Matendo 5:34-42
Matendo 5:34-42 NENO
Lakini Farisayo mmoja, jina lake Gamalieli, aliyekuwa mwalimu wa sheria, aliyeheshimiwa na watu wote, akasimama mbele ya Baraza la Wayahudi, akaamuru mitume watolewe nje kwa muda. Ndipo alipowaambia wazee wa Baraza, “Enyi wanaume wa Israeli, fikirini kwa uangalifu mnayotaka kuwatendea watu hawa. Kwa maana wakati uliopita, aliinuka mtu mmoja jina lake Theuda, alijidai kuwa yeye ni mtu maarufu, akapata wafuasi wapatao mia nne walioambatana naye. Lakini aliuawa, na wafuasi wake wote wakatawanyika, wakawa si kitu. Baada yake, alitokea Yuda Mgalilaya wakati wa kuorodhesha watu, naye akaongoza kundi la watu kuasi. Yeye pia aliuawa, nao wafuasi wake wakatawanyika. Kwa hiyo, kwa habari ya jambo hili nawashauri, jiepusheni na watu hawa. Waachieni waende zao! Kwa maana kama kusudi lao na shughuli yao imetokana na mwanadamu, haitafanikiwa. Lakini ikiwa imetoka kwa Mungu, hamtaweza kuwazuia watu hawa. Badala yake mtajikuta mnapigana na Mungu.” Wakapokea ushauri wa Gamalieli. Wakawaita mitume ndani, wakaamuru wachapwe mijeledi, kisha wakawaagiza wasinene tena kwa jina la Yesu, wakawaachia waende zao. Nao mitume wakatoka nje ya Baraza la Wayahudi, wakiwa wamejaa furaha kwa sababu wamehesabiwa kustahili kupata aibu kwa ajili ya jina la Yesu. Kila siku, Hekaluni na nyumba kwa nyumba, hawakuacha kufundisha na kuhubiri Habari Njema kwamba Yesu ndiye Kristo.


