Kutoka 21
21
Maagizo juu ya watumwa
(Kumb 15.12-18)
1Haya ndiyo maagizo utakayowapa Waisraeli: 2Ukimununua mutumwa Mwebrania, atakutumikia kwa miaka sita, lakini mwaka wa saba atakuwa huru na kuondoka, bila malipo. #Ang. Law 25.39-46 3Kama alinunuliwa mbele hajaoa, ataondoka peke yake. Lakini kama alikuja na muke wake, basi, ataondoka na muke wake. 4Kama bwana wake alimwoea muke, akamuzalia watoto wanawake au wanaume, basi, yule mwanamuke na watoto wake watakuwa mali ya yule bwana wake na yule mutumwa ataondoka peke yake. 5Lakini kama mutumwa yule akisema kwamba anamupenda bwana wake, muke wake na watoto wake na hataki kuondoka na kuwa huru, 6basi, bwana wake atamuleta mbele ya Mungu. Kisha atamupeleka kwenye mulango au kwenye kizingiti na kumutoboa sikio lake kwa chuma chenye kuchongwa. Naye atamutumikia bwana wake maisha yake yote.
7Mutu akimwuzisha binti yake kuwa mujakazi, yule hatapata uhuru wake kama watumwa wanaume. 8Ikiwa yule bwana wake alimununua akuwe mumoja wa wake zake, kisha asipendezwe naye, yule bwana ataacha baba ya yule mujakazi amukomboe. Yule bwana hana haki ya kumwuzisha kwa watu wa mataifa mengine, akiwa amemudanganya. 9Kama ataamua kumwoesha kwa mwana wake, atamutendea mujakazi yule kama vile binti yake. 10Kama yule bwana akioa muke mwingine, anapaswa kuendelea kumutosheleza muke wake wa kwanza kwa chakula, nguo na haki zake za ndoa. 11Ikiwa yule bwana hatamutimizia haki hizo tatu, basi, muke ataondoka na kuwa huru bila malipo yoyote.
Maagizo juu ya uasi
12Anayepiga mutu na kumwua, hakika anapaswa kuuawa. #Ang. Law 24.17 13Lakini kama hakukuwa amemuvizia, lakini ni kwa musiba, basi, yule mwuaji ataweza kukimbilia usalama pahali nitakapowachagulia. 14Lakini mutu akimushambulia mwenzake kwa makusudi na kumwua kwa werevu, hata kama akikimbilia kwenye mazabahu, mutamutoa kule kwenye mazabahu yangu na kumwua.
15Anayemupiga baba yake au mama yake hakika atauawa.
16Anayemukamata mutu kwa kinguvu kusudi amwuzishe au kumufanya mutumwa wake, hakika atauawa.
17Anayemulaani baba yake au mama yake hakika atauawa. #Ang. Law 20.9; Mat 15.4; Mk 7.10
18Watu wawili wakigombana, kisha mumoja akamupiga mwenzake jiwe au ngumi bila kumwua, lakini akigonjwa na kubaki katika kitanda, 19ikiwa yule aliyepigwa akisimama tena na kuweza kutembea kwa kutegemea fimbo, yule aliyemupiga atasamehewa. Lakini, atamulipa kwa ajili ya muda alioupoteza katika kitanda na kumutunza mpaka apone kabisa.
20Mutu akimupiga mutumwa wake au mujakazi wake kwa fimbo na kumwua palepale, hakika ataazibiwa. 21Lakini mutumwa yule au mujakazi yule akibaki muzima siku moja au mbili, bwana wake hataazibiwa, maana yule alikuwa ni mali yake.
22Wanaume wakipigana na kumwumiza mwanamuke mwenye mimba, hata mimba yake ikaharibika bila hasara ingine zaidi, yule aliyemwumiza atalipa feza kadiri mume wa mwanamuke yule atakavyodai na kama vile waamuzi watakavyoamua. 23Lakini kama kutakuwa hasara nyingine, basi, unapaswa kulipa uzima kwa uzima, 24jicho kwa jicho, jino kwa jino, mukono kwa mukono, muguu kwa muguu, #Ang. Law 24.19-20; Kumb 19.21; Mat 5.38 25kuchomwa moto kwa kuchomwa moto, kidonda kwa kidonda, na pigo kwa pigo.
26Mutu akimupiga mutumwa au mujakazi wake na kuliharibu jicho lake, anapaswa kumwachilia aende huru bila malipo kwa ajili ya jicho lake. 27Vilevile, akimupiga hata kumwongoa mutumwa wake au mujakazi wake jino, anapaswa kumwachilia huru kwa ajili ya jino lake.
Maagizo juu ya usalama wa wengine
28Ngombe akimupiga mutu pembe na kumwua, ngombe yule atauawa kwa kupigwa mawe na nyama yake haitakuliwa. Mwenye ngombe yule hatahukumiwa. 29Lakini kama ngombe yule amezoea kupiga watu pembe, na mwenye ngombe akaonywa lakini hakumufunga, kama ngombe yule akiua mume au muke, ngombe yule atapigwa mawe, na mwenye ngombe vilevile atauawa. 30Hata hivyo, yule mutu akilipishwa feza kwa kuokoa maisha yake, anapaswa kulipa kiasi kamili atakacholipishwa. 31Ngombe akimupiga mutoto wa mutu mwingine kwa pembe, shauri hili litaamuliwa kwa njia hiyohiyo. 32Kama ngombe yule akimupiga pembe mutumwa au mujakazi, mwenye ngombe atamulipa bwana wa yule mutumwa feza zenye bei ya shekeli makumi tatu na yule ngombe anapaswa kuuawa kwa kupigwa mawe.
33Mutu akiacha shimo wazi, au akichimba shimo kisha asilifunike, halafu ngombe au punda akatumbukia ndani, 34yule mwenye shimo lile anapaswa kulipa. Atatoa feza kwa mwenye nyama yule na nyama aliyekufa atakuwa wake.
35Ngombe wa mutu akimwumiza ngombe wa mutu mwingine na kumwua, basi, watu watamwuzisha yule ngombe aliyebaki muzima na kugawayana bei yake. Vilevile watagawayana yule ngombe aliyekufa. 36Lakini kama yule ngombe alikuwa amezoea kupiga wengine pembe na mwenye ngombe yule hakumufunga, yeye atalipa ngombe kwa ngombe na yule ngombe aliyeuawa atakuwa wake.
37Mutu akiiba ngombe au kondoo na kumuchinja au kumwuzisha, atalipa ngombe watano kwa kila ngombe na kondoo wane kwa kila kondoo.
Currently Selected:
Kutoka 21: SWC02
Highlight
Share
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.