YouVersion Logo
Search Icon

Maombolezo 3

3
Adhabu, toba na tumaini
1Mimi ni mtu niliyepata mateso
kwa fimbo ya ghadhabu yake Mungu.
2Amenichukua akanipeleka
mpaka gizani kusiko na mwanga.
3Amenyosha mkono wake dhidi yangu mimi tu,
akanichapa tena na tena mchana kutwa.
4Amenichakaza ngozi na nyama,
mifupa yangu ameivunja.
5Amenizingira na kunizungushia
uchungu na mateso.
6Amenikalisha gizani
kama watu waliokufa zamani.
7Amenizungushia ukuta nisitoroke,
amenifunga kwa minyororo mizito.
8Ingawa naita na kulilia msaada
anaizuia sala yangu isimfikie.
9Njia zangu ameziziba kwa mawe makubwa
amevipotosha vichochoro vyangu.
10Yeye ni kama dubu anayenivizia;
ni kama simba aliyejificha.
11Alinifukuza njiani mwangu,
akanilemaza na kuniacha mkiwa.
12Aliuvuta upinde wake,
akanilenga mshale wake.
13Alinichoma moyoni kwa mishale,
kutoka katika podo lake.
14Nimekuwa kitu cha dhihaka kwa watu wote,
mchana kutwa nimekuwa mtu wa kuzomewa.
15Amenijaza taabu,
akanishibisha uchungu.
16Amenisagisha meno katika mawe,
akanifanya nigaegae majivuni.
17Moyo wangu haujui tena amani,
kwangu furaha ni kitu kigeni.
18Nimewaza “Nimekata tamaa kabisa,
tumaini langu kwa Mwenyezi-Mungu limetoweka.”
19Kukumbuka taabu na kutangatanga kwangu
kwanipa uchungu kama wa nyongo.
20Nayafikiria hayo daima,
nayo roho yangu imejaa majonzi.
21Lakini nakumbuka jambo hili moja,
nami ninalo tumaini:
22Kwamba fadhili za Mwenyezi-Mungu hazikomi,
huruma zake hazina mwisho.
23Kila kunapokucha ni mpya kabisa,
uaminifu wake ni mkuu mno.
24Mwenyezi-Mungu ndiye hazina yangu
hivyo nitamwekea tumaini langu.
25Mwenyezi-Mungu ni mwema kwa wanaomtegemea,
ni mwema kwa wote wanaomtafuta.
26Ni vema mtu kungojea kwa saburi
ukombozi utokao kwa Mwenyezi-Mungu.
27Ni vema mtu kujifunza uvumilivu
tangu wakati wa ujana wake.
28Heri kukaa peke na kimya,
mazito yanapompata kutoka kwa Mungu.
29Yampasa kuinama na kujinyenyekesha,
huenda ikawa tumaini bado lipo.
30Yampasa kumgeuzia shavu mwenye kumpiga,
na kuwa tayari kupokea matusi yake.
31Mwenyezi-Mungu hatatutupa milele.
32Ingawa atufanya tuhuzunike,
atakuwa na huruma tena
kadiri ya wingi wa fadhili zake.
33Yeye hapendelei kuwatesa
wala kuwahuzunisha wanadamu.
34Wafungwa wote nchini
wanapodhulumiwa na kupondwa;
35haki za binadamu zinapopotoshwa
mbele yake Mungu Mkuu,
36kesi ya mtu inapopotoshwa mahakamani,
je, Mwenyezi-Mungu haoni hayo?
37Nani awezaye kuamuru kitu kifanyike
Mwenyezi-Mungu asipopanga iwe hivyo?
38Maafa na mema hutokea tu
kwa amri yake Mungu Mkuu.
39Kwa nini mtu anung'unike,
ikiwa ameadhibiwa kwa dhambi zake?
40Na tupime na kuchunguza mwenendo wetu,
tupate kumrudia Mwenyezi-Mungu.
41Tumfungulie Mungu huko mbinguni
mioyo yetu na kumwomba:
42“Sisi tulikukosea na kukuasi
nawe bado hujatusamehe.
43“Umejizungushia hasira yako ukatufuatia,
ukatuua bila huruma.
44Umejizungushia wingu zito,
sala yeyote isiweze kupenya humo.
45Umetufanya kuwa takataka na uchafu
miongoni mwa watu wa mataifa.
46“Maadui zetu wote wanatuzomea.
47Kitisho na hofu vimetuandama,
tumepatwa na maafa na maangamizi.
48Macho yangu yabubujika mito ya machozi
kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu.
49“Machozi yatanitoka bila kikomo,
50mpaka Mwenyezi-Mungu kutoka huko mbinguni
aangalie chini na kuona.
51Nalia na kujaa majonzi,
kuona yaliyowapata kina mama wa mji wangu.
52“Nimewindwa kama ndege
na hao wanichukiao bila sababu.
53Walinitupa shimoni nikiwa hai
na juu yangu wakarundika mawe.
54Maji yalianza kunifunika kichwa,
nami nikafikiri, ‘Huu ni mwisho wangu.’
55“Kutoka chini shimoni
nilikulilia ee Mwenyezi-Mungu.
56Wewe umenisikia nikikulilia:
‘Usiache kusikia kilio changu cha msaada
bali unipatie nafuu.’
57Nilipokuita ulinijia karibu
ukaniambia, ‘Usiogope!’
58“Umenitetea katika kisa changu ee Mwenyezi-Mungu,
umeyakomboa maisha yangu.
59Umeuona uovu niliotendewa ee Mwenyezi-Mungu,
uniamulie kwa wema kisa changu.
60Umeuona uovu wa maadui zangu,
na mipango yao yote ya hila dhidi yangu.
61“Umesikia matukano yao ee Mwenyezi-Mungu,
na mipango yao yote ya hila dhidi yangu.
62Maneno na mawazo ya maadui zangu siku nzima
ni juu ya kuniangamiza mimi.
63Wakati wote, wamekaa au wanakwenda,
mimi ndiye wanayemzomea.
64Uwalipize, ee Mwenyezi-Mungu
kadiri ya hayo matendo yao,
kadiri ya mambo waliyotenda wenyewe.
65Uipumbaze mioyo yao,
na laana yako iwashukie.
66Uwafuatie kwa hasira, uwaangamize,
uwafanye watoweke ulimwenguni.”

Currently Selected:

Maombolezo 3: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy