Zaburi 118
118
Zaburi 118
Shukrani kwa ajili ya ushindi
1Mshukuruni Bwana, kwa kuwa ni mwema;
fadhili zake zadumu milele.
2Israeli na aseme sasa:
“Fadhili zake zadumu milele.”
3Nyumba ya Haruni na iseme sasa:
“Fadhili zake zadumu milele.”
4Wote wanaomcha Bwana na waseme sasa:
“Fadhili zake zadumu milele.”
5Wakati wa maumivu yangu makuu, nilimlilia Bwana,
naye akanijibu kwa kuniweka huru.
6 Bwana yuko pamoja nami, sitaogopa.
Mwanadamu anaweza kunitenda nini?
7 Bwana yuko pamoja nami,
yeye ni msaidizi wangu.
Nitawatazama adui zangu
wakiwa wameshindwa.
8Ni bora kumkimbilia Bwana
kuliko kumtumainia mwanadamu.
9Ni bora kumkimbilia Bwana
kuliko kuwatumainia wakuu.
10Mataifa yote yalinizunguka,
lakini kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali.
11Walinizunguka pande zote,
lakini kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali.
12Walinizunguka kama kundi la nyuki,
lakini walikufa haraka kama miiba iteketeayo;
kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali.
13Nilisukumwa nyuma karibu kuanguka,
lakini Bwana alinisaidia.
14 Bwana ni nguvu yangu na wimbo wangu,
yeye amefanyika wokovu wangu.
15Sauti za shangwe na ushindi
zinavuma kwenye hema za wenye haki:
“Mkono wa kuume wa Bwana
umetenda mambo makuu!
16Mkono wa kuume wa Bwana
umeinuliwa juu,
mkono wa kuume wa Bwana
umetenda mambo makuu!”
17Sitakufa, bali nitaishi,
nami nitayatangaza matendo ya Bwana.
18 Bwana ameniadhibu vikali,
lakini hakuniacha nife.
19Nifungulie malango ya haki,
nami nitaingia na kumshukuru Bwana.
20Hili ni lango la Bwana
ambalo wenye haki wanaweza kuliingia.
21Nitakushukuru, kwa kuwa ulinijibu,
umekuwa wokovu wangu.
22Jiwe walilolikataa waashi,
limekuwa jiwe kuu la pembeni.
23 Bwana ametenda hili,
nalo ni la kushangaza machoni petu.
24Hii ndiyo siku Bwana aliyoifanya,
tushangilie na kufurahi ndani yake.
25Ee Bwana, tuokoe,
Ee Bwana, utujalie mafanikio.
26Heri yule ajaye kwa jina la Bwana.
Kutoka nyumba ya Bwana tunakubariki.
27 Bwana ndiye Mungu,
naye ametuangazia nuru yake.
Mkiwa na matawi mkononi,
unganeni kwenye maandamano ya sikukuu
hadi kwenye pembe za madhabahu.
28Wewe ni Mungu wangu, nitakushukuru,
wewe ni Mungu wangu, nitakutukuza.
29Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema;
fadhili zake zadumu milele.
Currently Selected:
Zaburi 118: NENO
Highlight
Share
Copy

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Neno: Biblia Takatifu™ Neno™
Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Version™
Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.