Zaburi 139:1-6,13-18
Zaburi 139:1-6 Biblia Habari Njema (BHN)
Ee Mwenyezi-Mungu, wewe umenichunguza; wewe wanijua mpaka ndani. Nikiketi au nikisimama, wewe wajua; wajua kutoka mbali kila kitu ninachofikiria. Watambua nikienda au nikipumzika; wewe wazijua shughuli zangu zote. Kabla sijasema neno lolote, wewe, ee Mwenyezi-Mungu, walijua kabisa. Uko kila upande wangu, mbele na nyuma; waniwekea mkono wako kunilinda. Maarifa yako yapita akili yangu; ni makuu mno, siwezi kuyaelewa.
Zaburi 139:13-18 Biblia Habari Njema (BHN)
Wewe umeniumba, mwili wangu wote; ulinitengeneza tumboni mwa mama yangu. Nakusifu maana nimefanywa kwa namna ya ajabu, matendo yako ni ya ajabu; wewe wanijua kabisakabisa. Umbo langu halikufichika kwako nilipotungwa kwa siri na ustadi ndani ya dunia. Wewe uliniona hata kabla sijazaliwa, uliandika kila kitu kitabuni mwako; siku zangu zote ulizipanga, hata kabla ya kuweko ile ya kwanza. Ee Mungu, mawazo yako ni makuu mno; hayawezi kabisa kuhesabika. Ningeyahesabu yangekuwa mengi kuliko mchanga. Niamkapo, bado nipo pamoja nawe.
Zaburi 139:1-6 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. Wewe wajua kuketi kwangu na kusimama kwangu; Umelifahamu wazo langu tokea mbali. Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu, Umeelewa na njia zangu zote. Maana hamna neno katika ulimini wangu Usilolijua kabisa, BWANA. Umenizingira nyuma na mbele, Ukaniwekea mkono wako. Maarifa hayo ni ya ajabu, yanishinda mimi, Hayadirikiki, siwezi kuyafikia.
Zaburi 139:13-18 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu, Uliniunga tumboni mwa mama yangu. Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa Kwa njia ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, Na nafsi yangu yajua sana, Mifupa yangu haikusitirika kwako, Nilipoumbwa kwa siri, Nilipoungwa kwa ustadi katika pande za chini za nchi; Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; Kitabuni mwako ziliandikwa zote pia, Siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado. Mawazo yako ni mazito sana kwangu; Ee Mungu; nayo ni makuu sana. Kama ningeyahesabu ni mengi kuliko mchanga; Niamkapo ningali pamoja nawe.
Zaburi 139:1-6 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu; Umelifahamu wazo langu tokea mbali. Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu, Umeelewa na njia zangu zote. Maana hamna neno ulimini mwangu Usilolijua kabisa, BWANA. Umenizingira nyuma na mbele, Ukaniwekea mkono wako. Maarifa hayo ni ya ajabu, yanishinda mimi, Hayadirikiki, siwezi kuyafikia.
Zab 139:13-18 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu, Uliniunga tumboni mwa mama yangu. Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, Na nafsi yangu yajua sana, Mifupa yangu haikusitirika kwako, Nilipoumbwa kwa siri, Nilipoungwa kwa ustadi pande za chini za nchi; Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; Chuoni mwako ziliandikwa zote pia, Siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado. Mungu, fikira zako zina thamani nyingi kwangu; Jinsi ilivyo kubwa jumla yake! Kama ningezihesabu ni nyingi kuliko mchanga; Niamkapo nikali pamoja nawe.
Zaburi 139:1-6 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)
Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. Unajua ninapoketi na ninapoinuka; unatambua mawazo yangu tokea mbali. Unafahamu kutoka kwangu na kulala kwangu; unaelewa njia zangu zote. Kabla neno halijafika katika ulimi wangu, wewe walijua kikamilifu, Ee BWANA. Umenizingira nyuma na mbele; umeweka mkono wako juu yangu. Maarifa haya ni ya ajabu mno kwangu, ni ya juu sana kwangu kuyafikia.
Zaburi 139:13-18 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)
Kwa maana wewe ndiwe uliyeumba utu wangu wa ndani; uliniunga pamoja tumboni mwa mama yangu. Ninakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa namna ya ajabu na ya kutisha; kazi zako ni za ajabu, ninajua hayo kikamilifu. Umbile langu halikufichika kwako, nilipoumbwa mahali pa siri. Nilipoungwa pamoja kwa ustadi katika vilindi vya nchi, macho yako yaliniona kabla mwili wangu haujakamilika. Siku zangu zote ulizonipangia ziliandikwa katika kitabu chako kabla haijakuwa hata moja. Tazama jinsi yalivyo ya thamani mawazo yako kwangu, Ee Mungu! Jinsi jumla yake ilivyo kubwa! Kama ningezihesabu, zingekuwa nyingi kuliko mchanga: niamkapo, bado niko pamoja nawe.