Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Pet UTANGULIZI

UTANGULIZI
Waraka huu wa Kwanza wa Petro ulikuwa wa “mzee” kule Rumi (5:1) au Babeli (5:13) - jina la kupanga la Rumi walilotumia Wayahudi na Wakristo katika maandishi yaliyohusu nyakati za mwisho (maandishi ya kiapokalipti, tazama k.m. Ufu 17:5-6), kwa viongozi waliosimamia makanisa ya Asia Ndogo (1:1; 5:2-3). Katika 5:12 kuna maneno yanayomvutia msomaji: “Kwa mkono wa Silwano”, maneno ambayo yanaweza kuwa na maana ya kwamba Petro aliweka sahihi yake katika waraka ambao Silwano aliandika kama katibu wake. Silwano ni Kilatini cha jina la Kiaramu “Sila” na inawezekana kuchukua kwamba hapa anahusika yule msafiri mwenzake Paulo (Mdo 15:22–18:5; rejea pia 2 Kor 1:19; 1 The 1:1). Wengine wanafikiri Petro alimtuma Silwano kupeleka waraka huu kwa walengwa kabla ya kufa kwake (yapata mwaka 64 B.K.).
Lengo kuu la Waraka huu ni kuwatia moyo wasomaji wake ambao wanakabiliwa na shida na mateso wadumishe mwenendo safi wa maisha wanayostahili wale wanaotangaza imani katika Yesu Kristo (1:6-7; 2:12; 3:17; 4:1,4,12-16,19). Katika 2:4-10 kanisa ni mrithi wa kweli wa lile agano la Mungu na katika 4:1-6 Wakristo wanapaswa kuonyesha kwa maisha yao wenyewe kwamba wamekataa tamaa za wanadamu na mitindo ya watu wa mataifa (4:1-6).
Kwa mfululizo wa mashauri au mawaidha, mwandishi anawakumbusha walengwa wake Wakristo kwamba wao ni familia ya Mungu mwenyewe (1:25), “taifa takatifu” (2:9), kwamba wanapaswa kujistahi kwa kila namna wapate kuwa mfano mwema (2:11–4:6) hata katika mazingira ambayo mwenendo wao mwema utaonekena kwa watu wa ulimwengu kuwa ni jambo lisiloeleweka na kudharauliwa au kuchukiwa. Katika sehemu hii ya 2:11–4:6 pia kuna mashauri kuhusu kutimiza wajibu katika mazingira mbalimbali ambayo yanahusiana na watu (2:13-14,17-18; 3:1-7) na kuwa na mwenendo unaofaa unaolingana na umoja wa kindugu katika kanisa, umoja ambao una msingi katika upendo ambao ndio unaotakiwa daima kwa sababu “mwisho wa mambo yote umekaribia” (4:7).
Mwisho mwandishi anatoa mashauri kadhaa kwa wenye madaraka katika kanisa (5:1-4) na mengine kwa waumini kwa jumla (5:5-11). Kisha salamu kadhaa kwa walengwa (5:5-12) kutoka kwa kanisa la Babeli… “wenzenu… hapa Babeli” na “mwanangu Marko” (5:13-14).

Iliyochaguliwa sasa

1 Pet UTANGULIZI: SUV

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha