Mathayo 22:41-46 - Compare All Versions
Mathayo 22:41-46 BHN (Biblia Habari Njema)
Mafarisayo walipokusanyika pamoja, Yesu aliwauliza, “Nyinyi mwaonaje juu ya Kristo? Je, ni mwana wa nani?” Wakamjibu, “Wa Daudi.” Yesu akawaambia, “Basi, inawezekanaje kwamba kwa nguvu ya Roho Mtakatifu Daudi anamwita yeye Bwana? Maana alisema: ‘Bwana alimwambia Bwana wangu: Keti upande wangu wa kulia, mpaka niwaweke maadui zako chini ya miguu yako.’ Basi, ikiwa Daudi anamwita Kristo ‘Bwana,’ anawezaje kuwa mwanawe?” Hakuna mtu yeyote aliyeweza kumjibu neno. Na tangu siku hiyo hakuna aliyethubutu tena kumwuliza swali.
Mathayo 22:41-46 SRUV (Swahili Revised Union Version)
Na Mafarisayo walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mnaonaje kuhusu Kristo? Ni mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi katika Roho kumwita Bwana, akisema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi katika mkono wangu wa kulia, Hata niwawekapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako? Basi, Daudi akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala hakuthubutu mtu yeyote tangu siku ile kumwuliza neno tena.
Mathayo 22:41-46 SUV (Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia)
Na Mafarisayo walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mwaonaje katika habari za Kristo? Ni mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi katika Roho kumwita Bwana, akisema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwawekapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako? Basi, Daudi akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala hakuthubutu mtu ye yote tangu siku ile kumwuliza neno tena.
Mathayo 22:41-46 NEN (Neno)
Mafarisayo wakiwa wamekusanyika pamoja, Yesu akawauliza, “Mnaonaje kuhusu Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” Wakamjibu, “Yeye ni mwana wa Daudi.” Akawaambia, “Inakuwaje basi kwamba Daudi, akinena kwa kuongozwa na Roho, anamwita Kristo ‘Bwana’? Kwa maana asema, “ ‘Bwana alimwambia Bwana wangu: “Keti mkono wangu wa kuume, hadi nitakapowaweka adui zako chini ya miguu yako.”’ Kama basi Daudi anamwita yeye ‘Bwana,’ awezaje kuwa mwanawe?” Hakuna mtu aliyeweza kumjibu Yesu neno. Tena tangu siku hiyo hakuna aliyethubutu kumuuliza tena maswali.