Zaburi 79
79
Zaburi 79
Maombi kwa ajili ya wokovu wa taifa
Zaburi ya Asafu.
1 Ee Mungu, mataifa yameuvamia urithi wako,
wamelinajisi Hekalu lako takatifu,
wameifanya Yerusalemu kuwa magofu.
2 Wametoa maiti za watumishi
kuwa chakula cha ndege wa angani
na nyama ya watakatifu wako
kwa wanyama wa nchi.
3 Wamemwaga damu kama maji
kuzunguka Yerusalemu yote,
wala hakuna yeyote wa kuwazika.
4 Tumekuwa kitu cha aibu kwa majirani zetu,
cha dharau na mzaha kwa wale wanaotuzunguka.
5 Hata lini, Ee Bwana? Je, wewe utakasirika milele?
Wivu wako utawaka kama moto hadi lini?
6 Mwaga ghadhabu yako kwa mataifa yasiyokukubali,
juu ya falme za hao wasioliitia jina lako,
7kwa maana wamemrarua Yakobo
na kuharibu nchi ya makao yake.
8 Usituhesabie dhambi za baba zetu,
huruma yako na itujie hima,
kwa maana tu wahitaji mno.
9 Ee Mungu Mwokozi wetu, utusaidie,
kwa ajili ya utukufu wa jina lako;
tuokoe na kutusamehe dhambi zetu
kwa ajili ya jina lako.
10 Kwa nini mataifa waseme,
“Yuko wapi Mungu wenu?”
Mbele ya macho yetu,
dhihirisha kati ya mataifa
kwamba unalipiza kisasi damu iliyomwagwa
ya watumishi wako.
11 Kilio cha huzuni cha wafungwa kifike mbele zako;
kwa nguvu za mkono wako
hifadhi wale waliohukumiwa kufa.
12 Walipize majirani zetu mara saba
aibu walizovurumisha kwako, Ee Bwana.
13 Ndipo sisi watu wako, kondoo wa malisho yako,
tutakusifu milele;
tutasimulia sifa zako
kizazi hadi kizazi.
Iliyochaguliwa sasa
Zaburi 79: NEN
Kuonyesha
Nakili
Linganisha
Shirikisha
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Holy Bible, Kiswahili Contemporary Version™ (Neno: Biblia Takatifu™) | Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. | Used with permission. All rights reserved worldwide.
Biblica® Cross Reference System | Copyright © 2025 by Biblica, Inc. | Used with permission. All rights reserved worldwide.