Walawi 26
26
Baraka kwa watiifu
(Kumb 7.12-24; 28.1-14)
1Musijitengenezee sanamu za miungu ya uongo, musishike sanamu zao za kuchongwa wala nguzo wala sanamu za mawe yaliyochongwa katika inchi yenu na kuviabudu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. 2Mushike Sabato zangu na kuheshimu Pahali pangu Patakatifu. Mimi ni Yawe.
3Kama mukifuata masharti yangu na kushika amri zangu, #Ang. Kumb 11.13-15; 28.1-14 4nitawanyeshea mvua kwa wakati unaofaa, inchi ipate kuzaa mavuno kwa wingi, nayo miti ya mashamba matunda yake. 5Kupepeta ngano kutaendelea mpaka wakati wa kuvuna zabibu, na mavuno ya zabibu mpaka wakati wa kupanda mbegu. Mutakuwa na chakula tele na kuishi kwa usalama katika inchi yenu. 6Nitawapa amani katika inchi hata muweze kulala bila kuogopeshwa na chochote. Nitaondoa nyama wakali katika inchi na inchi yenu haitapatwa na vita. 7Mutafukuza waadui zenu na kuwaua kwa upanga. 8Watano wenu watafukuza waadui mia moja na mia moja wenu watafukuza waadui elfu kumi. Waadui zenu wataangamia mbele yenu kwa upanga. 9Nitawarehemu na kuwajalia mupate watoto wengi na kuongezeka. Nami nitaliimarisha agano langu nanyi. 10Wakati wa mavuno mutakuwa mungali munakula mazao ya zamani. Tena itawapasa kuondoa yaliyobaki kwa kupata nafasi ya kulinda mavuno mapya. 11Nitaweka makao yangu kati yenu, wala sitawaachilia. 12Nitatembea kati yenu na kuwa Mungu wenu nanyi mutakuwa watu wangu. #Ang. 2 Kor 6.16 13Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi musikuwe watumwa wa Wamisri. Mimi nimevunja nira muliyofungiwa katika shingo lenu na kuwafanya mutembee wima.
Laana
(Kumb 28.15-68)
14Lakini kama hamutanisikiliza wala kufuata amri zangu, 15kama mukizarau masharti yangu na kuchukia kwa roho maagizo yangu mukiacha kutii amri zangu zote na kuvunja agano langu, 16basi, mimi nitafanya hivi: Nitawapiga kwa kuwaletea hofu kubwa ya rafla, kifua kikubwa na homa itakayowapofusha macho na kuwakondesha. Mutapanda mbegu zenu bila mafanikio maana waadui zenu ndio watakaozikula. 17Mimi nitawashambulia, nanyi mutapigwa na waadui zenu. Mutatawaliwa na wale wanaowachukia. Mutatishwa na kukimbia hata kama hakuna mutu yeyote anayewafukuza. 18Na kama hata kisha kuazibiwa hivyo hamutanisikiliza, basi, nitawaazibu mara saba zaidi kwa ajili ya zambi zenu. 19Kiburi chenu nitakivunja kabisa kwa kufanya mbingu kule juu kuwa ngumu kama chuma na inchi yenu bila mvua ikuwe ngumu kama shaba. 20Mutatumia nguvu zenu bure maana mashamba yenu hayatatoa mavuno na inchi yenu haitazaa matunda.
21Kama mukiendelea kunipinga na kukataa kunisikiliza, nitazidisha tena azabu yenu mara saba kadiri ya wingi wa zambi zenu. 22Nitaleta nyama wakali kati yenu ambao watawanyanganya watoto wenu na kula mifugo yenu na kupunguza hesabu yenu hata njia zenu zigeuke kama jangwa.
23Kama hata kisha azabu hiyo bado hamunigeukii mimi, lakini munazidi kupingana nami, 24basi, nami nitapingana nanyi na kuwaazibu mara saba zaidi kwa ajili ya zambi zenu. 25Nitawaletea upanga ambao utalipiza kisasi juu ya agano mulilovunja. Ninyi mutakimbilia katika miji yenu, lakini nitawaletea ugonjwa mukali na kuwatia katika mikono ya waadui zenu. 26Chakula chenu nitakipunguza hata wanawake kumi watumie mafika moja tu kwa kupika mikate. Watawagawanyia mukate wenu kwa kipimo. Na hata kisha kula mutaendelea kuwa na njaa tu.
27Na kama hata kisha hayo yote bado hamutanisikiliza mukiendelea kunipinga, 28basi nami nitapingana nanyi kwa hasira kali, na kuwaazibu mimi mwenyewe mara saba zaidi kwa ajili ya zambi zenu. 29Halafu mutakula watoto wenu, wanaume na wanawake. 30Nitaharibu pahali penu pa ibada kule juu ya milima, nitabomoa mazabahu zenu za kufukizia ubani, na kutupa maiti zenu juu ya sanamu za miungu yenu. Roho yangu itawachukia kabisa. 31Miji yenu nitaiteketeza, pahali penu patakatifu nitapafanya jangwa na harufu zenu nzuri za sadaka sitazikubali. 32Nitateketeza inchi yenu hivyo kwamba hata waadui wanaohamia mule watashangaa. 33Nitawatawanya ninyi kati ya watu wa mataifa na kuchomoa upanga juu yenu. Inchi yenu itakuwa ni ukiwa na miji yenu uharibifu.
34Ninyi mutakapokuwa katika mikono ya waadui zenu, halafu inchi itafurahia Sabato zake wakati itakapokuwa katika hali ya ukiwa. Inchi itapumzika na kufurahia Sabato zake. 35Kadiri itakapokuwa katika hali ya ukiwa, itapata sehemu ambayo haikupata katika Sabato zenu mulipokuwa mukiishi mule. 36Na kwa njia ya wamoja wenu watakaobaki nitaleta woga ndani ya moyo wao, katika inchi ya waadui zao hata jani linalopeperushwa litawakimbiza. Watakimbia kama mutu anayekimbia vita. Watakimbia na kuanguka hata kama hakuna mutu anayewafukuza. 37Wataangukiana ovyo kama mutu anayekimbia vita hata kama hakuna anayewafukuza. Hamutakuwa na nguvu yoyote kwa kuwashambulia waadui zenu. 38Mutaangamia kati ya mataifa na inchi za waadui zenu zitawameza. 39Kama wamoja kati yenu wakibakia katika inchi za waadui zenu watakonda na kuisha kwa sababu ya uovu wao na kwa sababu ya uovu wa wazee wao.
40Lakini kama wakitubu uovu wao na uovu wa wazee wao juu ya uasi waliotenda juu yangu na vilevile juu ya kupingana kwao nami, 41wakitambua kwa nini nilipingana nao na kuwapeleka katika inchi ya waadui zao, kama kweli moyo wao mugumu ukinyenyekea na kutubu uovu wao, 42basi, hapo nami nitakumbuka agano langu na Abrahamu, Isaka na Yakobo na kukumbuka ile inchi niliyowaahidia. #Ang. Mwa 17.7-8; 26.3-4; 28.13-14
43Wakati watakapokuwa inje ya inchi yao, inchi hiyo itafurahia Sabato zake hapo itakapokuwa katika hali ya ukiwa. Wakati huo wao watatubu uovu wao wa kuzarau maagizo yangu na kuchukia masharti yangu. 44Lakini, kwa hayo yote, wanapokuwa katika inchi ya waadui zao, mimi sitawatupa wala kuwachukia hata kuwaangamiza kabisa na kuvunja agano langu. 45Hapana! Kwa ajili yao nitakumbuka agano nililofanya na wazee wao ambao niliwatoa katika inchi ya Misri, mataifa yakishuhudia, kusudi mimi nikuwe Mungu wao. Mimi ni Yawe. 46Hayo ndiyo masharti, maagizo na sheria ambazo Yawe aliwapa watu wa Israeli kule kwenye mulima Sinai kwa njia ya Musa.
Currently Selected:
Walawi 26: SWC02
Highlight
Share
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.