Mwanzo 35
35
Yakobo anahamia Beteli
1Siku moja, Mungu akamwambia Yakobo: “Anza safari, uende kuishi Beteli na kunijengea mazabahu kule, mimi Mungu niliyekutokea wakati ulipomukimbia kaka yako Esau.”
2Basi, Yakobo akawaambia jamaa yake na wote aliokuwa nao: “Mutupilie mbali sanamu za miungu ya kigeni munazokuwa nazo, mujitakase na kubadilisha nguo zenu. 3Kisha, tutakwenda Beteli kusudi nimujengee Mungu mazabahu, Mungu ambaye alinisaidia siku ya taabu na kuwa nami popote nilipokwenda.” 4Basi, wakamupa Yakobo sanamu zote za miungu ya kigeni walizokuwa nazo pamoja na pete walizokuwa wamevaa kwa masikio. Na Yakobo akavizika chini ya muti wa mwalo uliokuwa karibu na Sekemu.
5Yakobo na wana wake walipokuwa wakisafiri, Mungu akawatia hofu wenyeji wa miji yote ya jirani hata hawakusubutu kuwafuatilia. 6Basi, Yakobo akafika Luzi, maana yake Beteli, katika inchi ya Kanana, pamoja na watu wote aliokuwa nao. 7Akajenga mazabahu pahali pale na kupaita “Mungu wa Beteli” maana ni pale ndipo pahali Mungu alipojionyesha kwake wakati alipokuwa akimukimbia kaka yake. 8Debora, mulezi wa Rebeka, akakufa, akazikwa chini ya muti wa mwalo upande wa kusini wa Beteli. Kwa hiyo Yakobo akauita muji ule “Mwalo wa Maombolezo”.
9Wakati alipokuwa akirudi kutoka Padani-Aramu, Mungu akamutokea tena Yakobo na kumubariki.
10Mungu akamwambia: “Jina lako ni Yakobo, lakini hautaitwa hivyo tena, lakini sasa jina lako litakuwa Israeli.” Kwa hiyo Yakobo akaitwa Israeli.
11Tena Mungu akamwambia: “Mimi ni Mungu Mwenye Nguvu#35.11 Mungu Mwenye Nguvu: Kiebrania: El Shadai.. Ujaliwe wazao wengi na kuongezeka. Taifa na kundi la mataifa watatokea kwako na wafalme watatokea katika uzao wako. 12Inchi niliyowapa Abrahamu na Isaka nitakupa wewe na wazao wako.” 13Basi, nyuma ya kuongea na Yakobo, Mungu akamwacha na kupanda juu. 14Yakobo akasimika nguzo ya jiwe la ukumbusho pahali pale Mungu alipozungumuza naye, akaitakasa kwa kuimiminia sadaka ya kinywaji na mafuta. 15Basi, Yakobo akapaita pahali pale alipozungumuza na Mungu Beteli.
Kuzaliwa kwa Benjamina na kifo cha Rakeli
16Yakobo na jamaa yake yote wakaendelea na safari yao kutoka Beteli. Walipokuwa umbali fulani mbele ya kufika Efurata, Rakeli akashikwa na uchungu mukali wa kuzaa. 17Naye alipokuwa katika uchungu ule, muzalishaji akamwambia: “Usiogope, umepata mutoto mwingine mwanaume.” 18Rakeli akiwa karibu kufa, akamupa yule mutoto jina Beni-oni.#35.18 Beni-oni: ni kama neno la Kiebrania lenye maana yake “mwana wa huzuni yangu”. Lakini baba yake akamwita mutoto yule Benjamina.#35.18 Benjamina: ni kama neno la Kiebrania lenye maana “mwana atakayebahatika”.
19Basi, Rakeli akakufa na kuzikwa kando ya njia inayokwenda Efurata, ni kusema Betelehemu. 20Yakobo akasimika nguzo ya ukumbusho juu ya kaburi ya Rakeli ambayo iko mpaka leo.
21Israeli, ndiye Yakobo, akaendelea na safari yake na kupiga kambi yake ngambo ya munara wa Ederi. 22Wakati Israeli alipokuwa anakaa katika inchi ile, mwana wake Rubeni, akalala na Biliha, habara ya baba yake. Naye Israeli akasikia habari hizo.
Wana wa Yakobo
(1 Sik 2.1-2)
Yakobo alikuwa na wana kumi na wawili. 23Wana wa Lea walikuwa Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Yakobo, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari na Zabuluni. 24Wana wa Rakeli walikuwa Yosefu na Benjamina. 25Wana waliozaliwa na Biliha, mujakazi wa Rakeli, walikuwa Dani na Nafutali. 26Na wana waliozaliwa na Zilpa, mujakazi wa Lea, walikuwa Gadi na Aseri. Hao ndio wana wa Yakobo, aliozaa alipokuwa kule Padani-Aramu.
Kifo cha Isaka
27Yakobo akaondoka akakwenda Mamure kwa baba yake Isaka, kule Kiriati-Arba ni kusema Hebroni, pahali ambapo Abrahamu na Isaka walikaa kama wageni. 28Isaka alipokuwa na miaka mia moja na makumi nane, 29akiwa muzee wa miaka mingi, akakufa na kukutana na wazee wake. Watoto wake, Esau na Yakobo wakamuzika.
Currently Selected:
Mwanzo 35: SWC02
Highlight
Share
Copy

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.