Ufunuo 7:1-12
Ufunuo 7:1-12 NENO
Baada ya hili nikaona malaika wanne wakiwa wamesimama katika pembe nne za dunia, wakizuia hizo pepo nne za dunia, ili pasiwe na upepo utakaovuma juu ya nchi au juu ya bahari au juu ya mti wowote. Nikaona malaika mwingine akipanda kutoka mawio ya jua akiwa na muhuri wa Mungu aliye hai. Akawaita kwa sauti kubwa wale malaika wanne waliokuwa wamepewa mamlaka ya kuidhuru nchi na bahari, akisema, “Msiidhuru nchi wala bahari, wala miti, hadi tuwe tumetia muhuri kwenye paji za nyuso za watumishi wa Mungu wetu.” Ndipo nikasikia idadi ya wale waliotiwa muhuri: elfu mia moja na arobaini na nne kutoka makabila yote ya Israeli. Kutoka kabila la Yuda elfu kumi na mbili walitiwa muhuri, kutoka kabila la Reubeni elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Gadi elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Asheri elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Naftali elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Manase elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Simeoni elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Lawi elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Isakari elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Zabuloni elfu kumi na mbili, kutoka kabila la Yusufu elfu kumi na mbili, na kutoka kabila la Benyamini elfu kumi na mbili. Baada ya hili nikatazama na hapo mbele yangu palikuwa na umati mkubwa wa watu ambao hakuna yeyote awezaye kuwahesabu, kutoka kila taifa, kila kabila, kila jamaa na kila lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi na mbele ya Mwana-Kondoo. Walikuwa wamevaa mavazi meupe na wakiwa wameshika matawi ya mitende mikononi mwao. Nao walikuwa wakipaza sauti kwa nguvu, wakisema: “Wokovu una Mungu wetu, yeye aliyeketi kwenye kile kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo!” Malaika wote walikuwa wamesimama kukizunguka kile kiti cha enzi na wale wazee, na wale viumbe wanne wenye uhai. Wakaanguka kifudifudi mbele ya hicho kiti cha enzi na kumwabudu Mungu, wakisema: “Amen! Sifa na utukufu na hekima na shukrani na heshima na uweza na nguvu viwe kwa Mungu wetu milele na milele. Amen!”