2 Mambo ya Siku 28
28
Mufalme Ahazi wa Yuda
(2 Fal 16.1-4)
1Ahazi alianza kutawala akiwa na umri wa miaka makumi mbili, alitawala kwa muda wa miaka kumi na sita kule Yerusalema. Yeye, hakufuata mufano muzuri wa Daudi babu yake, lakini alitenda maovu mbele za Yawe, 2na kufuata mienendo ya wafalme wa Israeli. Vilevile, alitengeneza hata sanamu za Mabali za madini yenye kuyeyushwa, 3akafukiza ubani kwenye Bonde la mwana wa Hinomu na kuwateketeza wana wake kama sadaka, akiiga desturi za kuchukiza za watu ambao walifukuzwa na Yawe wakati Waisraeli walipokuwa wanaingia katika inchi. 4Alitoa sadaka na kufukiza ubani pahali pa kuabudia miungu mingine, juu ya vilima na chini ya kila muti wenye majani mabichi.
Vita kati ya Suria na Israeli
(2 Fal 16.5)
5Yawe, Mungu wake akamwacha mufalme Ahazi ashindwe na mufalme wa Suria ambaye vilevile akawapeleka watu wake wengi, akarudi nao Damasiki. Vilevile, alimufanya ashindwe na mufalme wa Israeli ambaye alimushinda na kuua watu wengi sana. #Ang. Isa 7.1 6Peka, mwana wa Remalia akawaua watu wengi sana. Aliua waaskari mashujaa wa Yuda elfu mia moja na makumi mbili katika siku moja. Ilitokea vile kwa sababu walimwacha Yawe, Mungu wa babu zao. 7Zikiri, askari mumoja shujaa wa Israeli, alimwua Maseya, mwana wa mufalme, Azirikamu, musimamizi wa nyumba ya kifalme, na Elekana aliyekuwa mutu wa pili kwa mufalme. 8Jeshi la Israeli likapeleka wafungwa wandugu zao watu elfu mia mbili, wanawake na watoto. Waliwapeleka mpaka Samaria pamoja na mali nyingi waliyonyanganya.
Nabii Obedi
9Lakini kule Samaria kulikuwa nabii wa Yawe, jina lake Obedi. Yeye alitoka kwenda kukutana na waaskari wa Israeli walipokuwa karibu kuingia Samaria, akawaambia: “Yawe, Mungu wa babu zenu, alikuwa amewakasirikia watu wa Yuda, ndiyo maana aliwatia katika mikono yako lakini umewaua kwa hasira. Tendo hilo limetoka mbinguni. 10Sasa munakusudia kuwafanya wanaume na wanawake wa Yuda na Yerusalema watumwa wenu. Hamutambui kwamba ninyi vilevile mumetenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wenu? 11Sasa sikia yale ninayosema, muwarudishe wandugu zenu na wadada zenu muliowakamata kuwa wafungwa, maana kasirani kali ya Yawe iko juu yenu.”
12Nao wakubwa fulani wa Efuraimu, Azaria mwana wa Yohana, Berekia mwana wa Mesilemoti, Yehizikia mwana wa Salumu na Amasa mwana wa Hadilai, vilevile waliwagombeza wale waliotoka kwa vita. 13Wakawaambia: “Musiwalete humu wafungwa hao, kwa sababu munakusudia kutuletea kosa mbele ya Yawe, tendo hili huku litakuwa nyongezo ya zambi yetu na kosa letu; kwa sababu kosa letu tayari ni kubwa na kuna kasirani kali juu ya Israeli.” 14Hivyo, waaskari wakawaacha wafungwa wao na vitu vyote walivyonyanganya katika mikono ya wakubwa na mukutano wote. 15Wale wakubwa waliotajwa majina yao waliwatwaa wafungwa na kwa kutumia vitu vilivyonyanganywa wakawavalisha wafungwa ambao hawakukuwa na nguo; waliwapatia viatu, chakula na vinywaji, na kuwapakaa mafuta. Wale ambao walikuwa hawajiwezi, wakawabeba juu ya punda, wakawapeleka wafungwa wote mpaka Yeriko, muji wa mingazi, kwa wandugu zao; kisha wao wakarudi Samaria.
Ahazi anaomba musaada kutoka Asuria
(2 Fal 16.7-9)
16Wakati ule, mufalme Ahazi akatuma wajumbe kwa mufalme wa Asuria kusudi awasaidie 17kwa sababu Waedomu walikuwa wamekuja tena, wakashambulia inchi ya Yuda, wakawashinda na kupeleka wafungwa wengi. 18Wakati uleule, Wafilistini walikuwa wakiishambulia miji ya Sefela na Negebu ya Yuda. Walinyanganya miji ya Beti-Semesi, Ayaloni, Gederoti, Soko na vijiji vyake, Timuna na vijiji vyake, Gimuzo na vijiji vyake, wakafanya makao yao kule. 19Kwa maana Yawe alinyenyekeza inchi ya Yuda kwa ajili ya Ahazia mufalme wa Israeli sababu yeye alifanya uasherati katika Yuda na kumwasi Yawe. 20Tigilati-Pileseri, mufalme wa Asuria akamushambulia pahali pa kumutia nguvu. 21Kwa sababu Ahazi alitwaa zahabu kutoka katika nyumba ya Mungu, nyumba ya kifalme na nyumba za wakubwa, akamupa mufalme wa Asuria kama kodi; lakini jambo hili vilevile halikumusaidia kwa kitu.
Zambi za Ahazia
22Wakati alipokuwa katika taabu zaidi, mufalme huyu Ahazi alizidi kumwasi Yawe. 23Kwa sababu alitolea sadaka kwa miungu ya Damasiki iliyokuwa imemushinda katika vita akisema: “Kwa sababu miungu ya Suria iliwasaidia wafalme wa Shamu, nikiitolea sadaka labda itanisaidia nami vilevile.” Lakini ilisababisha kuangamia kwake na taifa lote la Israeli. 24Zaidi ya hayo, alikusanya vifaa vyote vya nyumba ya Mungu, akavikatakata vipandevipande, kisha akafunga milango ya nyumba ya Yawe na kujijengea mazabahu katika kila pembe ya Yerusalema. 25Na katika kila muji wa Yuda, akatengeneza pahali pa kufukizia ubani kwa miungu mingine. Kwa kutenda hivyo, akamukasirikisha Yawe, Mungu wa babu zake.
26Matendo yake mengine na mienendo yake yote, kutoka mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli. 27Mufalme Ahazi alikufa na kuzikwa katika muji wa Yerusalema, lakini si katika makaburi ya wafalme wa Israeli. Na Hezekia mwana wake, akatawala pahali pake. #Ang. Isa 14.28
Currently Selected:
2 Mambo ya Siku 28: SWC02
Highlight
Share
Compare
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.