Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Yeremia 31:1-14

Yeremia 31:1-14 Biblia Habari Njema (BHN)

Mwenyezi-Mungu asema: “Wakati utakuja ambapo nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Israeli nao watakuwa watu wangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Watu walionusurika kuuawa niliwaneemesha jangwani. Wakati Israeli alipotafuta kupumzika, mimi Mwenyezi-Mungu nilimtokea kwa mbali. Nami nimekupenda kwa mapendo ya daima, kwa hiyo nimeendelea kuwa mwaminifu kwako. Nitakujenga upya nawe utajengeka, ewe Israeli uliye mzuri! Utazichukua tena ngoma zako ucheze kwa furaha na shangwe. Utapanda tena mizabibu juu ya milima ya Samaria; wakulima watapanda mbegu na kuyafurahia mazao yake! Maana siku yaja ambapo mlinzi atapiga mbiu katika vilima vya Efraimu: ‘Amkeni, twende juu mpaka Siyoni kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.’” Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Imbeni kwa furaha kwa ajili ya Yakobo, pigeni vigelegele kwa ajili ya taifa kuu, tangazeni, shangilieni na kusema: ‘Mwenyezi-Mungu na awaokoe watu wake, amewaletea ukombozi waliobaki wa Israeli!’ Tazama, nitawaleta kutoka nchi ya kaskazini, nitawakusanya kutoka miisho ya dunia. Wote watakuwapo hapo; hata vipofu na vilema, wanawake waja wazito na wanaojifungua; umati mkubwa sana utarudi hapa. Watarudi wakiwa wanatoa machozi, nitawarudisha nikiwafariji; nitawapitisha kando ya vijito vya maji, katika njia iliyonyoka ambamo hawatajikwaa; maana mimi nimekuwa baba wa Israeli, Efraimu ni mzaliwa wangu wa kwanza. Enyi mataifa, sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu, litangazeni katika nchi za mbali, semeni: ‘Aliyemtawanya Israeli, atamkusanya, atamtunza kama mchungaji atunzavyo kondoo wake.’ Maana mimi Mwenyezi-Mungu nimemkomboa Yakobo, nimemwokoa kutoka kwa wenye nguvu kuliko yeye. Watakuja na kuimba kwa sauti juu ya mlima Siyoni, wataona fahari juu ya wema wangu mimi Mwenyezi-Mungu, kwa nafaka, divai na mafuta niwapavyo, kwa kondoo na ng'ombe kadhalika; maisha yao yatakuwa kama bustani iliyotiliwa maji, wala hawatadhoofika tena. Ndipo wasichana wao watafurahi na kucheza, vijana na wazee watashangilia kwa furaha. Nitageuza maombolezo yao kuwa furaha, nitawafariji na kuwapa furaha badala ya huzuni. Nitawashibisha makuhani kwa vinono, nitawaridhisha watu wangu kwa wema wangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Shirikisha
Soma Yeremia 31

Yeremia 31:1-14 Swahili Revised Union Version (SRUV)

Wakati huo, asema BWANA, nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Israeli, nao watakuwa watu wangu. BWANA asema hivi, Watu wale walioachwa na upanga walipata neema jangwani; yaani, Israeli, hapo nilipokwenda kumstarehesha. BWANA alinitokea zamani, akisema, Naam nimekupenda kwa upendo wa milele, ndiyo maana nimekuvuta kwa fadhili zangu. Mara ya pili nitakujenga, nawe utajengwa, Ee bikira wa Israeli mara ya pili utapambwa kwa matari yako, nawe utatokea katika michezo yao wanaofurahi. Mara ya pili utapanda mizabibu juu ya milima ya Samaria; wapanzi watapanda, nao watayafurahia matunda yake. Maana kutakuwa siku moja, ambayo walinzi watalia juu ya vilima vya Efraimu, Inukeni, tukaende Sayuni, kwa BWANA, Mungu wetu. Maana BWANA asema hivi, Mwimbieni Yakobo kwa furaha, mkampigie kelele mkuu wa mataifa, tangazeni, sifuni, mkaseme, Ee BWANA, uwaokoe watu wako, mabaki ya Israeli. Tazama, nitawaleta toka nchi ya kaskazini, na kuwakusanya katika miisho ya dunia, na pamoja nao watakuja walio vipofu, na hao wachechemeao, mwanamke mwenye mimba, na yeye pia aliye na uchungu wa kuzaa; watarudi huko, jeshi kubwa. Watakuja kwa kulia, na kwa maombi nitawaongoza; nitawapitisha kwenye mito ya maji, katika njia iliyonyoka; katika njia hiyo hawatajikwaa; maana mimi ni baba wa Israeli, na Efraimu ni mzaliwa wa kwanza wangu. Lisikieni neno la BWANA, enyi mataifa, litangazeni visiwani mbali; mkaseme, Aliyemtawanya Israeli atamkusanya, na kumlinda, kama mchungaji alindavyo kundi lake. Kwa maana BWANA amemweka huru Yakobo, amemkomboa mkononi mwake aliyekuwa hodari kuliko yeye. Nao watakuja, na kuimba katika mlima Sayuni, wataukimbilia wema wa BWANA, nafaka, na divai, na mafuta, na wachanga wa kondoo na wa ng'ombe; na roho zao zitakuwa kama bustani iliyotiwa maji; wala hawatahuzunika tena kabisa. Ndipo bikira atafurahi katika kucheza, na vijana na wazee pamoja; maana nitageuza masikitiko yao kuwa furaha, nami nitawafariji, na kuwafurahisha waache huzuni zao. Nami nitaishibisha roho ya makuhani kwa unono, na watu wangu watashiba kwa wema wangu, asema BWANA.

Shirikisha
Soma Yeremia 31

Yeremia 31:1-14 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)

Wakati huo, asema BWANA, nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Israeli, nao watakuwa watu wangu. BWANA asema hivi, Watu wale walioachwa na upanga walipata neema jangwani; yaani, Israeli, hapo nilipokwenda kumstarehesha. BWANA alinitokea zamani, akisema, Naam nimekupenda kwa upendo wa milele, ndiyo maana nimekuvuta kwa fadhili zangu. Mara ya pili nitakujenga, nawe utajengwa, Ee bikira wa Israeli mara ya pili utapambwa kwa matari yako, nawe utatokea katika michezo yao wanaofurahi. Mara ya pili utapanda mizabibu juu ya milima ya Samaria; wapanzi watapanda, nao watayafurahia matunda yake. Maana kutakuwa siku moja, ambayo walinzi watalia juu ya vilima vya Efraimu, Inukeni, tukaende Sayuni, kwa BWANA, Mungu wetu. Maana BWANA asema hivi, Mwimbieni Yakobo kwa furaha, mkampigie kelele mkuu wa mataifa, tangazeni, sifuni, mkaseme, Ee BWANA, uwaokoe watu wako, mabaki ya Israeli. Tazama, nitawaleta toka nchi ya kaskazini, na kuwakusanya katika miisho ya dunia, na pamoja nao watakuja walio vipofu, na hao wachechemeao, mwanamke mwenye mimba, na yeye pia aliye na utungu wa kuzaa; watarudi huko, jeshi kubwa. Watakuja kwa kulia, na kwa maombi nitawaongoza; nitawaendesha penye mito ya maji, katika njia iliyonyoka; katika njia hiyo hawatajikwaa; maana mimi ni baba wa Israeli, na Efraimu ni mzaliwa wa kwanza wangu. Lisikieni neno la BWANA, enyi mataifa, litangazeni visiwani mbali; mkaseme, Aliyemtawanya Israeli atamkusanya, na kumlinda, kama mchungaji alindavyo kundi lake. Kwa maana BWANA amemweka huru Yakobo, amemkomboa mkononi mwake aliyekuwa hodari kuliko yeye. Nao watakuja, na kuimba katika mlima Sayuni, wataukimbilia wema wa BWANA, nafaka, na divai, na mafuta, na wachanga wa kondoo na wa ng’ombe; na roho zao zitakuwa kama bustani iliyotiwa maji; wala hawatahuzunika tena kabisa. Ndipo bikira atafurahi katika kucheza, na vijana na wazee pamoja; maana nitageuza masikitiko yao kuwa furaha, nami nitawafariji, na kuwafurahisha waache huzuni zao. Nami nitaishibisha roho ya makuhani kwa unono, na watu wangu watashiba kwa wema wangu, asema BWANA

Shirikisha
Soma Yeremia 31

Yeremia 31:1-14 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)

“Wakati huo, nitakuwa Mungu wa koo zote za Israeli nao watakuwa watu wangu,” asema BWANA. Hili ndilo asemalo BWANA: “Watu watakaopona upanga watapata upendeleo jangwani; nitakuja niwape Israeli pumziko.” BWANA alitutokea wakati uliopita, akisema: “Nimekupenda kwa upendo wa milele, nimekuvuta kwa wema. Nitakujenga tena nawe utajengeka upya, ewe Bikira Israeli. Utachukua tena matari yako na kwenda kucheza na wenye furaha. Utapanda tena shamba la mizabibu juu ya vilima vya Samaria, wakulima watapanda na kufurahia matunda yake. Itakuja siku wakati walinzi watakapowapigia kelele juu ya vilima vya Efraimu wakisema, ‘Njooni, twendeni juu Sayuni, kwake BWANA Mungu wetu.’ ” Hili ndilo asemalo BWANA: “Mwimbieni Yakobo kwa furaha, mpigieni kelele aliye mkuu wa mataifa. Zifanyeni sifa zenu zisikike, nanyi mseme, ‘Ee BWANA, okoa watu wako, mabaki ya Israeli.’ Tazama, nitawaleta kutoka nchi ya kaskazini na kuwakusanya kutoka miisho ya dunia. Miongoni mwao watakuwepo vipofu na viwete, mama wajawazito na wenye utungu wa kuzaa. Umati mkubwa wa watu utarudi. Watakuja wakilia; wataomba wakati ninawarudisha. Nitawaongoza kando ya vijito vya maji katika mapito yaliyo tambarare ambapo hawatajikwaa, kwa sababu mimi ndimi baba wa Israeli, naye Efraimu ni mzaliwa wangu wa kwanza. “Sikieni neno la BWANA, enyi mataifa, litangazeni katika nchi za pwani ya mbali: ‘Yeye aliyewatawanya Israeli atawakusanya na atalichunga kundi lake la kondoo kama mchungaji.’ Kwa kuwa BWANA atamlipia fidia Yakobo na kuwakomboa mkononi mwa walio na nguvu kuliko wao. Watakuja na kupiga kelele kwa furaha katika miinuko ya Sayuni; watashangilia ukarimu wa BWANA: nafaka, divai mpya na mafuta, wana-kondoo wachanga na ndama wa makundi ya ngʼombe nitakaowapa. Watakuwa kama bustani iliyonyeshewa vizuri, wala hawatahuzunika tena. Kisha wanawali watacheza na kufurahi, vijana waume na wazee pia. Nitageuza maombolezo yao kuwa furaha, nitawapa faraja na furaha badala ya huzuni. Nitawashibisha makuhani kwa wingi, nao watu wangu watajazwa kwa ukarimu wangu,” asema BWANA.

Shirikisha
Soma Yeremia 31

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha