Isaya 54
54
Upendo wa Mungu kwa Israeli
1Yawe anasema hivi:
Imba kwa shangwe, ewe unayekuwa tasa,
wewe ambaye haujapata kuzaa!
Piga kelele na kuimba kwa nguvu,
wewe usiyepata kuzaa mutoto.
Maana watoto wako wewe uliyeachwa
watakuwa wengi kuliko wa yule anayekuwa na mume. #Ang. aya iliyorudiliwa katika Gal 4.27.
2Panua nafasi katika hema yako,
ongeza mapazia ya makao yako,
usijali mali unayotumia.
Urefushe kamba zako,
na kuimarisha misumari yako;
3maana utapanuka kila upande;
wazao wako watarizi mataifa,
miji iliyokuwa ukiwa itajaa watu.
4Usiogope, hautapata haya tena.
Usifazaike, hautazarauliwa tena.
Utaisahau haya uliyopata katika ujana wako,
wala hautakumbuka tena mazarau ya ujane wako.
5Muumba wako atakuwa mume wako.
Jina lake Yawe wa majeshi.
Mukombozi wako ni Mutakatifu wa Israeli.
Yeye anaitwa Mungu wa Ulimwengu Wote.
6Yerusalema, Yawe amekuita tena.
Ulikuwa kama vile muke aliyeachwa na kuhuzunika.
Mungu wako anasema:
Muke aliyeolewa akiwa kijana, anaweza kuachiliwa?
7Nilikuacha kwa muda mufupi tu.
Kwa huruma nyingi, nitakurudisha.
8Kwa hasira nyingi nilikuficha uso wangu kwa muda kidogo,
lakini kwa wema wa milele nitakuonea huruma.
Ni Yawe Mukombozi wako anayesema hivyo.
9Nitafanya kama nilivyofanya wakati wa Noa.
Wakati ule niliapa kwamba
sitaifunika tena dunia kwa mafuriko ya maji.
Basi sasa ninaapa kwamba sitakukasirikia tena
wala sitakukaripia tena. #Ang. Mwa 9.8-17
10Milima inaweza kutoweka,
vilima vinaweza kuondolewa,
lakini rehema zangu kwako sitaziacha,
agano langu la amani litaimarishwa.
Ni Yawe anayekuhurumia anayesema hivyo.
Yerusalema mupya
11Ewe Yerusalema, uliteseka,
ulitaabishwa na kukosa wa kukufariji,
lakini nitakujenga upya kwa mawe ya bei kali,
misingi yako itakuwa ya mawe ya yakuti. #Ang. Ufu 12.18-21
12Minara yako nitaijenga kwa mawe ya akiki,
milango yako kwa almasi,
na ukuta wako kwa mawe ya bei kali.
13Watu wako watafundishwa nami Yawe,
wana wako watapata ustawi mwingi. #Ang. Yn 6.45
14Utaimarishwa katika haki,
mbali na kaoneo,
nawe hautaogopa kitu;
mbali na hofu,
maana haitakukaribia.
15Mutu yeyote akikuja kukushambulia,
hatakuwa ametumwa nami.
Yeyote atakayekushambulia,
ataangamia mbele yako.
16Mimi ndiye niliyemwumba mufuaji wa vyuma,
anayewasha moto wa makaa na kufua silaha.
Ni mimi vilevile niliyemwumba mwangamizaji anayeangamiza.
17Silaha zote zilizotengenezwa kwa kukuzuru wewe
hazitafaa kwa kitu chochote.
Mutu akikushitaki, utamushinda.
Hiyo ndiyo haki niliyowapangia watumishi wangu.
Hizo ndizo haki nilizowahakikishia.
–Ni ujumbe wa Yawe.
Currently Selected:
Isaya 54: SWC02
Highlight
Share
Compare
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.