YouVersion Logo
Search Icon

Mathayo 1

1
Ukoo wa Yesu Kristo
(Luka 3:23-38)
1Yesu Kristo alikuwa wa ukoo wa Daudi, wa ukoo wa Abrahamu. Hii ndiyo orodha ya ukoo wake:
2Abrahamu alimzaa Isaka,
Isaka alimzaa Yakobo,
Yakobo alimzaa Yuda na ndugu zake,
3Yuda alimzaa Peresi na Zera (mama yao alikuwa Tamari),
Peresi alimzaa Hesroni,
Hesroni alimzaa Rami,
4Rami alimzaa Aminadabu,
Aminadabu alimzaa Nashoni,
Nashoni alimzaa Salmoni,
5Salmoni alimzaa Boazi (mama yake Boazi alikuwa Rahabu)
Boazi na Ruthu walikuwa wazazi wa Obedi,
Obedi alimzaa Yese,
6naye Yese alimzaa Mfalme Daudi.
Daudi alimzaa Solomoni (mama yake Solomoni alikuwa Bath-Sheba mke wa Uria).
7Solomoni alimzaa Rehoboamu,
Rehoboamu alimzaa Abiya,
Abiya alimzaa Asa,
8Asa alimzaa Yehoshafati,
Yehoshafati alimzaa Yoramu,
Yoramu alimzaa Uzia,
9Uzia alimzaa Yothamu,
Yothamu alimzaa Ahazi,
Ahazi alimzaa Hezekia,
10Hezekia alimzaa Manase,
Manase alimzaa Amoni,
Amoni alimzaa Yosia,
11Yosia alimzaa Yekonia na ndugu zake.
Huo ulikuwa wakati Wayahudi walipopelekwa uhamishoni Babuloni.
12Baada ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni Babuloni,
Yekonia alimzaa Shealtieli,
Shealtieli alimzaa Zerubabeli,
13Zerubabeli alimzaa Abiudi,
Abiudi alimzaa Eliakimu,
Eliakimu alimzaa Azori,
14Azori alimzaa Zadoki,
Zadoki alimzaa Akimu,
Akimu alimzaa Eliudi,
15Eliudi alimzaa Eleazari,
Eleazari alimzaa Mathani,
Mathani alimzaa Yakobo,
16Yakobo alimzaa Yosefu, mumewe Maria mama yake Yesu aitwaye Kristo.
17Basi, kulikuwa na vizazi kumi na vinne tangu Abrahamu mpaka Daudi, vizazi kumi na vinne tangu Daudi mpaka Wayahudi walipochukuliwa mateka Babuloni, na vizazi kumi na vinne tangu kuchukuliwa mateka mpaka wakati wa Kristo.
Kuzaliwa kwa Yesu
(Luka 2:1-7)
18Basi, hivi ndivyo Yesu Kristo alivyozaliwa: Maria, mama yake, alikuwa ameposwa na Yosefu. Lakini kabla hawajakaa pamoja kama mume na mke, alionekana kuwa mjamzito kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. 19Yosefu, mumewe, kwa vile alikuwa mwadilifu, hakutaka kumwaibisha hadharani; hivyo alikusudia kumwacha kwa siri. 20Alipokuwa bado anawaza jambo hilo, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akamwambia, “Yosefu, mwana wa Daudi, usiogope kumchukua Maria awe mke wako, maana amekuwa mjamzito kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. 21Atajifungua mtoto wa kiume, nawe utampa jina Yesu, kwa kuwa yeye ndiye atakayewaokoa watu wake katika dhambi zao.”
22Basi, haya yote yalitukia ili litimie lile neno Bwana alilosema kwa njia ya nabii:
23“Bikira atachukua mimba,
atamzaa mtoto wa kiume,
nao watampa jina Emanueli”
(maana yake, “Mungu yuko nasi”).
24Hivyo, Yosefu alipoamka usingizini alifanya kama malaika huyo alivyomwambia, akamchukua mke wake nyumbani. 25Lakini hakulala naye hata Maria alipojifungua mtoto wa kiume. Naye Yosefu akampa jina Yesu.

Currently Selected:

Mathayo 1: BHND

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy