Kutoka 32
32
Sanamu ya mwana-ngombe wa zahabu
(Kumb 9.6-29)
1Watu walipoona kwamba Musa amechelewa kurudi kutoka juu ya mulima, wakakusanyika mbele ya Haruni na kumwambia: Basi! Ututengenezee miungu itakayotuongoza, maana hatujui jambo lililomupata yule Musa aliyetutoa katika inchi ya Misri. #Ang. Mdo 7.40,41
2Haruni akawajibu: Mutwae pete za zahabu za masikio ya wake zenu, wana wenu na wabinti zenu, muniletee. 3Basi, watu wote wakatoa pete zote za zahabu za masikio yao, wakamuletea Haruni. 4Naye akazitwaa akaziyeyusha, akatengeneza sanamu ya mwana-ngombe.
Watu wakapaaza sauti wakasema: Ee Israeli, huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa katika inchi ya Misri. #Ang. 1 Fal 12.28; Mdo 7.41
5Kisha Haruni akamujengea yule mwana-ngombe mazabahu, halafu akatangaza: Kesho kutakuwa sikukuu kwa ajili ya Yawe. 6Kesho yake watu wakaamuka mapema wakatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Watu wakaikaa chini kwa kula na kunywa, kisha wakasimama na kucheza. #Ang. 1 Kor 10.7
7Yawe akamwambia Musa: Teremuka chini kwa maana watu wako uliowaleta kutoka inchi ya Misri wamejipotosha wenyewe. 8Wameacha mara moja njia niliyowaamuru, wakajifanyia sanamu ya mwana-ngombe, nao wamemwabudu na kumutolea sadaka wakisema: Ee Israeli, huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa katika inchi ya Misri! 9Ninawafahamu watu hawa. Wao wana vichwa vigumu. 10Sasa, usijaribu kunizuia. Uniache niwaangamize kwa kasirani kali. Kisha kutokana nawe nitaunda taifa kubwa.
11Lakini Musa akamusihi Yawe, Mungu wake, akisema: Ee Yawe, kwa nini hasira yako inawaka vikali juu ya watu wako uliowatoa katika inchi ya Misri kwa uwezo mukubwa na mukono wenye nguvu? #Ang. Hes l4.13-19 12Ukifanya hivyo, hakika Wamisri watasema: Aliwatoa kwa nia mbaya kwa kuwaua kwenye mulima na kuwateketeza kabisa katika dunia. Ee Yawe, tuliza hasira yako kali na kuacha jambo hilo baya ulilokusudia kufanya juu ya watu wako. 13Uwakumbuke watumishi wako, Abrahamu, Isaka na Israeli, ambao uliwaapia kwa nafsi yako mwenyewe, ukisema: Nitawazidisha wazao wenu kama nyota za mbinguni na inchi yote hii niliyowaahidia nitawapa vizazi vyenu wairizi milele. #Ang. Mwa 22.16-17; 17.8 14Basi, Yawe akaacha kuwafanyia watu wake lile jambo baya alilokuwa amesema.
15Kisha Musa akashuka kutoka juu ya mulima akiwa na vile vibao viwili vya agano katika mikono yake, vimeandikwa amri za Mungu pande zote. 16Vibao hivyo vilikuwa kazi ya Mungu mwenyewe na maandiko hayo Mungu mwenyewe aliyachora.
17Yoshua aliposikia kelele za watu, akamwambia Musa: Kuna kelele za vita ndani ya kambi.
18Lakini Musa akamujibu: Si kelele ya ushindi au kushindwa, lakini kelele ninayosikia ni kelele ya watu wanaoimba.
19Mara tu walipokaribia kambi walimwona yule mwana-ngombe na watu wakicheza. Hapo hasira ya Musa ikawaka kama moto, akatupa chini vile vibao kutoka mikono yake na kuvivunja pale chini ya mulima. 20Basi, akamutwaa yule mwana-ngombe akamuchoma kwa moto, akamusaga mpaka akakuwa unga, akakoroga unga huo katika maji na kuwalazimisha Waisraeli wakunywe.
21Musa akamwuliza Haruni: Walikufanya nini watu hawa hata ukawaingiza katika zambi kubwa hivyo?
22Haruni akamujibu: Ninakuomba, ee bwana wangu, hasira yako isiniwakie mimi mutumishi wako. Unafahamu jinsi watu hawa wanavyokuwa tayari kutenda maovu. 23Walikuja wakaniambia: Utufanyie miungu ambayo itatuongoza, maana yule Musa aliyetutoa katika inchi ya Misri hatujui jambo lililomupata. 24Nami nikawaambia, kila mumoja aliyekuwa na pete za zahabu azilete. Basi, wakaniletea, nami nikaziyeyusha juu ya moto na huyu mwana-ngombe akatokea.
25Basi, Musa alipoona kwamba watu wameasi na kufanya wanavyopenda (kwa kuwa Haruni aliwafanya waasi na kufanya wanavyopenda na kujiletea haya mbele ya waadui zao), 26Musa akasimama mbele ya mulango wa kambi na kuuliza: Ni nani anayekuwa upande wa Yawe? Akuje kwangu. Wana wote wa Lawi wakakusanyika pamoja mbele yake. 27Akawaambia: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kila mutu ajifungie upanga wake kwenye kiuno, azunguke kila pahali katika kambi, kutoka mulango moja mpaka mwingine, na kila mumoja amwue ndugu yake, rafiki yake na jirani yake. 28Wana wa Lawi wakafanya kama vile Musa alivyowaagiza. Siku hiyo watu yapata elfu tatu waliuawa. 29Musa akasema: Leo mumejitakasa ninyi wenyewe kwa kumutumikia Yawe, kwa vile hamukusita hata kuwaua watoto wenu au wandugu zenu. Mungu awajalie baraka leo hii.
Musa anawaombea Waisraeli
30Kesho yake Musa akawaambia watu: Mumetenda zambi kubwa! Sasa nitamwendea Yawe juu kwenye mulima; labda nitafanya upatanisho kwa ajili ya zambi yenu. 31Hivyo Musa akarudi kwa Yawe, akamwambia: Ninasikitika! Watu hawa wametenda zambi kubwa. Wamejifanyia wenyewe miungu ya zahabu. 32Lakini sasa, ninakuomba uwasamehe zambi yao. Ikiwa hautawasamehe, ninakusihi unifute mimi katika kitabu chako ambamo uliwaandika watu wako. #Ang. Zab 69.28; Ufu 3.5
33Lakini Yawe akamwambia Musa: Nitamufuta katika kitabu changu mutu yeyote aliyenitendea zambi. 34Lakini sasa kwenda uwaongoze watu mpaka pahali nilipokuambia. Malaika wangu atakutangulia. Hata hivyo, siku nitakapowafikia, nitawaazibu kwa sababu ya zambi yao.
35Yawe akawaletea watu ugonjwa mukali, kwa kuwa walimwomba Haruni awafanyie yule mwana-ngombe wa zahabu.
Valið núna:
Kutoka 32: SWC02
Áherslumerki
Deildu
Afrita
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.