Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Zaburi 18

18
Shukrani za kifalme kwa ushindi
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi mtumishi wa BWANA, aliyomwambia BWANA wakati BWANA alipomwokoa kutoka kwa mkono wa adui zake wote na kutoka kwa mkono wa Sauli. Akasema:
1 # Kum 32:4; 1 Sam 2:2; Zab 91:2 Wewe, BWANA, nguvu yangu, nakupenda sana;
2 # Ebr 2:13 BWANA ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu,
Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia,
Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu.
3 # Zab 76:4 Namwita BWANA astahiliye kusifiwa,
Hivyo nitaokoka na adui zangu.
4 # Zab 116:3 Kamba za mauti zilinizunguka,
Mafuriko ya uovu yakanitia hofu.
5Kamba za kuzimu zilinizunguka,
Mitego ya mauti ikanikabili.
6Katika shida yangu nilimwita BWANA,
Na kumlalamikia Mungu wangu.
Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake,
Kilio changu kikaingia masikioni mwake.
7 # Mdo 4:31 Ndipo nchi iliyotikisika na kutetemeka,
Misingi ya milima ikatingizika;
Ikatikisika kwa sababu alikuwa na ghadhabu.
8Kukapanda moshi kutoka puani mwake,
Moto wa kuteketeza ukatoka kinywani mwake,
Makaa ya moto yakamtoka.
9 # Isa 64:1 Aliziinamisha mbingu akashuka,
Kukawa na giza kuu chini ya miguu yake.
10 # Zab 99:1; 104:3 Akapanda juu ya kerubi akaruka,
Naam, aliruka upesi juu ya mabawa ya upepo.
11 # Zab 97:2 Alifanya giza kuwa mahali pake pa kujificha,
Kuwa hema yake ya kumzunguka.
Akiwa katika giza la mawingu mazito yaliyojaa maji.
12Toka mwangaza uliokuwa mbele zake
Kukapita mawingu yake makuu.
Ikashuka mvua ya mawe na makaa ya moto.
13 # Zab 29:3 BWANA alinguruma kutoka mbinguni,
Yeye Aliye Juu akaitoa sauti yake,
Mvua ya mawe na makaa ya moto.
14 # Hes 24:8; Kum 32:23; Ayu 6:4; Zab 21:12 Akaipiga mishale yake akawatawanya,
Naam, umeme mwingi sana, akawatapanya.
15Ndipo ilipoonekana mikondo ya maji,
Misingi ya ulimwengu ikafichuliwa,
Ee BWANA, kwa kukemea kwako,
Kwa mvumo wa pumzi ya puani mwako.
16 # Zab 144:7 Alinishukia kutoka juu, akanichukua,
Na kunitoa katika maji mengi.
17Akaniokoa na adui yangu mwenye nguvu,
Na wale walionichukia,
Maana walikuwa na nguvu kuliko mimi.
18Walinikabili siku ya msiba wangu,
Lakini BWANA alikuwa tegemeo langu.
19 # Zab 118:5 Akanitoa akanipeleka panapo nafasi,
Aliniponya kwa kuwa alipendezwa nami.
20 # 2 Sam 22:21; Mit 18:10; Mt 6:4; 1 Kor 3:8 BWANA alinitendea sawasawa na haki yangu,
Sawasawa na usafi wa mikono yangu akanilipa.
21Maana nimezishika njia za BWANA,
Wala sikumwasi Mungu wangu.
22Hukumu zake zote zilikuwa mbele yangu,
Wala amri zake sikubandukana nazo.
23Nami nilikuwa mkamilifu mbele zake,
Nikajilinda na uovu wangu.
24 # Rut 2:12; Mt 10:41,42 Ndipo BWANA akanilipa sawasawa na haki yangu,
Sawasawa na usafi wa mikono yangu mbele zake.
25 # Mt 18:32-35 Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili;
Kwa mkamilifu utajionesha kuwa mkamilifu;
26 # Law 26:23 Kwake ajitakasaye utajionesha kuwa mtakatifu;
Na kwa mpotovu utajionesha kuwa mkaidi.
27 # Mit 6:17 Maana Wewe wawaokoa watu wanaoonewa,
Na macho ya kiburi utayadhili.
28 # Ayu 18:6 Kwa kuwa Wewe unaiwasha taa yangu;
BWANA Mungu wangu aniangazia giza langu.
29Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi,
Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.
30 # Kum 32:4; Rum 12:3; Ufu 15:3; Zab 12:6 Mungu, njia yake ni kamilifu,
Ahadi ya BWANA imehakikishwa,
Yeye ndiye ngao yao.
Wote wanaomkimbilia.
31 # Kum 32:31; 2 Sam 22:32 Maana ni nani aliye Mungu ila BWANA?
Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu?
32Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu,
Naye anaifanya kamilifu njia yangu.
33 # Hab 3:19 Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu,
Na kunisimamisha mahali pangu pa juu.
34Anaifundisha mikono yangu vita,
Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba.
35Nawe umenipa ngao ya wokovu wako,
Mkono wako wa kulia umenitegemeza,
Na unyenyekevu wako umenikuza.
36Umezipanulia nafasi hatua zangu,
Na miguu yangu haikuteleza.
37Nitawafuatia adui zangu na kuwapata,
Wala sitarudi nyuma hadi wakomeshwe.
38Nitawapigapiga wasiweze kusimama,
Wataanguka chini ya miguu yangu.
39Nawe umenipa nguvu za vita,
Hunitiishia chini yangu walionishambulia.
40Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo,
Nao walionichukia nimewakatilia mbali.
41 # Mit 1:28 Walipiga yowe, lakini hakuna wa kuokoa,
Walimwita BWANA lakini hakuwajibu,
42Nikawaponda kama mavumbi mbele ya upepo,
Nikawatupa nje kama matope ya njiani.
43Umeniokoa kutoka kwa mashindano ya watu,
Umenifanya niwe kichwa cha mataifa.
Watu nisiowajua walinitumikia.
44Mara tu waliposikia habari zangu,
wakanitii.
Wageni walinijia wakinyenyekea.
45 # Mik 7:17 Wageni nao walitepetea,
Walitoka katika ngome zao wakitetemeka.
46 # Yer 10:10 BWANA ndiye aliye hai;
Na ahimidiwe mwamba wangu;
Na atukuzwe Mungu wa wokovu wangu;
47Ndiye Mungu anilipizaye kisasi;
Na kuwatiisha watu chini yangu.
48 # Zab 59:1 Huniponya na adui zangu;
Naam, waniinua juu yao walioniinukia,
Na kuniponya na mtu mjeuri.
49 # Rum 15:9 Basi, BWANA, nitakushukuru kati ya mataifa,
Nami nitaliimbia jina lako.
50 # Zab 144:10 Ampa mfalme wake wokovu mkuu,
Amfanyia fadhili masihi#18:50 Au, mtiwa mafuta. wake,
Daudi na wazawa wake hata milele.

Iliyochaguliwa sasa

Zaburi 18: SRUV

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha