Methali 14:1-17
Methali 14:1-17 Biblia Habari Njema (BHN)
Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake, lakini mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Mwenye mwenendo mnyofu humcha Mwenyezi-Mungu, lakini mpotovu humdharau Mungu. Mpumbavu hujiadhibu mwenyewe kwa kuropoka kwake, lakini mwenye hekima hulindwa na maneno yake. Bila ng'ombe wa kulima ghala za mtu ni tupu, mavuno mengi hupatikana kwa nguvu ya ng'ombe wa kulima. Shahidi mwaminifu hasemi uongo, lakini asiyeaminika hububujika uongo. Mwenye dharau hutafuta hekima bure, lakini mwenye busara hupata maarifa kwa urahisi. Ondoka mahali alipo mpumbavu, maana hapo alipo hamna maneno ya hekima. Hekima ya mwenye busara humwonesha njia yake, lakini upumbavu wa wapumbavu huwadanganya wenyewe. Wapumbavu huchekelea dhambi, bali wanyofu hupata fadhili kwa Mungu. Moyo waujua uchungu wake wenyewe, wala mgeni hawezi kushiriki furaha yake. Nyumba ya mtu mwovu itabomolewa, lakini hema ya wanyofu itaimarishwa. Njia unayodhani kuwa ni sawa, mwishoni yaweza kukuongoza kwenye kifo. Huzuni yaweza kufichika katika kicheko; baada ya furaha huja majonzi. Mtu mpotovu atavuna matunda ya mwenendo wake, naye mtu mwema atapata tuzo la matendo yake. Mjinga huamini kila kitu anachoambiwa, lakini mwenye busara huwa na tahadhari. Mwenye hekima ni mwangalifu na huepa uovu, lakini mpumbavu hajizuii wala hana uangalifu. Mwenye kuwaka hasira haraka hutenda kipumbavu, lakini mwenye busara ana uvumilivu.
Methali 14:1-17 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha BWANA; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau. Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi. Zizi ni safi ambapo hapana ng'ombe; Bali nguvu za ng'ombe zaleta faida nyingi. Shahidi mwaminifu hatasema uongo; Bali shahidi wa uongo, pumzi zake ni uongo. Mwenye dharau hutafuta hekima, asiipate; Bali maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu. Toka mbele ya uso wa mpumbavu, Maana hutaona kwake midomo ya maarifa. Akili za mwenye busara ni kujua njia yake; Lakini upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu. Wapumbavu huidharau hatia; Bali upo upendeleo kwa wenye haki. Moyo huujua uchungu wa nafsi yake, Wala mgeni haishiriki furaha yake. Nyumba ya mtu mwovu itabomolewa; Bali hema la mwenye haki litafanikiwa. Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti. Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo. Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake. Mjinga huamini kila neno; Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo. Mwenye hekima huhadhari, na kujitenga na uovu; Bali mpumbavu hupuuza yote, na hajali. Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga; Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa.
Methali 14:1-17 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha BWANA; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau. Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi. Zizi ni safi ambapo hapana ng’ombe; Bali nguvu za ng’ombe zaleta faida nyingi. Shahidi mwaminifu hatasema uongo; Bali shahidi wa uongo, pumzi zake ni uongo. Mwenye dharau hutafuta hekima, asiipate; Bali maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu. Toka mbele ya uso wa mpumbavu, Maana hutaona kwake midomo ya maarifa. Akili za mwenye busara ni kujua njia yake; Lakini upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu. Wapumbavu huidharau hatia; Bali upo upendeleo kwa wenye haki. Moyo huujua uchungu wa nafsi yake, Wala mgeni haishiriki furaha yake. Nyumba ya mtu mbaya itabomolewa; Bali hema ya mwenye haki itafanikiwa. Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti. Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo. Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake. Mjinga huamini kila neno; Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo. Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu; Bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai. Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga; Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa.
Methali 14:1-17 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)
Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake, bali mpumbavu huibomoa nyumba yake kwa mikono yake mwenyewe. Yeye ambaye njia zake ni nyofu humcha BWANA, bali yeye ambaye njia zake zimepotoka humdharau Mungu. Mazungumzo ya mpumbavu huleta fimbo mgongoni mwake, bali mwenye hekima hulindwa na maneno ya midomo yake. Pale ambapo hakuna mafahali, hori ni tupu, bali kutokana na nguvu za fahali huja mavuno mengi. Shahidi mwaminifu hadanganyi, bali shahidi wa uongo humimina uongo. Mwenye mzaha huitafuta hekima na haipati, bali maarifa huja kwa urahisi kwa anayepambanua. Kaa mbali na mtu mpumbavu, kwa maana hutapata maarifa katika midomo yake. Hekima ya mwenye busara ni kufikiria njia zake, bali upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu. Wapumbavu hudhihaki kujirekebisha kutoka dhambi, bali wema hupatikana miongoni mwa wanyofu. Kila moyo hujua uchungu wake wenyewe, wala hakuna yeyote awezaye kushiriki furaha yake. Nyumba ya mwovu itaangamizwa, bali hema la mnyofu litastawi. Iko njia ionekanayo kuwa sawa kwa mtu, bali mwisho wake huelekeza mautini. Hata katika kicheko moyo unaweza kuuma, nayo furaha yaweza kuishia katika majonzi. Wasio na imani watapatilizwa kikamilifu kwa ajili ya njia zao, naye mtu mwema atapewa thawabu kwa ajili ya njia yake. Mtu mjinga huamini kila kitu, bali mwenye busara hufikiria hatua zake. Mtu mwenye hekima humcha BWANA na kuepuka mabaya, bali mpumbavu hukasirika kwa hamaki na uzembe. Mtu anayekasirika kwa haraka hufanya mambo ya upumbavu, naye mtu wa hila huchukiwa.