Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Yeremia 31:1-14

Yeremia 31:1-14 BHN

Mwenyezi-Mungu asema: “Wakati utakuja ambapo nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Israeli nao watakuwa watu wangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nasema: Watu walionusurika kuuawa niliwaneemesha jangwani. Wakati Israeli alipotafuta kupumzika, mimi Mwenyezi-Mungu nilimtokea kwa mbali. Nami nimekupenda kwa mapendo ya daima, kwa hiyo nimeendelea kuwa mwaminifu kwako. Nitakujenga upya nawe utajengeka, ewe Israeli uliye mzuri! Utazichukua tena ngoma zako ucheze kwa furaha na shangwe. Utapanda tena mizabibu juu ya milima ya Samaria; wakulima watapanda mbegu na kuyafurahia mazao yake! Maana siku yaja ambapo mlinzi atapiga mbiu katika vilima vya Efraimu: ‘Amkeni, twende juu mpaka Siyoni kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.’” Maana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Imbeni kwa furaha kwa ajili ya Yakobo, pigeni vigelegele kwa ajili ya taifa kuu, tangazeni, shangilieni na kusema: ‘Mwenyezi-Mungu na awaokoe watu wake, amewaletea ukombozi waliobaki wa Israeli!’ Tazama, nitawaleta kutoka nchi ya kaskazini, nitawakusanya kutoka miisho ya dunia. Wote watakuwapo hapo; hata vipofu na vilema, wanawake waja wazito na wanaojifungua; umati mkubwa sana utarudi hapa. Watarudi wakiwa wanatoa machozi, nitawarudisha nikiwafariji; nitawapitisha kando ya vijito vya maji, katika njia iliyonyoka ambamo hawatajikwaa; maana mimi nimekuwa baba wa Israeli, Efraimu ni mzaliwa wangu wa kwanza. Enyi mataifa, sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu, litangazeni katika nchi za mbali, semeni: ‘Aliyemtawanya Israeli, atamkusanya, atamtunza kama mchungaji atunzavyo kondoo wake.’ Maana mimi Mwenyezi-Mungu nimemkomboa Yakobo, nimemwokoa kutoka kwa wenye nguvu kuliko yeye. Watakuja na kuimba kwa sauti juu ya mlima Siyoni, wataona fahari juu ya wema wangu mimi Mwenyezi-Mungu, kwa nafaka, divai na mafuta niwapavyo, kwa kondoo na ng'ombe kadhalika; maisha yao yatakuwa kama bustani iliyotiliwa maji, wala hawatadhoofika tena. Ndipo wasichana wao watafurahi na kucheza, vijana na wazee watashangilia kwa furaha. Nitageuza maombolezo yao kuwa furaha, nitawafariji na kuwapa furaha badala ya huzuni. Nitawashibisha makuhani kwa vinono, nitawaridhisha watu wangu kwa wema wangu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Soma Yeremia 31

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha