Hizi ni methali za Solomoni mfalme wa Israeli, mwana wa Daudi. Methali hizi zawapatia watu hekima na nidhamu; zawafanya waelewe maneno ya busara, zawafanya kuwa na nidhamu, utaratibu, uadilifu, haki na kutenda kwa usawa. Huwapatia wajinga werevu na vijana maarifa na hadhari. Mwenye hekima azisikie na kuongeza elimu yake, naye mwenye busara apate mwongozo. Mtu aelewe methali na mifano, maneno ya wenye hekima na vitendawili vyao. Kumcha Mwenyezi-Mungu ni msingi wa maarifa, lakini wapumbavu hudharau hekima na adabu. Mwanangu, sikiliza mwongozo wa baba yako, wala usiyapuuze mafundisho ya mama yako; hayo yatakupamba kilemba kichwani pako, kama mkufu shingoni mwako. Mwanangu, usikubali kushawishiwa na wenye dhambi. Wakisema: “Twende tukamvizie mtu na kumuua; njoo tukawashambulie wasio na hatia! Tutawameza kama Kuzimu wakiwa hai, watakuwa kama wale washukao Shimoni. Tutajitwalia mali zote za thamani, nyumba zetu tutazijaza nyara. Njoo ushirikiane nasi, vyote tutakavyopata tutagawana.” Wewe mwanangu usiandamane nao, uzuie mguu wako usifuatane nao. Maana wao wako mbioni kutenda maovu, haraka zao zote ni za kumwaga damu. Mtego utegwao huku ndege anaona, mtego huo wategwa bure. Wao huvizia na kujiangamiza wao wenyewe, hutega mtego wa kujinasa wao wenyewe. Ndivyo zilivyo njia za waishio kwa ukatili; ukatili huyaangamiza maisha ya wakatili.
Shirikisha
Soma Methali 1
Hifadhi mistari, soma bila mtandao, tazama klipu za mafunzo, na zaidi!
YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha
Nyumbani
Biblia
Mipango
Video