YouVersion Logo
Search Icon

Hesabu 35

35
Miji ya Walawi
1Yawe akasema na Musa katika mabonde ya Moabu, ngambo ya muto Yordani karibu na Yeriko, akamwambia: #Ang. Yos 21.1-42 2Uwaamuru Waisraeli kwamba kutokana na urizi watakaopewa, wawape Walawi miji ya kukaa na sehemu za malisho kandokando ya miji hiyo. 3Miji hiyo itakuwa yao, nao watakaa mule na malisho yake yatakuwa kwa ajili ya ngombe na mifugo yao pamoja na nyama wao wengine. 4Malisho ya maeneo mutakayowapa Walawi kandokando ya miji yataenea kila upande umbali wa metre mia ine na makumi tano kutoka kwenye kuta za miji hiyo. 5Kwa hiyo, eneo hilo la malisho litakuwa la metre mia tisa muraba na litaenea kila upande wa muji, muji wenyewe ukiwa katikati. Eneo hilo litakuwa malisho yao kandokando ya miji yao. 6Mutawapa Walawi miji sita ya makimbilio ambapo mutu akimwua mwenzake bila kukusudia ataruhusiwa kukimbilia. Pamoja na hiyo, mutawapa miji mingine makumi ine na miwili. 7Jumla ya miji mutakayowapa Walawi itakuwa makumi ine na minane; mutawapa miji hiyo pamoja na sehemu za malisho yake. 8Hesabu ya miji mutakayowapa Walawi katika urizi wa Waisraeli itategemea ukubwa wa kabila; kabila kubwa litatoa miji mingi na kabila dogo litatoa michache. Kila kabila litatoa miji yake kwa ajili ya Walawi kulingana na eneo litakalorizi.
Miji ya makimbilio
(Kumb 19.1-13; Yos 20.1-9)
9Yawe akaongea na Musa, akamwambia: 10Uwaambie Waisraeli kwamba wakati mutakapovuka muto Yordani na kuingia katika inchi ya Kanana, 11mutachagua miji itakayokuwa miji ya makimbilio ambamo kama mutu akimwua mwenzake bila kukusudia ataweza kukimbilia. 12Miji hiyo itakuwa pahali pa kukimbilia usalama kusudi huyo mwuaji asiuawe na mwenye kulipiza kisasi mbele ya kuhukumiwa na baraza la Waisraeli. 13Mutajitengea miji sita kwa ajili ya makimbilio. 14Kati ya miji hiyo sita mutakayotenga, mitatu ikuwe upande wa mashariki wa Yordani, na mitatu ikuwe katika inchi ya Kanana. 15Miji hii itakuwa ya makimbilio kwa ajili ya Waisraeli na wageni wa kudumu au wa muda wanaokaa pamoja nao. Mutu yeyote akimwua mwingine bila kukusudia anaweza kukimbilia huko.
16Lakini mutu akimupiga mwenzake kwa kitu cha chuma, na kumwua, mutu huyo ni mwuaji na anapaswa kuuawa. 17Mutu yeyote akimupiga mwenzake kwa jiwe, akikufa, mutu huyo ni mwuaji, anapaswa kuuawa. 18Kama akimupiga mwenzake kwa silaha ya muti ambayo inaweza kusababisha kifo, akikufa, mutu huyo ni mwuaji, na anapaswa kuuawa. 19Ndugu wa karibu wa mutu aliyeuawa atalipiza kisasi. Huyu atakapokutana na huyo mwuaji, atatimiza hukumu ya kifo.
20Vilevile, kama mutu anamuchukia mwenzake halafu, akimusukuma au kumutupia kitu kwa kumuvizia, 21au kwa kumupiga ngumi akikufa, basi mutu huyo aliyemupiga mwenzake ni mwuaji na anapaswa kuuawa. Ndugu wa karibu wa mutu aliyeuawa atalipiza kisasi atakapokutana naye.
22Lakini kama mutu akimusukuma mwenzake kwa rafla bila chuki au kumutupia kitu bila kumuvizia 23au mutu akirusha jiwe linaloweza kusababisha kifo, na kuua mutu bila kukusudia, ingawa hakukukuwa madeni kati yao na huyo aliyeua hakukusudia kumuzuru, 24basi, baraza lile litaamua kati ya huyo mwuaji na jamaa ya mutu aliyeuawa anayetaka kulipiza kisasi, kulingana na maagizo haya. 25Baraza litamwokoa mutu huyo aliyeua toka katika mikono ya ndugu ya mutu aliyeuawa, na kumurudisha katika muji wa makimbilio alimokuwa amekimbilia. Atakaa huko mpaka kufa kwa Kuhani Mukubwa wa wakati ule aliyechaguliwa kwa kupakwa mafuta matakatifu. 26Lakini huyo aliyeua akitoka inje ya muji aliokimbilia wakati wowote, 27halafu ndugu ya mutu aliyeuawa akimukuta inje ya mipaka ya muji huo wa makimbilio akimwua, huyo hatakuwa na kosa la kuua. 28Maana huyo aliyeua anapaswa kukaa ndani ya muji wa makimbilio mpaka Kuhani Mukubwa atakapokufa; lakini kisha kufa kwa Kuhani Mukubwa anaweza kurudi kwake.
29Sheria hizi zitakuwa masharti na maagizo katika vizazi vyenu vyote, pahali popote mutakapokaa.
30Mutu yeyote atakayeua mutu, atahukumiwa kifo kutokana na ushuhuda wa washuhuda wawili au zaidi; mutu yeyote hawezi kuhukumiwa kifo kutokana na ushuhuda wa mutu mumoja. #Ang. Kumb 17.6; 19.15
31Musipokee malipo yoyote kwa kuokoa maisha ya mwuaji aliyepatikana na kosa, akihukumiwa kifo; mutu huyo anapaswa kuuawa. 32Musipokee wala musikubali malipo yoyote kutoka kwa mutu aliyekimbilia katika muji wa makimbilio kwa kumuruhusu arudi kukaa kwake mbele ya kifo cha Kuhani Mukubwa. 33Mukifanya hivyo mutachafua inchi ambayo munakaa ndani yake. Umwangaji wa damu unachafua inchi, na hakuna sadaka inayoweza kutakasa inchi iliyofanyiwa mauaji isipokuwa kwa kumwua mwuaji huyo. 34Musichafue inchi ambayo munakaa ndani yake, inchi ambayo mimi ninakaa ndani yake; maana mimi Yawe ninakaa kati yenu Waisraeli.

Currently Selected:

Hesabu 35: SWC02

Highlight

Share

Compare

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in