YouVersion Logo
Search Icon

Walawi 23

23
1Yawe akamwambia Musa: 2Uwaambie Waisraeli hivi: Katika sikukuu zangu mimi Yawe ambazo zimepangwa mutakuwa na mukutano mutakatifu. Sikukuu ambazo nimepanga ni hizi: 3Kutakuwa siku sita za kufanya kazi. Lakini siku ya saba ni Sabato. Siku hiyo ni ya mapumziko, hamutafanya kazi na mutakuwa na mukutano mutakatifu. Siku hiyo ya saba hamutafanya kazi. Hiyo ni Sabato ambayo ni takatifu kwangu mimi Yawe katika makao yenu yote. #Ang. Kut 20.8-10; 23.12; 31.15; 34.21; 35.2; Kumb 5.12-14
4Sikukuu zingine zangu mimi Yawe ambazo mutakuwa na mukutano mutakatifu zitafanyika katika wakati huu uliopangwa.
Sikukuu ya Pasaka
(Hes 28.16-25)
5Magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza mutafanya kwa heshima yangu mimi Yawe sikukuu ya Pasaka. #Ang. Kut 12.1-13; Kumb 16.1-2 6Siku ya kumi na tano ya mwezi huohuo, sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu itaanza. Kwa muda wa siku saba, mutakula mikate isiyotiwa chachu. #Ang. Kut 12.14-20; 23.15; 34.18; Kumb 16.3-8 7Katika siku ya kwanza mutakuwa na mukutano mutakatifu. Siku hiyo musifanye kazi. 8Kwa muda wa siku hizo zote saba mutanitolea mimi Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto. Katika siku ya saba mutafanya mukutano mutakatifu. Musifanye kazi.
9Yawe akamwambia Musa: 10Uwaambie Waisraeli hivi: Mutakapoingia katika inchi ambayo ninawapa na kuvuna mazao yake, mutamuletea kuhani muganda wa mavuno ya kwanza. 11Kuhani atafanya nayo kitambulisho cha kunitolea siku inayofuata siku ya Sabato kusudi mupate kukubaliwa. 12Siku hiyo munapofanya kitambulisho cha kutoa huo muganda mbele yangu mutanitolea mimi Yawe sadaka ya kuteketezwa ya mwana-kondoo dume wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema. 13Pamoja na sadaka hiyo, mutatoa sadaka ya vyakula ya kilo mbili za unga laini uliochanganywa na mafuta ambayo mutanitolea mimi Yawe kwa moto, na harufu yake itanipendeza. Sadaka yake ya kinywaji ni litre moja ya divai. 14Mbele ya siku hiyo ya kuniletea mimi Mungu wenu sadaka hiyo, hamuruhusiwi kula mazao ya kwanza ya mavuno yenu, yakuwe mabichi, yamekaangwa au yemepikwa kuwa mikate. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu pahali popote mutakapoishi.
Sikukuu ya mavuno
(Hes 28.26-31; Kumb 16.9-12)
15Mutahesabu majuma saba kamili tangu siku ile inayofuata Sabato ile ambapo mutaleta muganda wa sadaka ya kunitolea kwa kitambulisho mimi Yawe. #Ang. Kut 23.16; 34.22; Kumb 16.9-12 16Katika siku ya makumi tano, siku ya pili ya Sabato ya saba, mutanitolea mimi Yawe sadaka ya vyakula vipya. 17Kila jamaa italeta mikate miwili ya sadaka ya kutoa kwa kitambulisho mbele yangu mimi Yawe. Kila mukate utatengenezwa kwa kilo mbili za unga laini uliotiwa chachu na huo mutanitolea mimi Yawe ukiwa ni matoleo ya malimbuko yenu. 18Pamoja na hayo, mutatoa wana-kondoo saba wa mwaka mumoja, mwana-ngombe dume mumoja, na kondoo dume wawili. Nyama hao watakuwa sadaka ya kuteketezwa pamoja na sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji. Harufu ya sadaka hizi itanipendeza mimi Yawe. 19Mutatoa beberu mumoja wa sadaka kwa ajili ya zambi na wana-kondoo dume wawili wa mwaka mumoja kwa ajili ya sadaka za amani. 20Kuhani atavipitisha mbele yangu mimi Yawe vikuwe sadaka ya kutoa kwa kitambulisho pamoja na mukate wa mavuno ya kwanza na wale wana-kondoo wawili. Vitu hivyo ni vitakatifu kwa Yawe navyo vitakuwa kwa matumizi ya kuhani tu. 21Siku hiyohiyo mutatoa tangazo ya mukutano mutakatifu. Musifanye kazi. Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu vyote, katika makao yenu.
22Unapovuna mavuno yako katika shamba, usivune kabisa mpaka kwenye mupaka wa shamba lako wala usirudi nyuma kukusanya mabaki. Utawaachia hayo wamasikini na wageni. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. #Ang. Law 19.9-10; Kumb 24.19-20
Sikukuu ya mwaka mupya
(Hes 29.1-6)
23Yawe akamwambia Musa: 24Uwaambie watu wa Israeli hivi: Siku ya kwanza ya mwezi wa saba mutafanya siku ya mapumziko, siku ya ukumbusho itakayotangazwa kwa mulio wa baragumu na kufanya mukutano mutakatifu. 25Musifanye kazi siku hiyo na munitolee mimi Yawe sadaka ya kuteketezwa kwa moto.
Siku ya upantanisho
(Hes 29.7-11)
26Yawe akamwambia Musa: #Ang. Law 16.29-34 27Siku ya kumi ya mwezi huu wa saba ni siku ya upatanisho. Siku hiyo ni siku ya kuwa na mukutano mutakatifu. Mutafunga kula na kutoa sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. 28Musifanye kazi zenu zozote za kawaida siku hiyo. Siku hiyo ni siku ya upatanisho, siku ya kuwafanyia ninyi upatanisho mbele ya Yawe, Mungu wenu. 29Mutu yeyote asiyefunga kula siku hiyo ni lazima atengwe mbali na watu wake. 30Mutu yeyote atakayefanya kazi yoyote siku hiyo nitamwangamiza kutoka watu wake. 31Musifanye kazi: hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu, na katika makao yenu yote. 32Siku hiyo, itakuwa kwenu Sabato ya mapumziko na mutafunga. Siku ya Sabato ni siku ya kumi ya mwezi huo tangu magaribi mpaka magaribi inayofuata.
Sikukuu ya vibanda
(Hes 29.12-39; Kumb 16.13-17)
33Yawe akamwambia Musa: #Ang. Kumb 16.13-15 34Uwaambie Waisraeli hivi: Tangu siku ya kumi na tano ya mwezi huo wa saba mutafanya sikukuu ya vibanda kwa muda wa siku saba kwa heshima ya Yawe. 35Siku ya kwanza ya siku hizo saba, mutakuwa na mukutano mutakatifu na musifanye kazi. 36Kwa muda wa siku saba mutatoa sadaka Yawe anazopewa kwa moto. Siku ya nane mutakuwa na mukutano mutakatifu na kumutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa. Mukutano huo ni mutakatifu. Siku hiyo musifanye kazi.
37Hizo ndizo sikukuu za Yawe zilizopangwa ambazo mutatoa tangazo kuwe mukutano mutakatifu wa kumutolea Yawe sadaka zinazotolewa kwa moto, sadaka za kuteketezwa na sadaka za vyakula, matoleo na sadaka za kinywaji, kila moja kwa siku yake yenyewe. 38Sadaka hizo ni pamoja na zile munazonitolea mimi Yawe siku ya Sabato kama vile na sadaka zenu za kawaida, sadaka za kutimiza viapo vyenu, na sadaka zenu za mapenzi munazonitolea mimi Yawe.
39Kisha kuvuna mashamba yenu mutafanya sikukuu kwa muda wa siku saba, tangu siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba. Siku ya kwanza itakuwa siku ya mapumziko na hata siku ya nane. 40Katika siku ya kwanza mutatwaa matunda ya miti yenu mizuri, matawi ya ngazi, matawi yenye majani mengi na matawi ya miti inayoota kandokando ya muto, nanyi mutafanya sikukuu mbele ya Yawe, Mungu wenu kwa siku saba. 41Kila mwaka munapaswa kufanya sikukuu hii kwa muda wa siku saba kwa heshima ya Yawe. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu. Mutaifanya katika mwezi wa saba. 42Kwa muda wa siku saba mutaishi katika vibanda. Wakaaji wote wa Israeli wataishi katika vibanda wakati huo. 43Jambo hilo litajulisha vizazi vyenu kwamba nilipowatoa babu zenu katika inchi ya Misri, niliwafanya waishi katika vibanda. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. 44Musa akawatangazia Waisraeli sikukuu za Yawe zilizopangwa.

Currently Selected:

Walawi 23: SWC02

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in