Yakobo 1:1-7
Yakobo 1:1-8 Biblia Habari Njema (BHN)
Mimi Yakobo, mtumishi wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo, nawaandikia nyinyi, makabila kumi na mawili, yaliyotawanyika ulimwenguni! Salamu! Ndugu zangu, muwe na furaha mnapopatwa na majaribu mbalimbali, kwani mwajua kwamba imani yenu ikisha stahimili, itawapatieni uvumilivu. Muwe na hakika kwamba uvumilivu wenu utawategemeza mpaka mwisho, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu, bila kupungukiwa chochote. Lakini kama mmoja wenu ametindikiwa hekima, basi, anapaswa kumwomba Mungu ambaye atampatia; kwani Mungu huwapa wote kwa wingi na kwa ukarimu. Lakini anapaswa kuomba kwa imani bila mashaka yoyote. Mtu aliye na mashaka ni kama mawimbi ya bahari ambayo husukumwa na kutupwatupwa na upepo. Kwa hiyo mtu aliye na mashaka, mwenye nia mbili na asiye na msimamo katika mwenendo wake wote, asidhani ya kwamba atapata chochote kile kutoka kwa Bwana.
Yakobo 1:1-7 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Yakobo, mtumwa wa Mungu, na wa Bwana Yesu Kristo, kwa makabila kumi na mawili waliotawanyika; salamu. Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno. Lakini mmoja wenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. Ila na aombe kwa imani, pasipo mashaka yoyote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari linalochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana.
Yakobo 1:1-7 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Yakobo, mtumwa wa Mungu, na wa Bwana Yesu Kristo, kwa kabila kumi na mbili waliotawanyika; salamu. Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno. Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana.
Yakobo 1:1-7 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)
Yakobo, mtumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo. Kwa makabila kumi na mawili yaliyotawanyika ulimwenguni. Salamu. Ndugu zangu, hesabuni kuwa ni furaha tupu mnapopatwa na majaribu mbalimbali, kwa sababu mnajua ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. Acheni saburi ikamilishe kazi yake, ili mpate kuwa wakamilifu na watimilifu, bila kupungukiwa chochote. Kama mtu yeyote miongoni mwenu amepungukiwa na hekima, basi amwombe Mungu, yeye awapaye watu wote kwa ukarimu wala hana kinyongo, naye atapewa. Lakini anapoomba, lazima aamini wala asiwe na shaka, kwa sababu mtu aliye na shaka ni kama wimbi la bahari, linalopeperushwa na upepo na kutupwa huku na huko. Mtu kama huyo asidhani ya kuwa atapata kitu chochote kutoka kwa Bwana.