YouVersion Logo
Search Icon

Methali 16

16
1Binadamu hupanga mipango yake,
lakini kauli ya mwisho ni yake Mwenyezi-Mungu.
2Matendo ya mtu huonekana kwake kuwa sawa,
lakini Mwenyezi-Mungu hupima nia ya mtu.
3Mwekee Mwenyezi-Mungu kazi yako,
nayo mipango yako itafanikiwa.
4Mwenyezi-Mungu ameumba kila kitu kwa kusudi lake;
hata waovu kwa ajili ya siku ya maangamizi.
5Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu;
hakika mtu wa namna hiyo hataacha kuadhibiwa.
6Kwa utii na uaminifu mtu huondolewa dhambi,
kwa kumcha Mwenyezi-Mungu huepuka uovu.
7Mwenyezi-Mungu akipendezwa na mwenendo wa mtu,
huwageuza hata adui zake kuwa marafiki.
8Afadhali mali kidogo kwa uadilifu,
kuliko mapato mengi kwa udhalimu.
9Mtu aweza kufanya mipango yake,
lakini Mwenyezi-Mungu huongoza hatua zake.
10Mfalme huamua kwa maongozi ya Mungu;
anapotoa hukumu hakosei.
11Mwenyezi-Mungu hutaka kipimo na mizani halali;
mawe yote mfukoni ya kupimia ni kazi yake.
12Ni chukizo kubwa wafalme kutenda uovu,
maana msingi wa mamlaka yao ni haki.
13Mfalme hupendelea mtu asemaye kwa unyofu;
humpenda mtu asemaye ukweli.
14Hasira ya mfalme ni kama mjumbe wa kifo;
mtu mwenye busara ataituliza.
15Uso wa mfalme ukingaa kuna uhai;
wema wake ni kama wingu la masika.
16Kupata hekima ni bora kuliko dhahabu;
kupata akili ni chaguo bora kuliko fedha.
17Njia ya wanyofu huepukana na uovu;
anayechunga njia yake huhifadhi maisha yake.
18Kiburi hutangulia maangamizi;
majivuno hutangulia maanguko.
19Afadhali kuwa mnyenyekevu na kuwa maskini,
kuliko kugawana nyara na wenye kiburi.
20Anayezingatia mafundisho atafanikiwa;
heri mtu yule anayemtumainia Mwenyezi-Mungu.
21Mwenye hekima moyoni huitwa mwenye akili;
neno la kupendeza huwavutia watu.
22Hekima ni chemchemi ya uhai kwake aliye nayo,
bali upumbavu ni adhabu ya wapumbavu.
23Moyo wa mwenye hekima humwezesha kusema kwa busara;
huyafanya maneno yake yawe ya kuvutia.
24Maneno mazuri ni kama asali;
ni matamu rohoni na yenye kuupa mwili afya.
25 # Taz Meth 14:12 Mtu aweza kuona njia yake kuwa sawa,
lakini mwishowe humwongoza kwenye kifo.
26Hamu ya chakula humhimiza mfanyakazi,
maana njaa yake humsukuma aendelee.
27Mtu mwovu hupanga uovu;
maneno yake ni kama moto mkali.
28Mtu mpotovu hueneza ugomvi,
mfitini hutenganisha marafiki.
29Mtu mkatili humshawishi jirani yake;
humwongoza katika njia mbaya.
30Anayekonyeza jicho kwa hila amepanga maovu;
anayekaza midomo amekwisha nuia mabaya.
31Kuwa na mvi za uzee ni taji la utukufu;
hupatikana kwa maisha ya uadilifu.
32Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwenye nguvu;
aitawalaye nafsi yake ni bora kuliko autekaye mji.
33Kura hupigwa kujua yatakayotukia,
lakini uamuzi ni wake Mwenyezi-Mungu.

Currently Selected:

Methali 16: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy