Mika Utangulizi
Utangulizi
Jina “Mika” maana yake ni “Ni nani aliye kama Bwana”. Mika alikuwa mkaazi wa mji wa Moresheth-Gathi kusini mwa Yuda, na aliishi wakati mmoja na Isaya na Hosea. Aliona Waashuru wakiendelea kustawi wakati Israeli ilikuwa ikididimia hadi ikawa jimbo la Ashuru baada ya kuanguka kwa Israeli mnamo 722 K.K. Yuda mara kwa mara ilipata vitisho kutoka kwa wafalme wa Ashuru waliofanikiwa. Mika alionya kuhusu hukumu ya Mungu dhidi ya falme zote mbili za Yuda na Israeli.
Hali kadhalika, alitabiri kuangamizwa kwa falme hizo kwa sababu ya uovu wa watawala, manabii wa uongo, makuhani waovu, wafanyabiashara wasio waaminifu, na mahakimu waliouza haki kwa rushwa. Kimsingi, Mika alitangaza hukumu kwa Yuda na Israeli kwa watawala, viongozi wa dini, wasimamizi wa haki, na matajiri hawakuwa na uchaji wala hofu ya Mungu katika kutimiza wajibu wao. Mbali na kutangaza hukumu dhidi ya waovu, pia Mika alitoa ujumbe wa matumaini. Alitangaza ahadi ya kufanywa upya kwa Sayuni na utawala wa amani kwa waliomwamini na kumtumaini Mungu. Alihubiri kwamba Sayuni mpya itakuwa kitovu cha utawala wa ulimwengu wote, mahali ambapo haki na amani halisi vitatamalaki. Sayuni mpya ilihusishwa kuwepo na “Mtawala katika Israeli” yaani Masiya, ambaye angezaliwa Bethlehemu na kuanzisha utawala wake ambao utadumu milele.
Mwandishi
Mika.
Kusudi
Kuwaonya mataifa ya Yuda na Israeli juu ya hukumu ya Mungu na kutangaza wokovu kwa wote watakaotubu na kuamini katika Masiya atakayezaliwa Bethlehemu.
Mahali
Samaria na Yerusalemu.
Tarehe
Mnamo 742–687 K.K.
Wahusika Wakuu
Watu wa Samaria na Yerusalemu.
Wazo Kuu
Hukumu na wokovu wa Masiya.
Mambo Muhimu
Huu ni mfano mzuri wa ushairi wa Kiebrania. Ziko sehemu tatu, kila moja ikianza na “Sikia” au “Sikiliza” (1:2; 3:1; 6:1) na kufunga na ahadi.
Yaliyomo
Hukumu dhidi ya Samaria na Yerusalemu (1:1‑16)
Mipango ya mwanadamu na mipango ya Mungu (2:1–3:12)
Urejesho wa Mungu (4:1–5:15)
Hukumu na huruma (6:1–7:20).
Iliyochaguliwa sasa
Mika Utangulizi: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Biblia Takatifu™ Neno™
Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Version™
Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.