ZAKARIA 4
4
Maono ya tano: Kinara cha taa
1Yule malaika aliyeongea nami, akanifikia tena, akaniamusha kama vile kumwamusha mutu toka katika usingizi. 2Akaniuliza: Unaona nini? Nami nikamujibu: Ninaona kinara cha taa cha zahabu. Juu yake kuna bakuli la mafuta na taa saba, na kila moja ina pahali pa kutilia tambi saba. 3Karibu na kinara hicho kuna miti miwili ya muzeituni; mumoja upande wa kuume na mwingine upande wa kushoto. #Ang. Ufu 11.4 4Basi, nikamwuliza yule malaika: Bwana, vitu hivi vina maana gani? 5Naye akanijibu: Haujui maana ya vitu hivi? Nikamujibu: Sijui bwana wangu.
6Yule malaika akaniambia vilevile niseme neno hili la Yawe juu ya Zerubabeli: Hauwezi kushinda kwa nguvu au kwa uwezo wako mwenyewe, lakini kwa musaada wa roho wangu. –Ni Yawe wa majeshi anayesema. #Ezra 5.2
7Tena, akaongeza kusema: Mulima huu ni kizuizi? Hapana! Wewe Zerubabeli utausawazisha. Wewe utaanzisha ujenzi mupya wa hekalu, na wakati utakapoliweka jiwe la mwisho, watu watashangilia wakisema: Ni zuri! Kweli, ni zuri!
8Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: 9Zerubabeli ameuweka musingi wa hekalu naye vilevile atalikamilisha. Hayo yatakapotukia, watu wangu watajua kwamba mimi Yawe wa majeshi ndimi niliyekutuma kwao. 10Maendeleo ya ujenzi wa hekalu yanaonekana madogo, na watu wanayazarau; lakini watamwona Zerubabeli akiendelea kulijenga hekalu, nao watafurahi.
Sasa, juu ya hizo taa saba, yule malaika akaniambia: Ni macho saba ya Yawe yanayoona kila nafasi katika dunia. #Ang. Ufu 5.6
11Nami nikazidi kuuliza: Hiyo miti miwili ya mizeituni inayokuwa upande wa kuume na wa kushoto wa kinara, ina maana gani? 12Na yale matawi mawili pembeni ya mirija miwili ya zahabu ambamo mafuta ya mizeituni yanatiririkia, yana maana gani?
13Naye akaniambia: Haujui?
Nami nikamujibu: Hapana, sijui Bwana!
14Halafu akaniambia: Hawa ndio wale watu wawili ambao Bwana wa ulimwengu wote aliwachagua kwa kuwapakaa mafuta kusudi wamutumikie.
Currently Selected:
ZAKARIA 4: SWC02
Highlight
Share
Compare
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.