Zaburi 92:1-8
Zaburi 92:1-8 Biblia Habari Njema (BHN)
Ni vema kukushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kuliimbia sifa jina lako, ee Mungu Mkuu. Ni vema kutangaza fadhili zako asubuhi, na uaminifu wako nyakati za usiku, kwa muziki wa zeze na kinubi, kwa sauti tamu ya zeze. Ee Mwenyezi-Mungu, matendo yako yanifurahisha; nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda. Matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, ni makuu mno! Mawazo yako ni mazito mno! Mtu mpumbavu hawezi kufahamu, wala mjinga hajui jambo hili: Kwamba waovu waweza kustawi kama nyasi, watenda maovu wote waweza kufanikiwa, lakini mwisho wao ni kuangamia milele, bali wewe, ee Mwenyezi-Mungu, u mkuu milele.
Zaburi 92:1-8 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Ni neno jema kumshukuru BWANA, Na kuliimbia jina lako sifa, Ee Uliye Juu. Kuzitangaza rehema zako asubuhi, Na uaminifu wako wakati wa usiku. Kwa chombo chenye nyuzi kumi, Na kwa kinanda, Na kwa mlio wa kinubi. Kwa kuwa umenifurahisha, BWANA, Kwa kazi yako; nitashangilia Kwa ajili ya matendo ya mikono yako. Ee BWANA, jinsi yalivyo makuu matendo yako! Mawazo yako ni mafumbo makubwa. Mtu mjinga hayatambui hayo, Wala mpumbavu hayafahamu. Hata wasio haki wakichipuka kama majani Na wote watendao maovu wakastawi. Mwishowe wataangamizwa milele; Bali Wewe, BWANA, U Mtukufu hata milele.
Zaburi 92:1-8 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Ni neno jema kumshukuru BWANA, Na kuliimbia jina lako, Ee Uliye juu. Kuzitangaza rehema zako asubuhi, Na uaminifu wako wakati wa usiku. Kwa chombo chenye nyuzi kumi, Na kwa kinanda, Na kwa mlio wa kinubi. Kwa kuwa umenifurahisha, BWANA, Kwa kazi yako; nitashangilia Kwa ajili ya matendo ya mikono yako. Ee BWANA, jinsi yalivyo makuu matendo yako! Mawazo yako ni mafumbo makubwa. Mtu mjinga hayatambui hayo, Wala mpumbavu hayafahamu. Wasio haki wakichipuka kama majani Na wote watendao maovu wakistawi. Ni kwa kusudi waangamizwe milele; Bali Wewe, BWANA, U Mtukufu hata milele.
Zaburi 92:1-8 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)
Ni vyema kumshukuru BWANA na kuliimbia jina lako, Ee Uliye Juu Sana, kuutangaza upendo wako asubuhi, na uaminifu wako wakati wa usiku, kwa zeze yenye nyuzi kumi na kwa sauti ya kinubi. Ee BWANA, kwa kuwa matendo yako yamenifurahisha, nitaziimba kwa shangwe kazi za mikono yako. Ee BWANA, tazama jinsi yalivyo makuu matendo yako, tazama jinsi yalivyo ya kina mawazo yako! Mjinga hafahamu, mpumbavu haelewi, ingawa waovu huchipua kama majani na wote watendao mabaya wanastawi, wataangamizwa milele. Bali wewe, Ee BWANA, utatukuzwa milele.