YouVersion Logo
Search Icon

Obadia 1

1
1 # Taz Isa 34:5-17; Yer 49:7-22; Eze 25:12-14; 35:1-15; Amo 1:11-12; Mal 1:2-5 Maono ya Obadia. Mambo aliyosema Bwana Mwenyezi-Mungu kuhusu taifa la Edomu.
Mwenyezi-Mungu ataadhibu Edomu
Tumepata habari kutoka kwa Mwenyezi-Mungu;
mjumbe ametumwa kati ya mataifa:
“Inukeni! Twende tukapigane na Edomu!”
2Mwenyezi-Mungu aliambia taifa la Edomu:
“Nitakufanya mdogo miongoni mwa mataifa,
utadharauliwa kabisa na wote.
3Kiburi chako kimekudanganya:
Kwa kuwa mji wako mkuu ni ngome ya miamba imara
na makao yako yapo juu milimani,
hivyo wajisemea,
‘Nani awezaye kunishusha chini?’
4Hata ukiruka juu kama tai,
ukafanya makao yako kati ya nyota,
mimi nitakushusha chini tu.
Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.
5“Kama wezi au wanyang'anyi wangekujia usiku,
je, wasingechukua tu kiasi cha kuwatosha?
Ikiwa wavunaji zabibu wangekujia,
je, wasingekuachia kiasi kidogo tu?
Lakini wewe, adui zako wamekuangamiza kabisa.
6Enyi wazawa wa Esau, mali zenu zimetekwa;
hazina zenu zote zimeporwa!
7Washirika wenzenu wamewadanganya,
wamewafukuza nchini mwenu.
Mliopatana nao wamewashinda vitani,
rafiki wa kutegemewa ndio waliokutegea mitego,
nawe hukuelewa yaliyokuwa yanatendeka.
8Mimi Mwenyezi-Mungu nakuuliza hivi:
Je, siku hiyo, sitawaangamiza wenye hekima kutoka Edomu
na wenye maarifa kutoka mlima Esau?
9Ewe Temani, mashujaa wako watatishika
na kila mtu atauawa mlimani Esau.
Sababu za Edomu kuadhibiwa
10“Kwa sababu ya matendo maovu
mliyowatendea ndugu zenu wazawa wa Yakobo,
mtaaibishwa na kuangamizwa milele.
11Siku ile mlisimama kando mkitazama tu,
wakati wageni walipopora utajiri wao,
naam, wageni walipoingia malango yao
na kugawana utajiri wa Yerusalemu kwa kura.
Kwa hiyo nanyi mlitenda kama wazawa wao.
12Msingalifurahia siku hiyo ndugu zenu walipokumbwa na mikasa;
msingaliwacheka Wayuda
na kuona fahari wakati walipoangamizwa;
msingalijigamba wenzenu walipokuwa wanataabika.
13Msingeliingia katika mji wa watu wangu,
siku walipokumbwa na maafa;
msingelipora mali zao, siku hiyo ya maafa yao.
14Msingelisimama kwenye njia panda
na kuwakamata wakimbizi wao;
wala msingeliwakabidhi kwa adui zao
wale waliobaki hai.
Mungu atayahukumu mataifa
15“Siku inakaribia ambapo mimi Mwenyezi-Mungu
nitayahukumu mataifa yote.
Kama mlivyowatendea wengine, ndivyo mtakavyotendewa,
mtalipwa kulingana na matendo yenu.
16Maana, kama walivyokunywa kikombe cha ghadhabu yangu
kwenye mlima wangu mtakatifu
ndivyo na mataifa jirani yatakavyokunywa;
watakunywa na kupepesuka,
wataangamia kana kwamba hawakuwahi kuwapo duniani.
Waisraeli watashinda
17“Lakini mlimani Siyoni watakuwapo wale waliosalimika
nao utakuwa mlima mtakatifu.
Wazawa wa Yakobo wataimiliki tena nchi iliyokuwa yao.
18Wazawa wa Yakobo watakuwa kama moto
na wazawa wa Yosefu kama miali ya moto.
Watawaangamiza wazawa wa Esau
kama vile moto uteketezavyo mabua makavu,
asinusurike hata mmoja wao.
Mimi, Mwenyezi-Mungu, nimesema.
19Wale wanaokaa Negebu wataumiliki mlima Esau;
wale wanaokaa Shefela wataimiliki nchi ya Wafilisti.
Waisraeli watamiliki nchi za Efraimu na Samaria
na watu wa Benyamini wataimiliki nchi ya Gileadi.
20Waisraeli walio uhamishoni Hala
wataimiliki Foinike hadi Sarepta.
Watu wa Yerusalemu walio uhamishoni Sefaradi
wataimiliki miji ya Negebu.
21Waokoaji watapanda juu ya mlima Siyoni
ili kuutawala mlima Esau;
naye Mwenyezi-Mungu atakuwa ndiye Mfalme.”

Currently Selected:

Obadia 1: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy