Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Isaya 31

31
Misri haitaweza kusaidia
1Ole wao wale waendao Misri kuomba msaada,
ole wao wanaotegemea farasi,
wanaotegemea wingi wa magari yao ya vita,
na nguvu za askari wao wapandafarasi,
nao hawamtegemei Mtakatifu wa Israeli,
wala hawamwombi Mwenyezi-Mungu shauri!
2Mungu ni mwenye busara na huleta maangamizi.
Habadilishi tamko lake;
ila yuko tayari kuwakabili watu waovu
kadhalika na wasaidizi wa watendao mabaya.
3Wamisri ni binadamu tu wala si Mungu;
farasi wao nao ni wanyama tu, si roho.
Mwenyezi-Mungu akiunyosha mkono wake,
taifa linalotoa msaada litajikwaa,
na lile linalosaidiwa litaanguka;
yote mawili yataangamia pamoja.
Mungu ataulinda mji wa Yerusalemu
4Mwenyezi-Mungu aliniambia:
“Kama vile simba au mwanasimba angurumavyo
kuyakinga mawindo yake,
hata kundi la wachungaji likiitwa kumkabili,
yeye hatishiki kwa kelele zao,
wala hashtuki kwa sauti zao.
Ndivyo atakavyoshuka Mwenyezi-Mungu wa majeshi
kupigana juu ya mlima Siyoni na kilima chake.
5Kama ndege arukavyo juu ya viota vyake,
ndivyo Mwenyezi-Mungu atakavyoulinda Yerusalemu,
ataulinda na kuukomboa,
atauhifadhi na kuuokoa.
6Enyi Waisraeli,
mrudieni huyo mliyemsaliti vibaya.
7Wakati utafika ambapo nyote
mtavitupilia mbali vinyago vyenu
vya fedha na dhahabu ambavyo
mmejitengenezea kwa mikono yenu,
vikawakosesha.
8Hapo Waashuru watauawa kwa upanga,
lakini si kwa upanga wa binadamu;
naam, wataangamizwa kwa upanga
ambao ni zaidi ya ule wa binadamu.
Waashuru watakimbia
na vijana wao watafanyizwa kazi za kitumwa.
9Mfalme wao atatoroka kwa hofu,
na maofisa wao wataiacha bendera yao kwa woga.
Hayo ameyatamka Mwenyezi-Mungu
ambaye moto wake umo mjini Siyoni,
naam, tanuri lake limo mjini Yerusalemu.”

Iliyochaguliwa sasa

Isaya 31: BHN

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha