Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Isaya 54

54
Upendo wa Mungu kwa Israeli
1Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Imba kwa shangwe ewe uliye tasa,
wewe ambaye hujapata kuzaa!
Paza sauti na kuimba kwa nguvu,
wewe usiyepata kujifungua mtoto.
Maana watoto wako wewe uliyeachwa
watakuwa wengi kuliko wa aliye na mume.#54:1 aya iliyokaririwa katika Gal 4:27.
2Panua nafasi hemani mwako,
tandaza mapazia hapo unapoishi,
usijali gharama zake.
Zirefushe kamba zake,
na kuimarisha vigingi vyake;
3maana utapanuka kila upande;
wazawa wako watamiliki mataifa,
miji iliyokuwa mahame itajaa watu.
4Usiogope maana hutaaibishwa tena;
usifadhaike maana hutadharauliwa tena.
Utaisahau aibu ya ujana wako,
wala hutaikumbuka tena fedheha ya ujane wako.
5Muumba wako atakuwa mume wako;
Mwenyezi-Mungu wa majeshi, ndilo jina lake,
Mtakatifu wa Israeli ndiye Mkombozi wako;
yeye aitwa ‘Mungu wa ulimwengu wote’.
6“Yerusalemu, Mwenyezi-Mungu amekuita tena wewe
kama vile mke aliyeachwa na kuhuzunika,
mke aliyeolewa akiwa kijana akaachwa.
Mungu wako anasema:
7Nilikuacha kwa muda mfupi tu;
kwa huruma nyingi, nitakurudisha.
8Kwa hasira nyingi nilikuficha uso wangu kwa kitambo,
lakini kwa fadhili za milele nitakuonea huruma.
Mimi Mwenyezi-Mungu Mkombozi wako, nimesema.
9 #54:9 Taz Mwa 9:8-17 “Nitafanya kama nilivyofanya wakati wa Noa:
Wakati ule niliapa kwamba
sitaifunika tena ardhi kwa gharika.
Basi sasa naapa kwamba sitakukasirikia tena
wala sitakukemea tena.
10Milima yaweza kutoweka,
vilima vyaweza kuondolewa,
lakini fadhili zangu hazitakuondoka,
agano langu la amani halitaondolewa.
Mimi Mwenyezi-Mungu nikuhurumiaye nimesema.
Yerusalemu mpya
11 #54:11-12 Taz Ufu 12:18-21 “Ewe Yerusalemu uliyeteseka,
uliyetaabishwa na kukosa wa kukufariji!
Nitakujenga upya kwa mawe ya thamani,
misingi yako itakuwa ya johari ya rangi ya samawati.
12Minara yako nitaijenga kwa mawe ya akiki,
malango yako kwa almasi,
na ukuta wako kwa mawe ya thamani.
13 #54:13 Taz Yoh 6:45 “Watu wako watafunzwa nami Mwenyezi-Mungu,
wanao watapata ustawi mwingi.
14Utaimarika katika uadilifu,
utakuwa mbali na dhuluma,
nawe hutaogopa kitu;
utakuwa mbali na hofu,
maana haitakukaribia.
15Mtu yeyote akija kukushambulia,
hatakuwa ametumwa nami.
Yeyote atakayekushambulia,
ataangamia mbele yako.
16“Tazama, mimi ndiye niliyemuumba mhunzi,
afukutaye moto wa makaa na kufua silaha.
Ni mimi pia niliyemuumba mwangamizi anayeangamiza.
17Silaha zote zilizoundwa kukudhuru wewe
hazitafaa chochote kile.
Mtu akikushtaki mahakamani, utamshinda.
Hilo ndilo fungu nililowapangia watumishi wangu.
Hizo ndizo haki nilizowathibitishia.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

Iliyochaguliwa sasa

Isaya 54: BHN

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha