SUV
Na jamaa za wana wa Kohathi, Walawi, hao wana wengine wa Kohathi waliosalia, wao walikuwa na miji ya kura yao katika kabila ya Efraimu. Nao wakawapa Shekemu pamoja na malisho yake, katika nchi ya vilima ya Efraimu, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji; na Gezeri pamoja na malisho yake; na Kibisaumu pamoja na malisho yake, na Beth-horoni pamoja na malisho yake, miji minne. Tena katika kabila ya Dani Elteke pamoja na malisho yake, na Gibethoni pamoja na malisho yake; na Aiyaloni pamoja na malisho yake, na Gath-rimoni pamoja na malisho yake; miji minne. Tena katika hiyo nusu ya kabila ya Manase, Taanaki pamoja na malisho yake, na Gath-rimoni pamoja na malisho yake; miji miwili. Miji yote ya jamaa za wana wa Kohathi waliosalia ilikuwa ni miji kumi, pamoja na malisho yake. Tena wana wa Gershoni, katika jamaa za Walawi, waliwapa, katika hiyo nusu ya kabila ya Manase, Golani katika Bashani pamoja na malisho yake, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji; na Beeshtera pamoja na malisho yake; miji miwili. Tena katika kabila ya Isakari, Kishioni pamoja na malisho yake, na Daberathi pamoja na malisho yake; na Yarmuthi pamoja na malisho yake, na Enganimu pamoja na malisho yake; miji minne. Tena katika kabila ya Asheri, Mishali pamoja na malisho yake, na Abdoni pamoja na malisho yake; na Helkathi pamoja na malisho yake, na Rehobu pamoja na malisho yake; miji minne. Tena katika kabila ya Naftali, Kedeshi katika Galilaya pamoja na malisho yake, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji, na Hamoth-dori pamoja na malisho yake, na Kartani pamoja na malisho yake; miji mitatu. Miji yote ya Wagershoni kwa kuandama jamaa zao ilikuwa ni miji kumi na mitatu, pamoja na malisho yake. Tena jamaa za wana wa Merari, hao Walawi waliosalia, katika kabila ya Zabuloni, Yokneamu pamoja na malisho yake, na Karta pamoja na malisho yake, na Dimna pamoja na malisho yake, na Nahalali pamoja na malisho yake; miji minne. Tena katika kabila ya Reubeni, Bezeri pamoja na malisho yake, na Yahasa pamoja na malisho yake, na Kedemothi pamoja na malisho yake, na Mefaathi pamoja na malisho yake; miji minne. Tena katika kabila ya Gadi Ramothi katika Gileadi pamoja na malisho yake, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji, na Mahanaimu pamoja na malisho yake; na Heshboni pamoja na malisho yake, na Yazeri pamoja na malisho yake; jumla yake miji minne. Miji hiyo yote ilikuwa ni miji ya wana wa Merari kwa kuandama jamaa zao, ni hizo jamaa za Walawi zilizosalia; na kura yao ilikuwa ni miji kumi na miwili. Miji yote ya Walawi iliyokuwa kati ya milki ya wana wa Israeli ilikuwa ni miji arobaini na minane, pamoja na malisho yake. Miji hiyo kila mmoja ulikuwa pamoja na malisho yake, yaliyouzunguka pande zote; ndivyo ilivyokuwa katika miji hiyo yote. Basi BWANA aliwapa Israeli nchi hiyo yote, ambayo aliapa kwamba atawapa baba zao; nao wakaimiliki, na kukaa mumo. Kisha BWANA akawapa raha pande zote, sawasawa na hayo yote aliyokuwa amewaapia baba zao; wala katika adui zao wote hakusimama hata mtu mmoja miongoni mwao mbele zao; yeye BWANA akawatia adui zao wote mikononi mwao. Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.