Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Wafalme 20:1-11

1 Wafalme 20:1-11 NENO

Basi, Ben-Hadadi mfalme wa Aramu akakusanya jeshi lake lote. Akifuatana na wafalme thelathini na wawili wakiwa na farasi na magari ya vita, akakwea kuuzingira Samaria na kuishambulia kwa jeshi. Akawatuma wajumbe katika mji kwa Ahabu mfalme wa Israeli, kusema, “Hivi ndivyo asemavyo Ben-Hadadi: ‘Fedha yako na dhahabu yako ni vyangu; nao wake zako walio wazuri sana na watoto ni wangu.’ ” Mfalme wa Israeli akajibu, “Iwe kama usemavyo, bwana wangu mfalme. Mimi na vyote nilivyo navyo ni mali yako.” Wale wajumbe wakaja tena na kusema, “Hivi ndivyo asemavyo Ben-Hadadi: ‘Nimewatuma kutaka fedha yako na dhahabu, wake zako na watoto wako. Lakini kesho wakati kama huu, nitawatuma maafisa wangu kukagua jumba lako la kifalme na nyumba za maafisa wako. Watatwaa kitu unachokithamini nao watakichukua.’ ” Mfalme wa Israeli akawaita wazee wote wa nchi, akawaambia, “Tazama jinsi mtu huyu anavyochochea matatizo! Alipotuma apelekewe wake zangu na watoto wangu, fedha zangu na dhahabu yangu, sikumkatalia.” Wazee na watu wote wakajibu, “Usimsikilize, wala usiyakubali matakwa yake.” Kwa hiyo akawajibu wajumbe wa Ben-Hadadi, “Mwambieni bwana wangu mfalme, ‘Mtumishi wako atafanya yote uliyoyadai mwanzoni, lakini dai hili la sasa siwezi kulitekeleza.’ ” Wakaondoka na kupeleka jibu kwa Ben-Hadadi. Kisha Ben-Hadadi akatuma ujumbe mwingine kwa Ahabu, kusema, “Miungu waniadhibu vikali zaidi ikiwa vumbi la Samaria litatosheleza konzi moja ya kila mtu ya wale wanaofuatana nami.” Mfalme wa Israeli akajibu, “Mwambieni, ‘Yule anayevaa mavazi ya vita asije akajisifu kama yule anayevua.’ ”