Methali 24:17-34
Methali 24:17-34 Biblia Habari Njema (BHN)
Usishangilie kuanguka kwa adui yako; usifurahie moyoni mwako kujikwaa kwake, maana Mwenyezi-Mungu aonaye hayo hatapendezwa; huenda akaacha kumwadhibu. Usihangaike kwa sababu ya watenda mabaya, wala usiwaonee wivu watu waovu, maana mwovu hatakuwa na mema baadaye; taa ya uhai wake itazimwa. Mwanangu, umche Mwenyezi-Mungu na kumheshimu mfalme, wala usishirikiane na wale wasio na msimamo, maana maangamizi yao huwapata ghafla. Hakuna ajuaye maafa watakayozusha. Ifuatayo pia ni misemo ya wenye hekima: Kupendelea watu katika hukumu si vizuri. Anayemwachilia mtu mwenye hatia, hulaaniwa na watu na kuchukiwa na mataifa. Lakini wanaowaadhibu waovu watapata furaha, na baraka njema zitawajia. Jibu lililo la haki, ni kama busu la rafiki. Kwanza fanya kazi zako nje, tayarisha kila kitu shambani, kisha jenga nyumba yako. Usishuhudie bure dhidi ya jirani yako, wala usiseme uongo juu yake. Usiseme, “Nitamtenda kama alivyonitenda! Ni lazima nilipize kisasi!” Nilipitia karibu na shamba la mvivu; shamba la mzabibu la mtu mpumbavu. Nilishangaa kuona limemea miiba, magugu yamefunika eneo lake lote, na ukuta wake wa mawe umebomoka. Nilitazama, nikawaza, mwishowe nikapata funzo: Lala tu kidogo; sinzia tu kidogo! Kunja mikono yako tu upumzike! Lakini kumbuka kwamba uwapo usingizini, umaskini utakuvamia kama mnyanganyi, ufukara kama mtu mwenye silaha.
Methali 24:17-34 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Usifurahi, adui yako aangukapo; Wala moyo wako usishangilie ajikwaapo; BWANA asije akaliona hilo, likamkasirisha; Akageuzia mbali naye hasira yake. Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya; Wala usiwahusudu wabaya; Kwa maana mtu mbaya hapati thawabu; Taa ya mtu mbaya itazimika. Mwanangu, mche BWANA, na mfalme; Wala usishirikiane na wenye kigeugeu; Maana msiba wao utatokea kwa ghafla; Tena ni nani aujuaye uharibifu wa miaka yao. Haya nayo pia ni maneno ya wenye akili. Kupendelea watu katika hukumu si kwema. Amwambiaye mtu mwovu, Wewe una haki; Makabila ya watu watamlaani, taifa watamchukia. Bali kwao wakemeao furaha itakuwako; Na baraka ya kufanikiwa itawajilia. Aibusu midomo atoaye jawabu la haki. Tengeneza kazi yako huko nje, Jifanyizie kazi yako tayari shambani, Ukiisha, jenga nyumba yako. Usimshuhudie jirani yako pasipo sababu, Wala usidanganye kwa midomo yako. Usiseme, Nitamtenda kama alivyonitenda mimi; Nitamlipa mtu huyo sawasawa na tendo lake. Nilipita karibu na shamba la mvivu, Na shamba la mizabibu la mtu asiye na akili. Kumbe! Lote pia limemea miiba; Uso wake ulifunikwa kwa viwawi; Na ukuta wake wa mawe umebomoka. Ndipo nilipoangalia na kufikiri sana; Niliona, nikapata mafundisho. Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, Bado kukunja mikono upate usingizi! Hivyo, umaskini wako huja kama mnyang'anyi, Na uhitaji wako kama mtu mwenye silaha.
Methali 24:17-34 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Usifurahi, adui yako aangukapo; Wala moyo wako usishangilie ajikwaapo; BWANA asije akaliona hilo, likamkasirisha; Akageuzia mbali naye hasira yake. Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya; Wala usiwahusudu wabaya; Kwa maana mtu mbaya hapati thawabu; Taa ya mtu mbaya itazimika. Mwanangu, mche BWANA, na mfalme; Wala usishirikiane na wenye kigeugeu; Maana msiba wao utatokea kwa ghafula; Tena ni nani aujuaye uharibifu wa miaka yao. Haya nayo pia ni maneno ya wenye akili. Kupendelea watu katika hukumu si kwema. Amwambiaye mtu mwovu, Wewe una haki; Kabila za watu watamlaani, taifa watamchukia. Bali kwao wakemeao furaha itakuwako; Na baraka ya kufanikiwa itawajilia. Aibusu midomo atoaye jawabu la haki. Tengeneza kazi yako huko nje, Jifanyizie kazi yako tayari shambani, Ukiisha, jenga nyumba yako. Usimshuhudie jirani yako pasipo sababu, Wala usidanganye kwa midomo yako. Usiseme, Nitamtenda kama alivyonitenda mimi; Nitamlipa mtu huyo sawasawa na tendo lake. Nalipita karibu na shamba la mvivu, Na shamba la mizabibu la mtu asiye na akili. Kumbe! Lote pia limemea miiba; Uso wake ulifunikwa kwa viwawi; Na ukuta wake wa mawe umebomoka. Ndipo nilipoangalia na kufikiri sana; Naliona, nikapata mafundisho. Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, Bado kukunja mikono upate usingizi! Hivyo, umaskini wako huja kama mnyang’anyi, Na uhitaji wako kama mtu mwenye silaha.
Methali 24:17-34 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)
Usitazame kwa kufurahia adui yako aangukapo; wakati anapojikwaa, usiruhusu moyo wako ushangilie. BWANA asije akaona na kuchukia akaiondoa ghadhabu yake mbali naye. Usikasirike kwa sababu ya wapotovu, wala usiwaonee wivu waovu, kwa maana mpotovu hana tumaini la siku zijazo, nayo taa ya waovu itazimwa. Mwanangu, mche BWANA na mfalme, wala usijiunge na waasi, kwa maana hao wawili watatuma maangamizi ya ghafula juu yao, naye ni nani ajuaye maafa wawezayo kuleta? Hii pia ni misemo ya wenye hekima: Kuonesha upendeleo katika hukumu si vyema: Yeyote amwambiaye mwenye hatia, “Wewe huna hatia,” makabila ya watu watamlaani, na mataifa watamkana. Bali itakuwa vyema kwa wale watakaowatia hatiani wenye hatia, nazo baraka tele zitawajilia juu yao. Jawabu la uaminifu ni kama busu la mdomoni. Maliza kazi zako za nje, nawe uweke mashamba yako tayari, baada ya hayo, jenga nyumba yako. Usishuhudie dhidi ya jirani yako bila sababu, au kutumia midomo yako kudanganya. Usiseme, “Nitamtenda kama alivyonitenda mimi; nitamlipiza mtu yule kwa kile alichonitendea.” Nilipita karibu na shamba la mvivu, karibu na shamba la mizabibu la mtu asiye na akili, miiba ilikuwa imeota kila mahali, ardhi ilikuwa imefunikwa na magugu, na ukuta wa mawe ulikuwa umebomoka. Nikatafakari moyoni mwangu lile nililoliona, nami nikajifunza somo kutokana na niliyoyaona: Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, bado kukunja mikono kidogo upate kupumzika: na umaskini utakuja juu yako kama mnyangʼanyi, na kupungukiwa kutakujia kama mtu mwenye silaha.