Kutoka 16
16
Mana na kwale
  1Waisraeli wote wakasafiri toka Elimu na kufika katika jangwa la Sini kati ya Elimu na Sinai. Hii ilikuwa siku ya kumi na tano ya mwezi wa pili tangu walipoondoka inchi ya Misri. 2Basi, Waisraeli wote pamoja wakamunungunikia Musa na Haruni kule katika jangwa. Wakasema hivi: 3“Heri Yawe angelituua tulipokuwa katika inchi ya Misri ambako tulikaa, tukakula nyama na mikate hata tukashiba. Lakini ninyi mumetuleta huku katika jangwa kwa kuua jamii hii yote kwa njaa!”
  4Halafu Yawe akamwambia Musa: “Mimi nitawanyeshea mikate kutoka mbinguni. Kila siku watu watatoka na kukusanya chakula cha siku hiyo. Kwa njia hii nitawapima nione kama watafuata sheria zangu au hawatazifuata. #Ang. Yn 6.31  5Lakini siku ya sita, wakati watakapotayarisha chakula walichokusanya, kipimo kile kitakuwa mara mbili ya chakula cha kila siku.”
  6Basi, Musa na Haruni wakawaambia watu wote wa Israeli: “Magaribi, mutatambua kwamba Yawe ndiye aliyewatoa katika inchi ya Misri! 7Tena, kesho asubui mutaona utukufu wa Yawe maana ameyasikia manunguniko muliyomunungunikia. Sisi ni nani hata mutunungunikie?” 8Tena Musa akasema: “Magaribi, Yawe atawapa nyama mupate kula na asubui atawapa mikate mupate kula na kushiba. Maana yeye ameyasikia manunguniko muliyomunungunikia. Sisi ni nani hata mutunungunikie? Musitunungunikie sisi lakini mumunungunikie Yawe.”
  9Kisha Musa akamwambia Haruni: “Uwaambie Waisraeli wote wakusanyike mbele ya Yawe, maana ameyasikia manunguniko yao.” 10Wakati Haruni alipokuwa akizungumuza na Waisraeli wote pamoja, watu wote wakaangalia kule katika jangwa na mara moja utukufu wa Yawe ukaonekana katika mawingu. 11Yawe akamwambia Musa: 12“Nimesikia manunguniko ya Waisraeli. Basi, uwaambie kwamba wakati wa magaribi watakula nyama na asubui watakula mukate. Hapo ndipo mutakapotambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu.”
  13Basi, kwa wakati wa magaribi kukakuja kwale wengi, wakafunika kambi ya Waisraeli. Asubui yake kukatokea umande, ukatanda kandokando ya kambi yao. 14Umande ule ulipotoweka, kukabaki kule katika jangwa kitu kama mukate mwembamba na mwepesi. 15Waisraeli walipoona kitu kile wakashangaa, wakaulizana: “Nini hii?”#16.15 Nini hii: Ang. maelezo ya 16.31. Hawakujua kilikuwa kitu gani.
Basi, Musa akawaambia: “Huu ni mukate ambao Yawe amewapa mukule. #Ang. 1 Kor 10.3  16Yawe ameamuru mufanye hivi: kila mutu akusanye chakula kipimo anachoweza kula. Ataokota kipimo cha litre ine#16.16 litre ine: Kiebrania: omeri moja. kwa kila mutu katika hema yake.”
  17Basi, Waisraeli wakafanya hivyo na ikakuwa kwamba wengine waliokota kwa wingi na wengine kidogo. 18Lakini wote walipopima kiasi walichookota katika kipimo cha litre ine, walitambua kwamba aliyeokota kingi hakukuwa na cha zaidi na aliyeokota kidogo, hakupungukiwa. Kila mumoja alikuwa ameokota kiasi alichoweza kula. #Ang. 2 Kor 8.15
  19Musa akawaambia watu: “Mutu yeyote asiache chakula hicho mpaka asubui.”
  20Lakini watu hawakumusikiliza Musa. Wamoja kati yao walijiwekea chakula mpaka asubui. Lakini asubui chakula hicho kikakuwa kimeoza na kuwa na vidudu. Musa akawakasirikia sana watu. 21Basi, kila asubui walikusanya chakula kila mutu kipimo alichohitaji kula. Jua lilipopanda juu na kuwa kali, kile chakula kingine kiliyeyuka.
  22Katika siku ya sita, Waisraeli walikusanya chakula hicho mara mbili, vipimo viwili vya litre ine kwa kila mutu. Basi, wazee wote wa Waisraeli wakamwendea Musa, wakamwelezea jambo hilo. 23Musa akawaambia: “Hii ndiyo amri ya Yawe. Kesho ni siku ya mapumziko. Ni Sabato takatifu ya Yawe. Basi, muende mupike au kuchemusha kile chakula munachohitaji leo na chakula kitakachobakia mukiweke mpaka kesho.” #Ang. Kut 20.8-11  24Basi, wakafanya hivyo na kuacha chakula kingine mpaka kesho yake kama vile Musa alivyosema. Asubui yake waliona kwamba hakikuharibika wala kuwa na vidudu. 25Basi, Musa akawaambia: “Mukule chakula hicho kilichobakia kwa sababu leo ni Sabato ya Yawe. Leo hamutapata chakula kule inje. 26Kwa siku sita mutakuwa mukikusanya chakula hiki, lakini siku ya saba ambayo ni Sabato hakitakuwa.”
  27Kwa siku ya saba watu wamoja walitoka kwenda kutafuta chakula, lakini hawakukipata. 28Hapo Yawe akamwambia Musa: “Mpaka wakati gani mutakataa kutii amri na sheria zangu? 29Mufahamu kwamba mimi Yawe nimewapa siku ya Sabato, ndiyo maana nimewapa chakula cha siku mbili kwa siku ya sita. Basi, kila mutu apumzike ndani ya nyumba yake. Mutu yeyote asitoke katika siku ya saba.” 30Kwa hiyo, watu walipumzika siku ya saba.
  31Waisraeli wakaita chakula hicho “Mana.”#16.31 Mana: Katika Kiebrania neno hili linasikilika kama ulizo “Nini hii?” Ang. 16.15. Kilikuwa kama mbegu za mutama mweupe na onjo yake ilikuwa kama mukate mwembamba uliotiwa asali. #Ang. Hes 11.7-8  32Musa akawaambia: “Hili ndilo agizo la Yawe: Mutwae kipimo kimoja cha litre ine ya mana na kukiweka kwa ajili ya wazao wenu, kusudi waweze kuona chakula nilichowakulisha katika jangwa wakati nilipowatoa katika inchi ya Misri.”
  33Musa akamwambia Haruni: “Twaa kopo, utie ndani yake kipimo kimoja cha litre ine ya mana na kuiweka mbele ya Yawe, ikuwe kwa ajili ya wazao wenu.” #Ang. Ebr 9.4
  34Basi, Haruni aliweka mana Pahali Patakatifu mbele ya Sunduku la Agano kusudi ilindwe kama vile Yawe alivyomwagiza Musa. 35Waisraeli walikula mana kwa muda wa miaka makumi ine, mpaka walipofika katika inchi iliyofaa kwa kuishi, ni kusema mpaka walipovuka mupaka wa Kanana. #Ang. Yos 5.12  36(Posho ya mana ilikuwa sehemu ya kumi ya kipimo cha kawaida kinachoitwa efa.)
      Currently Selected:
Kutoka 16: SWC02
Highlight
Share
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.