YouVersion Logo
Search Icon

Luka 15

15
Mfano wa kondoo aliyepotea
1 # Lk 5:29-30 Basi watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia wamsikilize. 2#Lk 5:30 Mafarisayo na waandishi wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao.
3Akawaambia mfano huu, akisema, 4#Mt 18:12-14 Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na tisa nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hadi amwone? #Eze 34:11,16; Lk 19:10 5Naye akiisha kumwona, humweka mabegani pake akifurahi. 6Na afikapo nyumbani kwake, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimekwisha kumpata kondoo wangu aliyepotea. 7Nawaambia, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na tisa ambao hawana haja ya kutubu.
Mfano wa sarafu iliyopotea
8Au ni mwanamke gani aliye na shilingi kumi, akipotewa na moja, asiyewasha taa na kufagia nyumba, na kutafuta kwa bidii hadi aione? 9Na akiisha kuiona, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimeipata tena shilingi ile iliyonipotea. 10#Efe 3:10 Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.
Mfano wa mwana mpotevu na kaka yake
11Akasema, Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; 12yule mdogo akamwambia babaye, Baba, nipe sehemu ya mali iliyo uridhi wangu. Akawagawia mali yake. 13#Mit 29:3 Na baada ya siku zisizokuwa nyingi, yule mdogo akakusanya vyote, akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati. 14Alipokuwa amekwisha tumia vyote, njaa kubwa iliingia katika nchi ile, yeye naye akaanza kuhitaji. 15Akaenda akashikamana na mwenyeji mmoja wa nchi ile; naye alimpeleka shambani kwake kulisha nguruwe. 16#Mit 23:31 Akawa akitamani kujishibisha kwa maganda waliyokula nguruwe, wala hapana mtu aliyempa kitu. 17Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kubakiza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. 18#Yer 3:12,13; Zab 51:4 Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; 19sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako. 20Akaondoka, akaenda kwa babaye. Alipokuwa bado mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu. 21Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena. 22Lakini baba aliwaambia watumwa wake, Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; 23mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; 24#Efe 2:1,5; 5:14 kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia. 25Basi, yule mwanawe mkubwa alikuwa shambani na alipokuwa akija na kuikaribia nyumba, alisikia sauti ya nyimbo na nderemo. 26Akaita mtumishi mmoja, akamwuliza, Mambo haya, maana yake nini? 27Akamwambia, Ndugu yako amekuja, na baba yako amemchinja ndama aliyenona, kwa sababu amempata tena, akiwa mzima. 28#Lk 15:2 Akakasirika, akakataa kuingia ndani. Basi babaye alitoka nje, akamsihi. 29Akamjibu baba yake, akasema, Tazama, mimi nimekutumikia miaka mingapi hii, wala sijakosa amri yako wakati wowote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nisherehekee na rafiki zangu; 30lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona. 31#Yn 17:10 Akamwambia, Mwanangu, wewe u pamoja nami sikuzote, na vyote nilivyo navyo ni vyako. 32Bali ilibidi kusherehekea na kushangilia kwa kuwa huyu ndugu yako alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana.

Currently Selected:

Luka 15: SRUVDC

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy