Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Waroma 16:1-24

Waroma 16:1-24 Biblia Habari Njema (BHN)

Napenda kumjulisha kwenu dada yetu Foibe ambaye ni mtumishi katika kanisa la Kenkrea. Mpokeeni kwa ajili ya Bwana kama iwapasavyo watu wa Mungu. Mpeni msaada wowote atakaohitaji kutoka kwenu, maana yeye amekuwa mwema sana kwa watu wengi na kwangu pia. Salamu zangu ziwafikie Priska na Akula, wafanyakazi wenzangu katika utumishi wa Kristo Yesu. Wao walihatarisha maisha yao kwa ajili yangu. Wanastahili shukrani; si tu kutoka kwangu, bali pia kutoka kwa makanisa yote ya watu wa mataifa mengine. Salamu zangu pia kwa kanisa linalokutana nyumbani kwao. Salamu zangu zimfikie rafiki yangu Epaineto ambaye ni wa kwanza katika mkoa wa Asia kumwamini Kristo. Nisalimieni Maria ambaye amefanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu. Salamu zangu kwa Androniko na Yunia, wananchi wenzangu waliofungwa gerezani pamoja nami; wao wanajulikana sana kati ya mitume; tena walikuwa Wakristo kabla yangu mimi. Salamu zangu kwa Ampliato, rafiki yangu katika kuungana na Bwana. Salamu zangu zimfikie Urbano, mfanyakazi mwenzangu katika utumishi wa Kristo; salamu zangu pia kwa rafiki yangu Staku. Nisalimieni Apele ambaye uaminifu wake kwa Kristo umethibitishwa. Salamu zangu kwa wote walio nyumbani mwa Aristobulo. Salamu zangu kwa Herodiana, mwananchi mwenzangu; na kwa jamaa yote ya Narkisi iliyojiunga na Bwana. Nisalimieni Trufena na Trufosa wanaofanya kazi katika utumishi wa Bwana, na rafiki yangu Persi ambaye amefanya mengi kwa ajili ya Bwana. Nisalimieni Rufo, mtu hodari sana katika kazi ya Bwana, na mama yake ambaye ni mama yangu pia. Nisalimieni Asunkrito, Flegoni, Herme, Patroba, Herma na ndugu wote walio pamoja nao. Nisalimieni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa, pamoja na watu wote wa Mungu walio pamoja nao. Salimianeni nyinyi kwa nyinyi kwa ishara ya upendo. Salamu kwenu kutoka kwa makanisa yote ya Kristo. Ndugu zangu, nawasihi mwafichue wote wanaosababisha mafarakano na kuwafanya watu wengine waanguke, kinyume cha mafundisho mliyofundishwa. Jiepusheni na watu hao, maana watu wa namna hiyo hawamtumikii Kristo Bwana wetu, bali wanayatumikia matumbo yao wenyewe. Kwa maneno yao matamu na hotuba za kubembeleza hupotosha mioyo ya watu wanyofu. Kila mtu amesikia juu ya utii wenu katika mambo mema, na bila hatia kuhusu mambo mabaya. Naye Mungu aliye chanzo cha amani hatakawia kumponda Shetani chini ya miguu yenu. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nanyi. Timotheo, mfanyakazi mwenzangu, anawasalimu. Hali kadhalika Lukio, Yasoni, na Sosipateri, wananchi wenzangu, wanawasalimu. Nami Tertio, ninayeandika barua hii, nawasalimuni kwa jina la Bwana. Gayo, mwenyeji wangu, pamoja na kanisa lote linalokutana kwake, anawasalimu. Erasto, mweka hazina wa mji huu, pamoja na Kwarto, wanawasalimu. [ Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nanyi nyote. Amina.]

Shirikisha
Soma Waroma 16

Waroma 16:1-24 Swahili Revised Union Version (SRUV)

Namkabidhi kwenu Fibi, dada yetu, aliye mhudumu wa kanisa lililoko Kenkrea; ili mmpokee katika Bwana, kama iwapasavyo watakatifu; mkamsaidie katika neno lolote atakalohitaji kwenu; kwa sababu yeye naye amekuwa msaidizi wa watu wengi, akanisaidia mimi pia. Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika nyumba yao. Nisalimieni Epaineto, mpenzi wangu, aliye malimbuko ya Asia kwa Kristo. Nisalimieni Mariamu, aliyejishughulisha sana kwa ajili yenu. Nisalimieni Androniko na Yunia, jamaa zangu, waliofungwa pamoja nami, ambao ni maarufu miongoni mwa mitume; nao walikuwa katika Kristo kabla yangu. Nisalimieni Ampliato, mpenzi wangu katika Bwana. Nisalimieni Urbano, mtenda kazi pamoja nami katika Kristo, na Stakisi, mpenzi wangu. Nisalimieni Apele, mwenye kukubaliwa katika Kristo. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Aristobulo. Nisalimieni Herodioni, jamaa yangu. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Narkiso, walio katika Bwana. Nisalimieni Trifaina na Trifosa, wenye bidii katika Bwana. Nisalimieni Persisi, mpendwa aliyejitahidi sana katika Bwana. Nisalimieni Rufo, mteule katika Bwana, na mamaye, aliye mama yangu pia. Nisalimieni Asinkrito, Flegoni, Herme, Patroba, Herma, na ndugu walio pamoja nao. Nisalimieni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa, na watakatifu wote walio pamoja nao. Salimianeni kwa busu takatifu. Makanisa yote ya Kristo yawasalimu. Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao. Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu. Maana utii wenu umewafikia watu wote; basi nafurahi kwa ajili yenu, lakini nataka ninyi kuwa wenye hekima katika mambo mema, na wasio na hatia katika mambo mabaya. Naye Mungu wa amani atamponda Shetani chini ya miguu yenu upesi. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi. [Amina.] Timotheo, mtenda kazi pamoja nami, awasalimu, na Lukio, na Yasoni, na Sosipatro, jamaa zangu. Mimi Tertio, niliyeandika waraka huu, nawasalimu katika Bwana. Gayo, mwenyeji wangu, na wa kanisa lote pia, awasalimu. Erasto, wakili wa mji, na Kwarto, ndugu yetu, wanawasalimu. [ Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi nyote. Amina.]

Shirikisha
Soma Waroma 16

Waroma 16:1-24 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)

Namkabidhi kwenu Fibi, ndugu yetu, aliye mhudumu wa kanisa lililoko Kenkrea; kwamba mmpokee katika Bwana, kama iwapasavyo watakatifu; mkamsaidie katika neno lo lote atakalohitaji kwenu; kwa sababu yeye naye amekuwa msaidizi wa watu wengi, akanisaidia mimi pia. Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika nyumba yao. Nisalimieni Epaineto, mpenzi wangu, aliye malimbuko ya Asia kwa Kristo. Nisalimieni Mariamu, aliyejitaabisha sana kwa ajili yenu. Nisalimieni Androniko na Yunia, jamaa zangu, waliofungwa pamoja nami, ambao ni maarufu miongoni mwa mitume; nao walikuwa katika Kristo kabla yangu. Nisalimieni Ampliato, mpenzi wangu katika Bwana. Nisalimieni Urbano, mtenda kazi pamoja nami katika Kristo, na Stakisi, mpenzi wangu. Nisalimieni Apele, mwenye kukubaliwa katika Kristo. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Aristobulo. Nisalimieni Herodioni, jamaa yangu. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Narkiso, walio katika Bwana. Nisalimieni Trifaina na Trifosa, wenye bidii katika Bwana. Nisalimieni Persisi, mpenzi aliyejitahidi sana katika Bwana. Nisalimieni Rufo, mteule katika Bwana, na mamaye, aliye mama yangu pia. Nisalimieni Asinkrito, Flegoni, Herme, Patroba, Herma, na ndugu walio pamoja nao. Nisalimieni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa, na watakatifu wote walio pamoja nao. Salimianeni kwa busu takatifu. Makanisa yote ya Kristo yawasalimu. Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao. Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu. Maana utii wenu umewafikilia watu wote; basi nafurahi kwa ajili yenu, lakini nataka ninyi kuwa wenye hekima katika mambo mema, na wajinga katika mambo mabaya. Naye Mungu wa amani atamseta Shetani chini ya miguu yenu upesi. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi. [Amina.] Timotheo, mtenda kazi pamoja nami, awasalimu, na Lukio, na Yasoni, na Sosipatro, jamaa zangu. Mimi Tertio, niliyeandika waraka huu, nawasalimu katika Bwana. Gayo, mwenyeji wangu na wa Kanisa lote pia awasalimu. Erasto, wakili wa mji, awasalimu, na Kwarto, ndugu yetu. [ Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi nyote. Amina.]

Shirikisha
Soma Waroma 16

Waroma 16:1-24 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)

Napenda kumtambulisha kwenu dada yetu Foibe, mtumishi katika kanisa la Kenkrea. Naomba mpokeeni katika Bwana ipasavyo watakatifu na kumpa msaada wowote atakaohitaji kutoka kwenu, kwa maana yeye amekuwa msaada kwa watu wengi, mimi nikiwa miongoni mwao. Wasalimuni Prisila na Akila, watumishi wenzangu katika Kristo Yesu. Wao walihatarisha maisha yao kwa ajili yangu; wala si mimi tu ninayewashukuru bali pia makanisa yote ya watu wa Mataifa. Lisalimuni pia kanisa linalokutana nyumbani mwao. Msalimuni rafiki yangu mpendwa Epaineto, aliyekuwa mtu wa kwanza kumwamini Kristo huko jimbo la Asia. Msalimuni Mariamu, aliyefanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu. Wasalimuni Androniko na Yunia, jamaa zangu ambao wamekuwa gerezani pamoja nami. Wao ni maarufu miongoni mwa mitume, nao walikuwa katika Kristo kabla yangu. Msalimuni Ampliato, yeye nimpendaye katika Bwana. Msalimuni Urbano, mtendakazi mwenzetu katika Kristo, pamoja na rafiki yangu mpendwa Stakisi. Msalimuni Apele aliyejaribiwa na akaithibitisha imani yake katika Kristo. Wasalimuni wote walio nyumbani mwa Aristobulo. Msalimuni ndugu yangu Herodioni. Wasalimuni wote walio nyumbani mwa Narkiso walio katika Bwana. Wasalimuni Trifaina na Trifosa, wale wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana. Msalimuni rafiki yangu mpendwa Persisi, mwanamke mwingine aliyefanya kazi kwa bidii katika Bwana. Msalimuni Rufo, mteule katika Bwana, pamoja na mama yake, ambaye amekuwa mama kwangu pia. Wasalimuni Asinkrito, Flegoni, Herme, Patroba, Herma na ndugu wote walio pamoja nao. Wasalimuni Filologo, Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa na watakatifu wote walio pamoja nao. Salimianeni kwa busu takatifu. Makanisa yote ya Kristo yanawasalimu. Ndugu zangu, nawasihi mjihadhari na kujiepusha na wale watu waletao matengano na kuweka vikwazo mbele yenu dhidi ya mafundisho mliyojifunza. Kwa maana watu kama hao hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali wanatumikia tamaa zao wenyewe. Kwa kutumia maneno laini na ya kubembeleza, hupotosha mioyo ya watu wajinga. Kila mtu amesikia kuhusu utii wenu, nami nimejawa na furaha tele kwa ajili yenu. Lakini nataka mwe na hekima katika mambo mema na bila hatia katika mambo maovu. Mungu wa amani atamponda Shetani chini ya miguu yenu upesi. Neema ya Bwana wetu Yesu iwe nanyi. Amen. Timotheo, mtendakazi mwenzangu anawasalimu. Vivyo hivyo Lukio, Yasoni, na Sosipatro, ndugu zangu. Mimi, Tertio, niliye mwandishi wa waraka huu, nawasalimu katika Bwana. Gayo, ambaye ni mwenyeji wangu na wa kanisa lote, anawasalimu. Erasto, mweka hazina wa mji huu, pamoja na Kwarto ndugu yetu pia wanawasalimu. [ Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe pamoja nanyi nyote. Amen.]

Shirikisha
Soma Waroma 16