Yeremia 23:1-9
Yeremia 23:1-9 Biblia Habari Njema (BHN)
“Ole wao wachungaji wanaowaangamiza na kuwatawanya kondoo wa malisho yangu!” Kwa hiyo, mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli nasema hivi kuhusu wachungaji wanaowachunga watu wangu: Nyinyi mmewatawanya kondoo wangu na kuwafukuza, wala hamkuwatunza. Basi, nami pia nitawaadhibu kwa ajili ya matendo yenu maovu. Kisha, nitawakusanya kondoo wangu waliobaki kutoka nchi zote nilikowatawanya, na kuwarudisha malishoni mwao. Nao watazaa na kuongezeka. Nitawapa wachungaji watakaowatunza vema, nao hawatakuwa na woga tena wala kufadhaika, na hakuna hata mmoja wao atakayepotea, mimi Mwenyezi-Mungu nimesema. “Tazama, siku zaja nitakapomchipushia Daudi chipukizi adili. Huyo atatawala kama mfalme, na atatenda kwa busara, haki na uadilifu katika nchi. Katika siku za utawala wake, Yuda ataokolewa na Israeli ataishi kwa usalama. Naye ataitwa, ‘Mwenyezi-Mungu ni uadilifu wetu.’ “Kwa hiyo siku zaja, nasema mimi Mwenyezi-Mungu, ambapo watu hawataapa tena kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyewatoa watu wa Israeli nchini Misri’, bali wataapa kwa kusema, ‘Kama aishivyo Mwenyezi-Mungu aliyewatoa na kuwaongoza Waisraeli kutoka nchi ya kaskazini na kutoka nchi zote ambako aliwatawanya.’ Kisha wataishi katika nchi yao wenyewe.” Kuhusu hao manabii wasiofaa, mimi imevunjika moyo, mifupa yangu yote inatetemeka; nimekuwa kama mlevi, kama mtu aliyelemewa na pombe, kwa sababu yake Mwenyezi-Mungu na maneno yake matakatifu.
Yeremia 23:1-9 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Ole wao wachungaji, wanaoharibu kondoo za malisho yangu na kuwatawanya! Asema BWANA. Kwa sababu hiyo BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, juu ya wachungaji wanaowalisha watu wangu, Mmetawanya kundi langu, na kuwafukuza, wala hamkwenda kuwatazama; angalieni, nitawapatiliza uovu wa matendo yenu, asema BWANA. Nami nitakusanya mabaki ya kundi langu, katika nchi zile zote nilizowafukuza, nami nitawaleta tena mazizini mwao; nao watazaa na kuongezeka. Nami nitaweka juu yao wachungaji watakaowalisha; wala hawataona hofu tena, wala kufadhaika, wala hatapotea hata mmoja wao, asema BWANA. Tazama siku zinakuja, asema BWANA, nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi. Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, BWANA ni haki yetu. Kwa hiyo, angalia, siku zinakuja, asema BWANA, ambapo hawatasema tena, Aishivyo BWANA, aliyewatoa wana wa Israeli katika nchi ya Misri; lakini, Aishivyo BWANA, aliyewapandisha na kuwaongoza wazao wa nyumba ya Israeli kutoka nchi ya kaskazini, na kutoka nchi zote nilikowafukuza; nao watakaa katika nchi yao wenyewe. Kuhusu habari za manabii. Moyo wangu ndani yangu umevunjika, Mifupa yangu yote inatikisika. Nimekuwa kama mtu aliye mlevi, Na kama mtu aliyeshindwa na divai; kwa ajili ya BWANA, na kwa ajili ya maneno yake matakatifu.
Yeremia 23:1-9 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Ole wao wachungaji, wanaoharibu kondoo za malisho yangu na kuwatawanya! Asema BWANA. Kwa sababu hiyo BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, juu ya wachungaji wanaowalisha watu wangu, Mmetawanya kundi langu, na kuwafukuza, wala hamkwenda kuwatazama; angalieni, nitawapatiliza uovu wa matendo yenu, asema BWANA. Nami nitakusanya mabaki ya kundi langu, katika nchi zile zote nilizowafukuza, nami nitawaleta tena mazizini mwao; nao watazaa na kuongezeka. Nami nitaweka juu yao wachungaji watakaowalisha; wala hawataona hofu tena, wala kufadhaika, wala hatapotea hata mmoja wao, asema BWANA. Tazama siku zinakuja, asema BWANA, nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi. Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, BWANA ni haki yetu. Kwa hiyo, angalia, siku zinakuja, asema BWANA, ambapo hawatasema tena, Aishivyo BWANA, aliyewatoa wana wa Israeli katika nchi ya Misri; lakini, Aishivyo BWANA, aliyewapandisha na kuwaongoza wazao wa nyumba ya Israeli kutoka nchi ya kaskazini, na kutoka nchi zote nilikowafukuza; nao watakaa katika nchi yao wenyewe. Katika habari za manabii. Moyo wangu ndani yangu umevunjika, Mifupa yangu yote inatikisika. Nimekuwa kama mtu aliye mlevi, Na kama mtu aliyeshindwa na divai; kwa ajili ya BWANA, na kwa ajili ya maneno yake matakatifu.
Yeremia 23:1-9 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)
“Ole wao wachungaji wanaoharibu na kutawanya kondoo wa malisho yangu!” asema BWANA. Kwa hiyo hili ndilo BWANA, Mungu wa Israeli, analowaambia wachungaji wanaowachunga watu wangu: “Kwa sababu mmelitawanya kundi langu na kuwafukuzia mbali, wala hamkuwatunza, basi mimi nitawaadhibu kwa ajili ya uovu mliofanya,” asema BWANA. “Mimi mwenyewe nitayakusanya mabaki ya kundi langu kutoka nchi zote ambazo nimewafukuzia, nami nitawarudisha katika malisho yao, ambapo watazaa na kuongezeka idadi yao. Nitaweka wachungaji juu yao ambao watawachunga, nao hawataogopa tena au kutishwa, wala hatapotea hata mmoja,” asema BWANA. BWANA asema, “Siku zinakuja, nitakapomwinulia Daudi Tawi lenye haki, Mfalme atakayetawala kwa hekima, na kutenda lililo haki na sawa katika nchi. Katika utawala wake, Yuda ataokolewa, na Israeli ataishi salama. Hili ndilo jina atakaloitwa: BWANA ni Haki Yetu.” BWANA asema, “Hivyo basi, siku zinakuja, ambapo watu hawatasema tena, ‘Hakika kama BWANA aishivyo, aliyewapandisha Waisraeli kutoka Misri,’ bali watasema, ‘Hakika kama BWANA aishivyo, aliyewatoa wazao wa Israeli kutoka nchi ya kaskazini na nchi zote alizokuwa amewafukuzia.’ Ndipo wataishi katika nchi yao wenyewe.” Kuhusu manabii: Moyo wangu umevunjika ndani yangu; mifupa yangu yote inatetemeka. Nimekuwa kama mtu aliyelewa, kama mtu aliyelemewa na divai, kwa sababu ya BWANA na maneno yake matakatifu.