Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Ezekieli 12:1-28

Ezekieli 12:1-28 Biblia Habari Njema (BHN)

Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia: “Wewe mtu! Wewe unakaa kati ya watu waasi. Wana macho lakini hawaoni; wana masikio lakini hawasikii. Wao ni watu waasi. Basi, ewe mtu, fanya kama vile unakwenda uhamishoni: Ondoka wakiwa wanakuona, ukimbilie mahali pengine. Nenda kama mkimbizi kutoka mahali ulipo mpaka mahali pengine wao wakikuona. Labda wataelewa, ingawa wao ni waasi. Hakikisha wanaona unachofanya. Funga mzigo wako uutoe nje na kuwa tayari kuondoka jioni kama wafanyavyo watu wanaokwenda uhamishoni. Wakiwa wanakuangalia toboa ukuta wa nyumba, upitie hapo na kwenda nje. Wakiwa wanakuona, jitwike mabegani mzigo wako na kuondoka wakati wa giza. Funika uso wako usiweze kuona unakwenda wapi. Ndivyo ninavyokufanya uwe ishara kwa Waisraeli.” Basi, nikafanya kama nilivyoamriwa. Siku hiyo, wakati wa mchana, nikafunga mzigo wangu kama mzigo wa mtu anayekimbia. Jioni nikautoboa ukuta na giza lilipokuwa likiingia, nikatoka, nimejitwika mzigo wangu mabegani, watu wote wakiniona. Kesho yake asubuhi, Mwenyezi-Mungu akaniuliza: “Wewe mtu! Je, hao waasi wa Israeli hawajakuuliza maana ya hicho ulichofanya? Waambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema: Kauli hii yangu yahusu mambo yatakayompata mtawala wa Yerusalemu na watu wote wa Israeli wanaoishi humo. Waambie kuwa wewe ni ishara kwao; kama ulivyofanya ndivyo itakavyotendeka kwao: Watakwenda uhamishoni; naam, watachukuliwa mateka. Naye mtawala wao atajitwika mzigo wake mabegani wakati wa usiku, atatoka kupitia ukuta atakaotoboa apate kutoka; atafunika uso wake ili asiione nchi kwa macho yake. Lakini nitatandaza wavu wangu juu yake, naye atanaswa katika mtego wangu. Nitampeleka Babuloni, nchi ya Wakaldayo; naye akiwa huko atakufa bila kuiona hiyo nchi. Wafuasi wake wote, washauri wake na vikosi vyake vyote, nitawatawanya nje kila upande. Nitauchomoa upanga na kuwafuatilia nyuma. Nitakapowatawanya kati ya mataifa mengine na nchi za mbali, ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu. Lakini nitawaacha wachache waokoke vitani, wanusurike njaa na maradhi mabaya; ili hao waweze kuwasimulia watu wa mataifa wanamoishi jinsi walivyotenda mabaya. Ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.” Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia: “Wewe mtu, kula chakula na kunywa maji yako ukitetemeka kwa hofu. Waambie watu wa nchi hii, kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema juu ya wakazi wa Yerusalemu ambao bado wamo nchini Israeli, kwamba watakula chakula chao kwa hofu na watakunywa maji yao kwa kufadhaika, kwani nchi yao haitakuwa na kitu, kwa sababu kila mkazi ni mdhalimu. Miji yenye watu itateketezwa, na nchi itakuwa ukiwa. Nanyi mtatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.” Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia: “Wewe mtu: Kwa nini methali hii inatajwa katika Israeli: ‘Siku zaja na kupita, lakini maono ya nabii hayatimii?’ Waambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema kwamba nitakomesha methali hiyo nao hawataitumia tena nchini Israeli. Waambie kuwa wakati umewadia ambapo maono yote yatatimia. Maana hapatakuwa tena na maono ya uongo au kupiga bao miongoni mwa Waisraeli. Mimi Mwenyezi-Mungu mwenyewe nitatangaza yatakayotukia. Nayo yatatukia bila kukawia. Wakati wa uhai wenu, enyi watu waasi, neno nitakalotamka nitalitimiza. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.” Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: “Wewe mtu, Waisraeli wanafikiri kwamba maono yako yanahusu siku za baadaye sana, na unabii wako wahusu nyakati za mbali sana! Kwa hiyo waambie, kwamba mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema kuwa maneno yangu yote yatatimia karibuni. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema!”

Ezekieli 12:1-28 Swahili Revised Union Version (SRUV)

Neno la BWANA likanijia tena, kusema, Mwanadamu, wewe unakaa kati ya nyumba iliyoasi, watu ambao wana macho ya kuona, ila hawaoni, wana masikio ya kusikia, ila hawasikii; kwa maana ni nyumba iliyoasi. Basi, mwanadamu, funga tayari vyombo kwa uhamisho, ukahame wakati wa mchana mbele ya macho yao; nawe utahama toka mahali pako hapa mpaka mahali pengine mbele ya macho yao; labda watafahamu, wajapokuwa ni nyumba iliyoasi. Nawe utatoa vyombo vyako, wakati wa mchana, mbele ya macho yao, kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa; nawe mwenyewe utatoka, wakati wa jioni, mbele ya macho yao, kama watu watokavyo katika kuhamishwa. Toboa mahali ukutani mbele ya macho yao, ukachukue vitu kwa kuvipitisha pale. Mbele ya macho yao utajitwika begani pako, na kuvichukua nje gizani; utafunika uso wako, hata usiione nchi; kwa maana nimekuweka uwe ishara kwa nyumba ya Israeli. Nikafanya vile vile kama nilivyoamriwa; nilitoa vyombo vyangu wakati wa mchana kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa, na wakati wa jioni nikautoboa ukuta kwa mkono wangu; nikavitoa gizani, nikavichukua begani, mbele ya macho yao. Asubuhi neno la BWANA likanijia, kusema, Mwanadamu, nyumba ya Israeli, je! Nyumba ile iliyoasi, hawakukuambia, Unafanya nini wewe? Waambie, Bwana MUNGU asema hivi; Ufunuo huu wamhusu mkuu wa Yerusalemu, na nyumba yote ya Israeli walio kati yao. Sema, Mimi ni ishara kwenu; kama mimi nilivyotenda, wao nao watatendwa vile vile; watahamishwa, watakwenda kufungwa. Naye mkuu aliye kati yao atachukua begani katika giza; naye atatoka kwenda zake; watatoboa mahali ukutani, wapate kuvichukua vyombo vyao nje; atafunika uso wake, kwa sababu hataiona nchi kwa macho yake. Tena wavu wangu nitautandika juu yake, naye atanaswa kwa mtego wangu; nami nitampeleka Babeli, mpaka nchi ya Wakaldayo; lakini hataiona, ingawa atakufa huko. Nami nitawatawanya kwa pepo zote wote wamzungukao ili wamsaidie, na vikosi vyake vyote; nami nitaufuta upanga nyuma yao. Nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA; nitakapowatawanya kati ya mataifa, na kuwatapanya katika nchi zote. Lakini nitawasaza watu wachache miongoni mwao na kuwaokoa na upanga, na njaa, na tauni ili watangaze habari ya machukizo yao yote, kati ya mataifa huko waendako; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA. Tena neno la BWANA likanijia, kusema, Mwanadamu, ule chakula chako kwa mtetemo, ukanywe maji yako kwa kutetemeka na kwa kuyatunza sana; ukawaambie watu wa nchi, Bwana MUNGU asema hivi, kuhusu habari zao wakaao Yerusalemu, na katika nchi ya Israeli; Watakula chakula chao kwa kukitunza sana, na maji yao watayanywa kwa ushangao, nchi yao iwe ukiwa, kwa kukosa vitu vyote viijazavyo, kwa sababu ya udhalimu wao wote wakaao ndani yake. Na miji yote yenye watu itakuwa maganjo, nayo nchi itakuwa ukiwa; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi BWANA. Neno la BWANA likanijia, kusema, Mwanadamu, ni mithali gani hii mliyo nayo katika nchi ya Israeli, mkisema, Siku hizo zinakawia na maono yote hayatimizwi. Basi uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Nitaikomesha mithali hii, wasiitumie tena kama mithali katika Israeli; lakini uwaambie, Siku hizo ni karibu, na utimilizo wa maono yote. Kwa maana hayatakuwapo tena maono yoyote ya ubatili, wala ubashiri wa kujipendekeza, katika nyumba ya Israeli. Maana mimi ni BWANA; mimi nitanena, na neno lile nitakalolinena litatimizwa; wala halitakawilishwa tena; maana katika siku zenu, Ewe nyumba iliyoasi, nitalinena neno hilo na kulitimiza, asema Bwana MUNGU. Neno la BWANA likanijia tena, kusema, Mwanadamu, tazama, hao wa nyumba ya Israeli husema, Maono hayo ayaonayo ni ya siku nyingi zijazo, naye anatabiri habari ya nyakati zilizo mbali sana. Basi uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Maneno yangu hayatakawilishwa tena hata moja, bali neno nitakalolinena litatimizwa, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 12:1-28 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)

Neno la BWANA likanijia tena, kusema, Mwanadamu, wewe unakaa kati ya nyumba iliyoasi, watu ambao wana macho ya kuona, ila hawaoni, wana masikio ya kusikia, ila hawasikii; kwa maana ni nyumba iliyoasi. Basi, mwanadamu, funga tayari vyombo kwa uhamisho, ukahame wakati wa mchana mbele ya macho yao; nawe utahama toka mahali pako hapa mpaka mahali pengine mbele ya macho yao; labda watafahamu, wajapokuwa ni nyumba iliyoasi. Nawe utatoa vyombo vyako, wakati wa mchana, mbele ya macho yao, kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa; nawe mwenyewe utatoka, wakati wa jioni, mbele ya macho yao, kama watu watokavyo katika kuhamishwa. Toboa mahali ukutani mbele ya macho yao, ukachukue vitu kwa kuvipitisha pale. Mbele ya macho yao utajitwika begani pako, na kuvichukua nje gizani; utafunika uso wako, hata usiione nchi; kwa maana nimekuweka uwe ishara kwa nyumba ya Israeli. Nikafanya vile vile kama nilivyoamriwa; nalitoa vyombo vyangu wakati wa mchana kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa, na wakati wa jioni nikautoboa ukuta kwa mkono wangu; nikavitoa gizani, nikavichukua begani, mbele ya macho yao. Asubuhi neno la BWANA likanijia, kusema, Mwanadamu, nyumba ya Israeli, je! Nyumba ile iliyoasi, hawakukuambia, Unafanya nini wewe? Waambie, Bwana MUNGU asema hivi; Ufunuo huu wamhusu mkuu wa Yerusalemu, na nyumba yote ya Israeli walio kati yao. Sema, Mimi ni ishara kwenu; kama mimi nilivyotenda, wao nao watatendwa vile vile; watahamishwa, watakwenda kufungwa. Naye mkuu aliye kati yao atachukua begani katika giza; naye atatoka kwenda zake; watatoboa mahali ukutani, wapate kuvichukua vyombo vyao nje; atafunika uso wake, kwa sababu hataiona nchi kwa macho yake. Tena wavu wangu nitautandika juu yake, naye atanaswa kwa mtego wangu; nami nitampeleka Babeli, mpaka nchi ya Wakaldayo; lakini hataiona, angawa atakufa huko. Nami nitawatawanya kwa pepo zote wote wamzungukao ili wamsaidie, na vikosi vyake vyote; nami nitaufuta upanga nyuma yao. Nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA; nitakapowatawanya kati ya mataifa, na kuwatupa-tupa katika nchi zote. Lakini nitawasaza watu wachache miongoni mwao na kuwaokoa na upanga, na njaa, na tauni ili watangaze habari ya machukizo yao yote, kati ya mataifa huko waendako; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA. Tena neno la BWANA likanijia, kusema, Mwanadamu, ule chakula chako kwa matetemo, ukanywe maji yako kwa kutetemeka na kwa kuyatunza sana; ukawaambie watu wa nchi, Bwana MUNGU asema hivi, katika habari zao wakaao Yerusalemu, na katika nchi ya Israeli; Watakula chakula chao kwa kukitunza sana, na maji yao watayanywa kwa ushangao, nchi yao iwe ukiwa, kwa kukosa vitu vyote viijazavyo, kwa sababu ya udhalimu wao wote wakaao ndani yake. Na miji yote yenye watu itakuwa maganjo, nayo nchi itakuwa ukiwa; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi BWANA. Neno la BWANA likanijia, kusema, Mwanadamu, ni mithali gani hii mliyo nayo katika nchi ya Israeli, mkisema, Siku hizo zinakawia na maono yote hayatimizwi. Basi uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Nitaikomesha mithali hii, wasiitumie tena kama mithali katika Israeli; lakini uwaambie, Siku hizo ni karibu, na utimilizo wa maono yote. Kwa maana hayatakuwapo tena maono yo yote ya ubatili, wala ubashiri wa kujipendekeza, katika nyumba ya Israeli. Maana mimi ni BWANA; mimi nitanena, na neno lile nitakalolinena litatimizwa; wala halitakawilishwa tena; maana katika siku zenu, Ewe nyumba iliyoasi, nitalinena neno hilo na kulitimiza, asema Bwana MUNGU. Neno la BWANA likanijia tena, kusema, Mwanadamu, tazama, hao wa nyumba ya Israeli husema, Maono hayo ayaonayo ni ya siku nyingi zijazo, naye anatabiri habari ya nyakati zilizo mbali sana. Basi uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Maneno yangu hayatakawilishwa tena hata moja, bali neno nitakalolinena litatimizwa, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 12:1-28 Neno: Bibilia Takatifu 2025 (NENO)

Neno la BWANA likanijia kusema: “Mwanadamu, unaishi miongoni mwa watu waasi. Wana macho ya kuona, lakini hawaoni, na masikio ya kusikia lakini hawasikii, kwa kuwa ni watu waasi. “Kwa hiyo, mwanadamu, funga mizigo yako kwa kwenda uhamishoni tena wakati wa mchana, wakiwa wanakutazama, toka nje na uende mahali pengine kutoka hapo ulipo. Huenda wataelewa, ingawa wao ni nyumba ya uasi. Wakati wa mchana, wakiwa wanakutazama, toa nje mizigo yako iliyofungwa kwa ajili ya kwenda uhamishoni. Kisha wakati wa jioni, wakiwa wanakutazama toka nje kama wale wanaoenda uhamishoni. Wakiwa wanakutazama, toboa ukuta utolee mizigo yako hapo. Beba mizigo hiyo begani mwako wakikuangalia uichukue nje wakati wa giza la jioni. Funika uso wako ili usione nchi, kwa maana nimekufanya ishara kwa nyumba ya Israeli.” Basi nikafanya kama nilivyoamriwa. Wakati wa mchana nilitoa vitu vyangu nje vilivyofungwa tayari kwa uhamishoni. Kisha wakati wa jioni nikatoboa ukuta kwa mikono yangu. Nikachukua mizigo yangu nje wakati wa giza la jioni, nikiwa nimeibeba mabegani mwangu huku wakinitazama. Asubuhi neno la BWANA likanijia kusema: “Mwanadamu, je, nyumba ile ya uasi ya Israeli haikukuuliza, ‘Unafanya nini?’ “Waambie, ‘Hili ndilo asemalo BWANA Mwenyezi: Unabii huu unamhusu mkuu aliye katika Yerusalemu na watu wote wa nyumba ya Israeli walio huko.’ Waambie, ‘Mimi ni ishara kwenu.’ “Kama vile nilivyotenda, basi litatendeka vivyo hivyo kwao. Wataenda uhamishoni kama mateka. “Mkuu aliye miongoni mwao atabeba mizigo yake begani wakati wa giza la jioni na kuondoka, na tundu litatobolewa ukutani ili apite. Atafunika uso wake ili asiweze kuiona nchi. Nitamtandazia wavu wangu, naye atanaswa kwenye mtego wangu; nitamleta hadi Babeli, nchi ya Wakaldayo, lakini hataiona, naye atafia huko. Wote wanaomzunguka nitawatawanya pande zote: watumishi wake na majeshi yake yote; nami nitawafuatilia kwa upanga. “Wao watajua kwamba Mimi ndimi BWANA, nitakapowatawanya miongoni mwa mataifa, na kuwatapanya katika nchi zote. Lakini nitawaokoa wachache wao, wasiuawe kwa upanga, njaa na tauni, ili katika mataifa watakakoenda waweze kukiri matendo yao yote ya kuchukiza. Ndipo watajua kuwa Mimi ndimi BWANA.” Neno la BWANA likanijia kusema: “Mwanadamu, tetemeka unapokula chakula chako, tetemeka kwa hofu unapokunywa maji yako. Waambie watu wa nchi: ‘Hili ndilo asemalo BWANA Mwenyezi kuhusu wakaaji wa Yerusalemu na katika nchi ya Israeli: Watakula chakula chao kwa wasiwasi na kunywa maji yao kwa kufadhaika, kwa kuwa nchi yao itanyangʼanywa kila kitu chake kwa sababu ya udhalimu wa wote wanaoishi humo. Miji inayokaliwa na watu itaharibiwa na nchi itakuwa ukiwa. Ndipo mtajua kuwa Mimi ndimi BWANA.’ ” Neno la BWANA likanijia kusema: “Mwanadamu, ni ipi hii mithali mlio nayo katika nchi ya Israeli: ‘Siku zinapita na hakuna maono yoyote yanayotimia’? Waambie, ‘Hili ndilo asemalo BWANA Mwenyezi: Nitaikomesha mithali hii, nao hawataitumia tena katika Israeli.’ Waambie, ‘Siku zimekaribia ambapo kila ono litatimizwa. Kwa maana hapatakuwa tena na maono ya uongo wala ubashiri wa kujipendekeza miongoni mwa watu wa Israeli. Lakini Mimi BWANA nitasema neno nitakalo, nalo litatimizwa bila kuchelewa. Kwa kuwa katika siku zako, ewe nyumba ya uasi, nitatimiza kila nisemalo, asema BWANA Mwenyezi.’ ” Neno la BWANA likanijia kusema: “Mwanadamu, nyumba ya Israeli inasema, ‘Maono yale anayoyaona ni kwa ajili ya miaka mingi ijayo, naye hutabiri kuhusu siku zijazo zilizo mbali.’ “Kwa hiyo, waambie, ‘Hili ndilo asemalo BWANA Mwenyezi: Hakuna maneno yangu yatakayocheleweshwa tena zaidi, lolote nisemalo litatimizwa, asema BWANA Mwenyezi.’ ”