Isaya 64
64
1 Laiti ungepasua mbingu na kushuka chini,
ili milima itetemeke mbele zako!
2 Kama vile moto unavyoteketeza vijiti
na kusababisha maji kuchemka,
shuka ukafanye jina lako lijulikane kwa adui zako,
na kusababisha mataifa yatetemeke mbele zako!
3 Kwa maana ulipofanya mambo ya kutisha ambayo hatukuyatazamia,
ulishuka, nayo milima ikatetemeka mbele zako.
4 Tangu nyakati za zamani hakuna yeyote aliyesikia,
hakuna sikio lililotambua,
hakuna jicho lililomwona Mungu mwingine ila wewe,
anayetenda mambo kwa ajili ya wale wamngojeao.
5 Uliwasaidia watu wale watendao yaliyo haki kwa furaha,
wale wazikumbukao njia zako.
Lakini wakati tulipoendelea kutenda dhambi kinyume na njia zako,
ulikasirika.
Tutawezaje basi kuokolewa?
6 Sisi sote tumekuwa kama mtu aliye najisi,
nayo matendo yetu yote ya uadilifu ni kama matambaa machafu;
sisi sote tunasinyaa kama jani,
na kama upepo maovu yetu hutupeperusha.
7 Hakuna yeyote anayeliitia jina lako
wala anayejitahidi kukushika,
kwa kuwa umetuficha uso wako
na kutuacha tudhoofike kwa sababu ya dhambi zetu.
8 Lakini, Ee Bwana, wewe ndiwe Baba yetu.
Sisi ni udongo, na wewe ndiwe mfinyanzi;
sisi sote tu kazi ya mkono wako.
9 Ee Bwana, usikasirike kupita kiasi,
usizikumbuke dhambi zetu milele.
Ee Bwana, utuangalie, twakuomba,
kwa kuwa sisi sote tu watu wako.
10Miji yako mitakatifu imekuwa jangwa;
hata Sayuni ni jangwa, Yerusalemu ni ukiwa.
11 Hekalu letu takatifu na tukufu,
ambako baba zetu walikusifu wewe,
limechomwa kwa moto,
navyo vitu vyote tulivyovithamini
vimeharibika.
12 Ee Bwana, baada ya haya yote, utajizuia?
Je, utanyamaza, na kutuadhibu kupita kiasi?
Iliyochaguliwa sasa
Isaya 64: NEN
Kuonyesha
Nakili
Linganisha
Shirikisha
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Holy Bible, Kiswahili Contemporary Version™ (Neno: Biblia Takatifu™) | Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. | Used with permission. All rights reserved worldwide.
Biblica® Cross Reference System | Copyright © 2025 by Biblica, Inc. | Used with permission. All rights reserved worldwide.