Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Zaburi 89:1-18

Zaburi 89:1-18 BHND

Ee Mwenyezi-Mungu, nitaimba fadhili zako milele; nitavitangazia vizazi vyote uaminifu wako. Natamka kuwa fadhili zako zadumu milele; uaminifu wako ni thabiti kama mbingu. Umesema: “Nimefanya agano na mteule wangu, nimemwapia mtumishi wangu Daudi: ‘Daima nitamweka mzawa wako kuwa mfalme, tena nitaudumisha ufalme wako milele.’” Mbingu na zisifu maajabu yako, ee Mwenyezi-Mungu; uaminifu wako usifiwe katika kusanyiko la watakatifu. Nani mbinguni awezaye kulinganishwa nawe ee Mwenyezi-Mungu? Nani aliye sawa nawe kati ya viumbe vya mbinguni? Wewe waogopwa katika baraza la watakatifu; wote wanaokuzunguka wanatiwa hofu kuu. Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, ni nani mwenye nguvu kama wewe, ee Mwenyezi-Mungu? Uaminifu umekuzunguka pande zote. Wewe watawala machafuko ya bahari; mawimbi yake yakiinuka, wayatuliza. Uliliponda joka Rahabu na kuliua; uliwatawanya adui zako kwa nguvu yako. Mbingu ni zako na dunia ni yako pia; ulimwengu na vitu vyote vilivyomo wewe uliviumba. Wewe uliumba kaskazini na kusini; milima Tabori na Hermoni inakusifu kwa furaha. Mkono wako una nguvu, mkono wako una nguvu na umeshinda! Uadilifu na haki ni msingi wa utawala wako; fadhili na uaminifu vyakutangulia! Heri watu wanaojua kukushangilia, wanaoishi katika mwanga wa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu. Wanafurahi mchana kutwa kwa sababu yako, na kukusifu kwa ajili ya uadilifu wako. Wewe ndiwe fahari na nguvu yao; kwa wema wako twapata ushindi. Ee Mwenyezi-Mungu, mlinzi wetu ni wako, mfalme wetu ametoka kwako ewe Mtakatifu wa Israeli.

Soma Zaburi 89

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na Zaburi 89:1-18

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha