YouVersion Logo
Search Icon

Yeremia 51

51
1 Hili ndilo asemalo Bwana:
“Tazama nitaamsha roho ya mwangamizi
dhidi ya Babeli na watu wakaao Leb-Kamai.#51:1 Leb-Kamai ni Ukaldayo, yaani Babeli, kwa fumbo.
2Nitawatuma wageni Babeli
kumpepeta na kuiharibu nchi yake;
watampinga kila upande
katika siku ya maafa yake.
3 Usimwache mpiga upinde afunge kamba upinde wake,
wala usimwache avae silaha zake.
Usiwaonee huruma vijana wake;
angamiza jeshi lake kabisa.
4 Wataanguka waliouawa katika Babeli,
wakiwa na majeraha ya kutisha barabarani zake.
5 Kwa maana Israeli na Yuda hawajaachwa
na Mungu wao, Bwana Mwenye Nguvu Zote,
ingawa nchi yao imejaa uovu
mbele zake yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli.
6 “Kimbieni kutoka Babeli!
Okoeni maisha yenu!
Msiangamizwe kwa sababu ya dhambi zake.
Ni wakati wa kisasi cha Bwana,
atamlipa kile anachostahili.
7 Babeli alikuwa kikombe cha dhahabu katika mkono wa Bwana;
aliufanya ulimwengu wote ulewe.
Mataifa walikunywa mvinyo wake;
kwa hiyo sasa wameingiwa na wazimu.
8 Babeli ataanguka ghafula na kuvunjika.
Mwombolezeni!
Tafuteni zeri ya kutuliza maumivu yake,
labda anaweza kupona.
9 “ ‘Tungemponya Babeli,
lakini hawezi kuponyeka;
tumwacheni, na kila mmoja wetu aende nchi yake mwenyewe,
kwa kuwa hukumu yake inafika angani,
inapanda juu hadi mawinguni.’
10 “ ‘Bwana amethibitisha haki yetu;
njooni, tutangaze katika Sayuni
kitu ambacho Bwana Mungu wetu amefanya.’
11“Noeni mishale,
chukueni ngao!
Bwana amewaamsha wafalme wa Wamedi,
kwa sababu nia yake ni kuangamiza Babeli.
Bwana atalipiza kisasi,
kisasi kwa ajili ya Hekalu lake.
12 Twekeni bendera juu ya kuta za Babeli!
Imarisheni ulinzi,
wekeni walinzi,
andaeni waviziao!
Bwana atatimiza kusudi lake,
amri yake juu ya watu wa Babeli.
13 Wewe uishiye kando ya maji mengi
na uliye na wingi wa hazina,
mwisho wako umekuja,
wakati wako wa kukatiliwa mbali.
14 Bwana Mwenye Nguvu Zote
ameapa kwa nafsi yake mwenyewe:
‘Hakika nitakujaza na watu, kama kundi la nzige,
nao watapiga kelele za ushindi juu yako.’
15 “Aliiumba dunia kwa uweza wake;
akaweka misingi ya ulimwengu kwa hekima yake
na akazitandaza mbingu kwa ufahamu wake.
16 Atoapo sauti yake, maji yaliyo katika mbingu hunguruma,
huyafanya mawingu yainuke kutoka miisho ya dunia.
Hupeleka umeme wa radi pamoja na mvua,
naye huuleta upepo kutoka ghala zake.
17 “Kila mtu ni mjinga na hana maarifa;
kila sonara ameaibishwa na sanamu zake.
Vinyago vyake ni vya udanganyifu,
havina pumzi ndani yavyo.
18 Havifai kitu, ni vitu vya kufanyia mzaha,
hukumu yavyo itakapowadia, vitaangamia.
19 Yeye Aliye Fungu la Yakobo sivyo alivyo,
kwani ndiye Muumba wa vitu vyote,
pamoja na kabila la urithi wake:
Bwana Mwenye Nguvu Zote ndilo jina lake.
20 “Wewe ndiwe rungu langu la vita,
silaha yangu ya vita:
kwa wewe navunjavunja mataifa,
kwa wewe naangamiza falme,
21 kwa wewe navunjavunja
farasi na mpanda farasi,
kwa wewe navunjavunja
gari la vita na mwendeshaji wake,
22 kwa wewe napondaponda
mwanaume na mwanamke,
kwa wewe napondaponda
mzee na kijana,
kwa wewe napondaponda
kijana wa kiume na mwanamwali,
23kwa wewe nampondaponda
mchungaji na kundi,
kwa wewe nampondaponda
mkulima na maksai,
kwa wewe nawapondaponda
watawala na maafisa.
24 “Mbele ya macho yako nitamlipiza Babeli na wote waishio Ukaldayo kwa ajili ya makosa yote waliyofanya katika Sayuni,” asema Bwana.
25 “Mimi niko kinyume nawe, ee mlima unaoharibu,
wewe uangamizaye dunia yote,”
asema Bwana.
“Nitanyoosha mkono wangu dhidi yako,
nikuvingirishe kutoka kwenye kilele cha mwamba,
na kukufanya mlima ulioteketezwa kwa moto.
26 Hakuna jiwe litakalochukuliwa kutoka kwako
kwa ajili ya kufanywa jiwe la pembeni,
wala jiwe lolote kwa ajili ya msingi,
kwa maana utakuwa ukiwa milele,”
asema Bwana.
27 “Twekeni bendera katika nchi!
Pigeni tarumbeta katikati ya mataifa!
Andaeni mataifa kwa ajili ya vita dhidi yake,
iteni falme hizi dhidi yake:
Ararati, Mini na Ashkenazi.
Wekeni jemadari dhidi yake,
pelekeni farasi wengi kama kundi la nzige.
28Andaeni mataifa kwa ajili ya vita dhidi yake,
wafalme wa Wamedi,
watawala wao na maafisa wao wote,
pamoja na nchi zote wanazotawala.
29 Nchi inatetemeka na kugaagaa,
kwa kuwa makusudi ya Bwana dhidi ya Babeli yanasimama:
yaani, kuangamiza nchi ya Babeli
ili pasiwe na yeyote atakayeishi humo.
30 Mashujaa wa Babeli wameacha kupigana,
wamebaki katika ngome zao.
Nguvu zao zimekwisha,
wamekuwa kama wanawake.
Makazi yake yameteketezwa kwa moto,
makomeo ya malango yake yamevunjika.
31 Tarishi mmoja humfuata mwingine,
na mjumbe humfuata mjumbe,
kumtangazia mfalme wa Babeli
kwamba mji wake wote umetekwa,
32 Vivuko vya mito vimekamatwa,
mabwawa yenye mafunjo yametiwa moto,
nao askari wameingiwa na hofu kuu.”
33 Hili ndilo Bwana Mwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli, asemalo:
“Binti Babeli ni kama sakafu ya kupuria
wakati inapokanyagwa;
wakati wa kumvuna utakuja upesi.”
34 “Nebukadneza mfalme wa Babeli ametula,
ametufanya tuchangayikiwe,
ametufanya tuwe gudulia tupu.
Kama nyoka ametumeza
na kujaza tumbo lake kwa vyakula vyetu vizuri,
kisha akatutapika.
35Jeuri iliyofanyiwa miili yetu#51:35 Au: Jeuri tuliyofanyiwa sisi na watoto wetu. na iwe juu ya Babeli,”
ndivyo wasemavyo wakaao Sayuni.
“Damu yetu na iwe juu ya wale waishio Babeli,”
asema Yerusalemu.
36 Kwa hiyo, hili ndilo Bwana asemalo:
“Tazama, nitatetea shauri lako
na kulipiza kisasi kwa ajili yako;
nitaikausha bahari yake
na kuzikausha chemchemi zake.
37 Babeli utakuwa lundo la magofu
na makao ya mbweha,
kitu cha kutisha na kudharauliwa,
mahali asipoishi mtu.
38Watu wake wote wananguruma kama simba wadogo,
wanakoroma kama wana simba.
39 Lakini wakati wakiwa wameamshwa,
nitawaandalia karamu
na kuwafanya walewe,
ili wapige kelele kwa kicheko,
kisha walale milele na wasiamke,”
asema Bwana.
40“Nitawateremsha kama wana-kondoo waendao machinjoni,
kama kondoo dume na mbuzi.
41 “Tazama jinsi Sheshaki#51:41 Sheshaki ni Babeli kwa fumbo. atakamatwa,
majivuno ya dunia yote yatakavyonyakuliwa.
Babeli atakuwa mwenye hofu kiasi gani
kati ya mataifa!
42 Bahari itainuka juu ya Babeli;
mawimbi yake yenye kunguruma yatamfunika.
43 Miji yake itakuwa ukiwa,
kame na jangwa,
nchi ambayo hakuna yeyote anayeishi ndani yake,
ambayo hakuna mtu anayepita humo.
44 Nitamwadhibu Beli katika Babeli,
na kumfanya atapike kile alichokimeza.
Mataifa hayatamiminika tena kwake.
Nao ukuta wa Babeli utaanguka.
45 “Tokeni ndani yake, enyi watu wangu!
Okoeni maisha yenu!
Ikimbieni hasira kali ya Bwana.
46 Msikate tamaa wala msiogope tetesi
zitakaposikika katika nchi;
tetesi moja inasikika mwaka huu,
nyingine mwaka unaofuata;
tetesi juu ya jeuri katika nchi,
na ya mtawala dhidi ya mtawala.
47 Kwa kuwa hakika wakati utawadia
nitakapoziadhibu sanamu za Babeli;
nchi yake yote itatiwa aibu,
na watu wake wote waliouawa
wataangukia ndani yake.
48 Ndipo mbingu na dunia na vyote vilivyomo ndani yake
vitapiga kelele za shangwe juu ya Babeli,
kwa kuwa kutoka kaskazini
waharabu watamshambulia,”
asema Bwana.
49 “Babeli ni lazima aanguke kwa sababu ya kuwaua Waisraeli,
kama vile waliouawa duniani kote
walivyoanguka kwa sababu ya Babeli.
50Wewe uliyepona upanga,
ondoka wala usikawie!
Mkumbuke Bwana ukiwa katika nchi ya mbali,
na utafakari juu ya Yerusalemu.”
51 “Tumetahayari, kwa maana tumetukanwa
na aibu imefunika nyuso zetu,
kwa sababu wageni wameingia
mahali patakatifu pa nyumba ya Bwana.”
52 “Lakini siku zinakuja,” asema Bwana,
“nitakapoadhibu sanamu zake,
na katika nchi yake yote
waliojeruhiwa watalia kwa maumivu makali.
53 Hata kama Babeli ikifika angani
na kuziimarisha ngome zake ndefu,
nitatuma waharabu dhidi yake,”
asema Bwana.
54“Sauti ya kilio inasikika kutoka Babeli,
sauti ya uharibifu mkuu
kutoka nchi ya Wakaldayo.
55 Bwana ataiangamiza Babeli,
atanyamazisha makelele ya kishindo chake.
Mawimbi ya adui yatanguruma kama maji makuu,
ngurumo ya sauti zao itavuma.
56 Mharabu atakuja dhidi ya Babeli,
mashujaa wake watakamatwa,
nazo pinde zao zitavunjwa.
Kwa kuwa Bwana ni Mungu wa kisasi,
yeye atalipiza kikamilifu.
57 Nitawafanya maafisa wake na wenye busara walewe,
watawala wao, maafisa, pamoja na wapiganaji wao;
watalala milele na hawataamka,”
asema Mfalme, ambaye jina lake ni Bwana Mwenye Nguvu Zote.
58 Hili ndilo Bwana Mwenye Nguvu Zote asemalo:
“Ukuta mnene wa Babeli utasawazishwa,
na malango yaliyoinuka yatateketezwa kwa moto;
mataifa yanajichosha bure,
taabu ya mataifa ni nishati tu ya miali ya moto.”
59 Huu ndio ujumbe Yeremia aliompa afisa Seraya mwana wa Neria mwana wa Maaseya, alipokwenda Babeli pamoja na Sedekia mfalme wa Yuda, katika mwaka wa nne wa utawala wake. 60 Yeremia alikuwa ameandika ndani ya kitabu kuhusu maafa yote yatakayoipata Babeli, yaani yote yaliyokuwa yameandikwa kuhusu Babeli. 61Yeremia akamwambia Seraya, “Utakapofika Babeli, hakikisha kwamba umesoma maneno haya yote kwa sauti kubwa. 62 Kisha sema, ‘Ee Bwana, umesema utaangamiza mahali hapa ili mtu wala mnyama asiishi ndani yake, napo patakuwa ukiwa milele.’ 63 Utakapomaliza kusoma hiki kitabu, kifungie jiwe kisha ukitupe ndani ya Mto Frati. 64 Kisha sema, ‘Hivi ndivyo Babeli utakavyozama na usiinuke tena, kwa sababu ya maafa nitakayoleta juu yake. Nao watu wake wataanguka.’ ”
Maneno ya Yeremia yanaishia hapa.

Currently Selected:

Yeremia 51: NEN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy