YouVersion Logo
Search Icon

1 Tim UTANGULIZI

UTANGULIZI
Nyaraka kwa Timotheo na Tito huitwa “Nyaraka za Uchungaji” kwa sababu zimeandikwa kwa viongozi wa makanisa na kwa jumla zina malengo ya kuwashauri juu ya jinsi inavyowapasa kuziongoza jumuiya za kikristo.
Timotheo alikuwa mwenyeji wa Listra, mama yake alikuwa Myahudi na baba yake Mgiriki. Kadiri ya 2 Tim 1:5 na 3:15 Timotheo alikuwa amejua Maandiko Matakatifu tangu ujana wake na alipata kuwa Mkristo kwa njia ya mama na nyanya yake kabla ya kukutana na Paulo katika safari yake ya kwanza ya kitume alipotembelea miji ya Galatia (2 Tim 3:10-11; Mdo 13:14-15:22). Baada ya miaka mitatu Paulo alipotembelea tena mkoa wa Galatia alimchukua Timotheo awe msaidizi wake (Mdo 16:1-3). Makanisa yaliridhia uamuzi huo (1 Tim 4:14). Paulo anampa sifa ya kuwa mwanawe na mara nyingi alimsifia kwa upendo wake na kujitolea kwa ajili ya kazi ya Bwana. (1 Kor 4:17; Flp 2:19-20; 1 Tim 1:18).
Waraka wa kwanza kwa Timotheo una malengo mawili makuu: kwanza kabisa ni mwongozo kuhusu matatizo ya uongozi wa kanisa na kupinga mafundisho ya uongo. Kwa hiyo, Waraka huu unatoa mawaidha kuhusu taratibu za ibada (2:1-125), sifa zinazotakiwa kutoka kwa mtu anayetaka kuwa askofu (3:11-7), na mashemasi (3:8-13) (wadhifa wa “askofu” na “shemasi” haukuwa umewekwa dhahiri kama ilivyokuwa baadaye). Waraka unatoa pia mwongozo juu ya jinsi viongozi wa kanisa wanavyopaswa kuhusika katika hali ya kujinyima anasa za mwili (4:1-10), mtazamo wao kuhusu watu mbalimbali binafsi (5:1-22), kama vile wajane (5:3-16), wazee wa kanisa (5:17-20) na watumwa (6:1-2). Pili, mwandishi anawaonya vikali waalimu ambao wamekosa ufahamu na kupotea katika mazungumzo yasiyo na faida na mwishoni huishia katika kuizamisha imani yao (1:3-7,19-20; 6:3-10). Kwa namna ya pekee, katika 6:3-10, Paulo ana maneno makali ya kuwaonya wale wanaojaribu kutumia dini kwa faida yao wenyewe. Pia kuna maonyo kuhusu watu wengine waliojidai kuwa na ujuzi wa kweli na kujiona juu kuliko maumbile na hivyo kukataza kuoa na kuwataka watu waache kabisa kula vyakula fulani.

Currently Selected:

1 Tim UTANGULIZI: SUV

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy